HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, March 25, 2022

Mkurugenzi TEA awapa neno wahitimu kidato cha sita

 Na Mwandishi Wetu, Sengerema

WAHITIMU wa kidato cha sita wametakiwa kusoma kwa bidii ili waweze kuitumikia nchi yao kwa uzalendo katika fani mbalimbali baadaye.

Ushauri huo ulitolewa jana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Bahati Geuzye, alipokuwa mgeni rasmi kwenye mahafali ya 33 ya Kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Sengerema Mkoani Mwanza.

Jumla ya wanafunzi 576 kutoka tahasusi 10 za Sayansi, Biashara na Sanaa wanatarajia kuhitimu masomo hayo Mwezi Mei shuleni hapo.

“Mnapaswa kujiandaa vya kutosha kwasababu taifa linawategemea mje kuilitumika kwenye fani mbalimbali hivyo hakikisheni mnafaulu kwa viwango vya juu sana,” alisema

Alisema ili taifa liweze kusonga mbele kwa kasi kiuchumi linapaswa kuwa na wasomi waliobobea kwenye taaluma mbalimbali badala ya kutegemea wataalamu kutoka mataifa mengine.

Aliwataka wanafunzi hao kujifunza uzalendo na uaminifu kwa nchi yao ili watakapopata kazi mara baada ya kumaliza shule waiwezeshe nchi kupiga hatua kubwa kimaendeleo kwa kasi.

Aidha, aliupongeza uongozi wa shule na wanafunzi wa shule hiyo kwani takwimu zinaonyesha kuwa imekuwa ikifanya vizuri kitaaluma mwaka hadi mwaka na aliwataka wasibweteke na mafanikio hayo.

“Mmekuwa mkifanya vizuri nawaomba muendelee kufanya vizuri zaidi na ikiwezekana muwe kwenye 10 bora kitaifa mwaka huu na naamini mkiweka nia mtafanikiwa kufika kwenye kumi bora,” alisema

Shule ya Sekondari Sengerema yenye wanafunzi 1,306 ni miongoni mwa shule 17 kongwe za sekondari ambazo zilikarabatiwa kwa uratibu wa TEA na imeshatumia Sh bilioni moja kukarabati shule hiyo mwaka 2017/2018.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), Bahati Geuzye akimkabidhi cheti mmoja wa wahitimu wa kidato cha sita wa shule ya sekondari Sengerema mkoani Mwanza alipokuwa mgeni rasmi juzi.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Bahati Geuzye akiwasili kwenye mahafali ya 33 ya Kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Sengerema Mkoani Mwanza. 
(PICHA: MPIGA PICHA WETU)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad