HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, November 17, 2021

MKUU WA WILAYA YA TUNDURU AKABIDHI HUNDI KWA VIKUNDI VYA BODABODA

 Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma Julius Mtatiro wa nne kushoto akikabidhi mfano wa hundi kwa viongozi wa kikundi cha Bodaboda wakati wa hafla ya kukabidhi mikopo kwa vikundi vya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu ,wa pili kulia Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri Chiza Malando.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Tunduru mkoani Ruvuma Chiza Malando akiongea jana wakati wa hafla ya kutoa mikopo kwa vikundi vya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu katika wilaya hiyo ambapo zaidi ya Sh milioni 103 zimetolewa,katikati MKuu wa wilaya ya Tunduru Julius Mtatiro.

Na Muhidin Amri, Tunduru
HALMASHAURI ya wilaya Tunduru mkoani Ruvuma kupitia bajeti ya mapato ya ndani imetenga Sh. milioni 264,570,167.88 sawa na asilimia 10 kama mikopo kwa ajili ya kuviwezesha vikundi 20 vya kimkakati vya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu.

Fedha hizo ni utekelezaji wa sera,miongozo na maagizo mbalimbali yanayohusu uwezeshaji wa mikopo isiyo na riba kwa vikundi hivyo katika mwaka wa fedha 2021/2022.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wilaya ya Tunduru Jacelyne Mganga wakati wa utoaji mikopo ya Sh. milioni 103 kwa makundi hayo maalum.

Alisema, fedha hizo ni kwa ajili ya kuendeleza viwanda vidogo vinavyojishughulisha na ushonaji,usindikaji,useremala,uchomeaji,Bodaboda na kilimo cha kimkakati cha mazao ya chakula na biashara.

Alisema, vikundi vilivyopata mikopo ni vyenye sifa ambapo Sh.milioni 50 fedha zilizotokana na asilimia 10 ya robo ya kwanza ya mwaka 2021/2022 na Sh.milioni 53 ni fedha zilizotokana na marejesho kutoka kwa makundi hayo.

Aidha alisema, kwa siku za usoni Halmashauri inakusudia kufanya maamuzi magumu ya kupeleka fedha za mikopo kwa vikundi vilivyo na miradi endelevu inayofanya kazi, badala ya fedha hizo kupeleka kwa vikundi vilivyobuni mradi.

Kwa mujibu wa Mganga,hatua hiyo ni baada ya kubaini miongoni kuwa changamoto za marejesho ya mikopo imevikumba vikundi vingi vilivyobuni miradi kushindwa kutekeleza na hatimaye kushindwa kurejesha mikopo kwa wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya Tunduru Chiza Malando alisema, Halmashauri ya wilaya imetenga kiasi cha Sh.milioni 264,570,167.88 kukopesha makundi maalum ya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

Hata hivyo alisema, katika utekelezaji wa mpango huo changamoto kubwa ni urejeshaji wa mikopo hiyo kwa baadhi ya vikundi jambo lililoifanya Halmashauri kuchukua hatua ya kuwapeleka mahakamani wana vikundi walioshindwa au kuchelewa kurudisha mikopo.

Malando amewaomba wana vikundi waliopata fedha hizo, kuhakikisha wanakwenda kuzifanya kazi iliyokusudiwa na wanarejesha kwa wakati ili ziweze kukopeshwa kwa vikundi vingine vyenye mahitaji.

Mkuu wa wilaya ya Tunduru Julius Mtatiro amewaasa wana vikundi kuupokea mkopo huo na kurejesha kwa wakati ili vikundi vingine viweze kunufaika.

Mtatiro, amepiga marufuku tabia ya baadhi wana vikundi kugawana fedha hizo na kutekeleza mradi wa mtu mmoja mmoja kwani ni hatari kwa kuwa vikundi vingi vinashindwa kurejesha kwa taratibu zilizotumika awali.

Aidha alisema, kumekuwa na malalamiko mbalimbali kutoka katika wana kikundi hususani baadhi ya watu kuitaji fedha za mkopo na kutumia bila ya utaratibu hivyo kusababisha vikundi vingi kusambaratika.
Baadhi ya wanavikundi waliopata mikopo ya vijana,wanawake na watu wenye ulemavu kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya Tunduru, wakicheza muziki baada kupata mikopo yenye thamani ya Sh.milioni 103 iliyotolewa na Halmashauri ya wilaya Tunduru.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad