HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, April 15, 2022

Dkt.Biteko: Wizara itaendelea kuwasikiliza wadau wake

 


WAZIRI wa Madini, Dkt.Doto Biteko amesema, wizara yake itaendelea kuwasikiliza wadau wote wa Sekta ya Madini ili kuzungumza kwa pamoja kuhusu shughuli za madini

Ameyasema hayo Aprili 14, 2022 wakati akizungumza na Viongozi wa Chama cha Mabroka Tanzania (CHAMATA) alipokutana nao kuzungumza kuhusu ukuaji na usimamizi wa sekta ndogo ya biashara ya madini katika Ukumbi wa Msekwa Bungeni Jijini Dodoma.

Dkt.Biteko amesema kuwa, Wizara ya Madini imekuwa ikikutana na wadau wote wa Sekta ya Madini kupitia maonesho mbalimbali ya madini na mikutano inayofanyika hapa nchini ili kuwasikiliza na kuzungumza nao kuhusu changamoto mbalimbali za sekta na kuzitafutia majawabu.

Ameongeza kuwa, wizara inatarajia kuendelea kukutana na makundi maalum mbalimbali ili kuwasikiliza na kutatua changamoto kwa pamoja na kuwataka CHAMATA washikamane katika umoja wao Ili kuwa na sauti ya pamoja kama ilivyo kwa vyama vingine vilivyopo katika Sekta ya Madini.

Dkt. Biteko amewataka CHAMATA kuimarisha umoja wao na kuhakikisha wanakisajili chama chao ili kiwe chama imara kabla hawajapeleka malalamiko yao kwa Serikali.

"Nimefurahi mno, hamna mtu aliyewashawishi kuunda chama, nyie wenyewe mmeamua kuunda hicho chama, nendeni mkakisimamie vizuri, "amesema Dkt.Biteko.

Akizunguzia kuhusu utoroshaji wa madini unaofanywa na wafanyabiashara wasio waaminifu, Dkt.Biteko amewataka CHAMATA kuwa mabalozi kwa wafanyabiashara wenzao katika kuhamasisha kuacha kutorosha madini.

Amesema, Serikali imeweka Masoko ya Madini ili kuondoa urasimu na kuongeza kuwa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan akiwa Mwanza aliagiza watu wapeleke madini yao kwenye masoko kutoka sehemu yoyote na wauze bila kusumbuliwa.

"Ninataka kutumia nafasi hii kuwaomba wale wote tuliopewa dhamana ya kusimamia Sekta ya Madini, wale watu ambao wanapeleka madini sokoni wasisumbuliwe, mtu asipate msukosuko, aone raha ya kwenda sokoni, soko liwe mahali pa kimbilio la wachimbaji, "amesisitiza Dkt. Biteko.

Naye, Mwenyekiti wa CHAMATA, Bw. Jeremia Kituyo amesema kuwa, CHAMATA inataka kuona Sekta ya Madini inakuwa na mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa ili Tanzania inufaike ipasavyo na rasilimali ya madini nchini.

Aidha, Kituyo ameishukuru wizara kwa uanzishwaji wa Masoko ya Madini nchini ambayo yamekuwa na mchango mkubwa kwa wafanyabiashara wa madini.

kikao hicho, kilihudhuriwa na watendaji mbalimbali kutoka Tume ya Madini na Wizara ya Madini ikiwa ni mwendelezo wa Waziri wa Madini kukutana na kuzungumza na wadau mbalimbali kuhusu Sekta ya Madini

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad