HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, March 5, 2022

MKUU WA MAJESHI AWASAMEHE VIJANA WA JKT 853

Kaimu Mkurugenzi wa habari na Uhusiano na Msemaji Mkuu Jeshi la wananchi (JWTZ), Luteni Kanali Gaudentius Ilonda, akizungumza na waandishi wa habari makao Makuu ya zamani ya jeshi hilo Upanga Ngome jijini Dar es Salaam leo Machi 5,2022.

MKUU wa Majeshi ya ulinzi Nchini, Jenerali Venance Mabeyo ametoa Msamaha kwa vijana 853 kati ya 854 walifanya vitendo vya kukiuka nidhamu jeshini na kuamuru kuwa vijana hao wote warejeshwe katika makambi ya jeshi la kujenga Taifa tayari kwa kuendelea na mafunzo yao.

Amegiza kuwa Vijana hao wote 853 wapokelewa katika Kambi ya kujenga Taifa kikosi namba 841 iliyopo Mafinga mkoani Iringa Machi 12,2022 huku taratibu zingine wataelekezwa baada ya kupokelewa huku mwenzao mmoja akiwa alishafariki

Akitoaa taarifa hiyo leo Machi 5, 2022 Kaimu Mkurugenzi wa habari na Uhusiano na Msemaji Mkuu Jeshi la wananchi (JWTZ), Luteni Kanali Gaudentius Ilonda, makao Makuu ya zamani ya jeshi hilo Upanga Ngome jijini Dar es Salaam amesema, Mabeyo ametoa msamaha huo baada ya uchunguzi na utafiti uliofanywa kwa kina na jeshi hilo na kubaini sababu ambazo zilifanywa na vijana hao.

Amezitaja sababu hizo kuwa vijana wengi walifanya vile kutokana na utoto wao na kutojitambua huku ikidhirika kuwa wengine walifanya vile kwa kurubuniwa na wengine walifanya vitendo hivyo kwa kufuata Mkumbo.

"JWTZ imefanya uchunguzi kwa vijana hao kila mmoja mahali alipo walipokatiswa mafunzo hadi kufikia sasa, jeshi limekwenda mkoa kwa mkoa, Wilaya kwa Wilaya tarafa kwa tarafa na kata kwa kata hadi vijijjni na kujiridhisha kwamba vijana hao wamechunguzwa hadi kwa ngazi ya familia bila familia na vijana wenyewe kujua nini kinaendelea." Amesema Luteni Kanali Ilonda.

Amesema, baada ya uchunguzi huo, JWTZ imejiridhisha pasipo na shaka kwamba vijana hao kwa sasa mwenendo wao ni wa kuridhisha na wanastahili msahama waliopatiwa na hivyo ameomba Umma wa watanzania kuendelea kuwaamini vijana hao na tuwe tayari kuwapa nafasi nyingine waendelee na mafunzo yao.

Aidha JWTZ imesisitiza kuwa vijana wanaohusika kurudi kambini ni wale tu walioachishwa mafunzo na kufukuzwa kutokana na sababu za makosa ya nidhamu na kurejeshwa makwao mwaka jana.

Aidha jeshi limewataka wale wote wasiohusika na msamahama huu kutojaribu kudangaya kwani Jeshi limeenda mbali zaidi kwa kujua kuwa katika msafara wa namba na kenge watajipenyeza hivyo amewataadharisha vijana wengine ambao hawausiki na msamahama huo kwa orodha yote ya vijana imeandaliwa huku kukiwa na picha zao pamoja na Makundi yao ya damu hivyo udanganyifu hautakuwepo.

Aidha ameiomba Umma wa watanzania kuacha vitendo vya kuwarubuni vijana hawa hasa wanapokuwa katika mafunzo yao kule kwenye Kambi za kujenga Taifa, waachwe wapatiwe mafunzo ya stadi za maisha ili waje kulitumikia Taifa lao kwa moyo mmoja.

Mapema Mwaka jana Aprili 17, 2021 Mkuu wa majeshi nchini Tanzania, Jenerali Venance Mabeyo aliwafukuza vijana 854 wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) waliokiuka taratibu kwa kuanzisha mgomo na kuandamana kwenda Ikulu wakishinikiza kuajiriwa jeshini.

"Aprili 8, 2021 vijana wetu wa JKT wapatao 854 walianzisha mgomo, kukataa kufanya kazi maeneo mengine na kufanya maandamano kwenda Ikulu kwa madai ya kutaka kumuona Rais ili wadai kuandikishwa jeshini kama walivyoahidiwa na aliyekuwa rais wa Tanzania, John Magufuli."

Vijana hao ni kati ya vijana 2400 walioahidiwa kuandikishwa Jeshini na walifanya uamuzi huo baada ya jeshi kuamua kuwapunguza katika kazi ya ujenzi wa Ikulu Chamwino baada ya kazi kupungua ili waende kufanya kazi katika maeneo mengine lakini wao wakapinga kwa madai wangekosa kuandikishwa jeshini.

JWTZ halikuwa na lengo hilo na walilazimika kusitisha mikataba yao kwa kuwa kosa walilolifanya ni sawa na uasi na ulikuwa hauvumiliki.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad