HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, March 2, 2022

UNESCO, ILO zafunda nchi 4 namna ya kumaliza unyanyapaa kwa walemavu


KIKAO kazi cha  kimataifa  cha wataalamu toka mashirika yasiyo ya kiserikali, serikali na mashirika ya watu wenye ulemavu kinachohusu mbinu za kukomesha unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wenye ulemavu kimeanza kufanyika  mjini Dodoma huku wataalamu waliobobea wakishawishi elimu itakayowawezesha walemavu hao kujitegemea.

Aidha kikao kazi hicho pia kinapitia mpango kazi wa mradi unaotekelezwa na UNESCO na ILO Kupitia mradi unaofadhiliwa na United Nations Partnership on the Rights of Persons with Disabilities (UNPRPD) wenye lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi wa watu wenye ulemavu katika vyuo vya ufundi na kazini.

Majadiliano yalilenga zaidi katika kuhakikisha kwamba wanadamu wanavunja mzunguko wa umaskini na kutengwa kwa watu wenye ulemavu.

Kongamano hilo lililohusisha watu kutoka Tanzania, Msumbiji, Namibia na Zimbabwe lilioanza Februari 28 hadi Machi 4 liliambiwa kwamba dunia ina watu zaidi ya bilioni 1 wenye aina tofauti za ulemavu huku asilimia 80 ya walemavu wote wanaishi katika nchi zinazoendelea.

Katika mazungumzo ambayo mengine yalifanyika kwa njia ya video, ilielezwa na  Mtaalamu  wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Unesco)  anayeshughulikia masuala ya jamii na sayansi ya binadamu, Ofisi ya Kanda Nairobi, David Ochieng Onyango, kuwa  nchini Zimbabwe, watu wenye ulemavu wanawakilisha asilimia 9 ya watu wote huku nchini Tanzania watu milioni mbili wanaishi na ulemavu.

Kwa mujibu wa mada iliyotolewa Onyango idadi hiyo ni sawa na asilimia 5.8 ya watu wote nchini, huku asilimia 50 yao hawawezi kumudu huduma za afya huku wanawake wenye ulemavu wakiwa na uwezekano wa mara 2 au zaidi kunyanyaswa kingono kuliko wanawake wasio na ulemavu.

Katika kongamano hilo pamoja na washiriki kulielezwa kuwa miongoni mwa Malengo 7 ya SDGs yanarejelea kwa uwazi watu wenye ulemavu huku ikielezwa kuwa suluhu ya maisha bora kwao ni kuwapatia masomo yanayohusiana na ufundi kwa vitendo (TVET) na kupatikana kwa ajira.

"Watu hawa wenye ulemavu wanaendelea kuachwa nyuma na hii imetokana na masuala kadhaa, ikiwa ni pamoja na imani hasi za kitamaduni, kidini na fikra potofu ambazo bado zipo miongoni mwa jamii," alisema Onyango.

Katika kongamano hilo lilipata nafasi ya kuelimishwa kuhusu mradi wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (UNPRPD) wenye lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi na kuvunja mzunguko wa umaskini na kutengwa kwa watu wenye ulemavu kwa mataifa ya Msumbiji, Namibia, Tanzania na Zimbabwe.

Mradi huo ulioshirikisha mashirika ya UNESCO  na ILO wenye lengo la kusaidia nchi hizo kuunda na kujaribu kwa pamoja mifumo na zana zinazoweza kusaidia walemavu kwenye taasisi za Ufundi Stadi na Mafunzo (TVET), waajiri, wafanyakazi na mashirika ya waajiri kuelewa kwa pamoja na kushughulikia mifumo ya unyanyapaa na ubaguzi ambayo kuwepo kwa watu wenye ulemavu.

"Lengo la kuboresha uwezo wa watu wenye ulemavu kupata programu za TVET na kazi zenye staha kwa kubadilisha kanuni za kitamaduni, kijamii na kidini zinazochochea unyanyapaa na ubaguzi." Alisema Onyango.
 
Mtaalamu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO)  anayeshughulikia masuala ya jamii na sayansi ya binadamu, Ofisi ya Kanda Nairobi, Bw. David Ochieng Onyango akiwasilisha mada wakati wa Kikao kazi cha kimataifa cha wataalamu toka mashirika yasiyo ya kiserikali, Serikali na mashirika ya watu wenye ulemavu kwa lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wenye ulemavu kilichoratibiwa na UNESCO na ILO kwa ufadhili wa mradi wa Shirika la Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (UNPRPD) kinachoendelea mjini Dodoma.
Mkuu wa kitengo cha Elimu ofisi ya UNESCO nchini, Bi Faith Shayo akisambaza nakala za mawasilisho ya mada wakati wa kikao kazi cha kimataifa cha wataalamu kutoka mashirika yasiyo ya kiserikali, Serikali na mashirika ya watu wenye ulemavu kwa lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wenye ulemavu kilichoratibiwa na UNESCO na ILO kwa ufadhili wa mradi wa Shirika la Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (UNPRPD) kinachoendelea mjini Dodoma.
Baadhi ya wadau kutoka mashirika yasiyo ya kiserikali, Serikali na mashirika ya watu wenye ulemavu walioshiriki kikao kazi chenye lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wenye ulemavu kilichoratibiwa na UNESCO na ILO kwa ufadhili wa mradi wa Shirika la Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (UNPRPD) kinachoendelea mjini Dodoma.
Picha ya pamoja ya wadau kutoka mashirika yasiyo ya kiserikali, Serikali na mashirika ya watu wenye ulemavu walioshiriki kikao kazi chenye lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wenye ulemavu kilichoratibiwa na UNESCO na ILO kwa ufadhili wa mradi wa Shirika la Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (UNPRPD) kinachoendelea mjini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad