HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, November 5, 2021

MFUMO MPYA WA KIELETRONIKI WA MALIPO YA ADA YA MAEGESHO WABORESHWA

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Ummy Mwalimu (wa katikati) akizungumza na Waandishi wa Habari, Watendaji wa TARURA wakati akitangaza Mfumo mpya wa Kieletroniki uliosimikwa ambao utaanza kutumika tena Desemba Mosi, 2021 baada ya Mfumo wa awali kulalamikiwa na Wananchi wengi katika maeneo mbalimbali. Wa pili kulia ni Mtendaji Mkuu wa TARURA, Mhandisi Victor Seff.

Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV
SERIKALI imesema kuwa mfumo wa Kieletroniki wa malipo ya ada ya maegesho utaanza tena kutumika Desemba Mosi 2021 baada ya kujitokeza changamoto mbalimbali katika mfumo wa awali uliosimikwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Ummy Mwalimu amesema Oktoba 9, 2021 alisitisha kwa muda matumizi ya mfumo wa zamani wa TARURA baada ya kuwepo malalamiko kwa Wananchi waliokuwa wanatumia Mfumo huo husika hususani maeneo ya Dar es Salaam.

Waziri Ummy amesema mfumo huo mpya ulioundwa na TARURA umeboreshwa kwa kiasi kikubwa ili kuondoa kero na changamoto za awali zilizojitokeza kwa Watumiaji ikiwemo changamoto ya Wananchi hao kufungiwa Minyororo kwenye Magari yao, kuokoa muda katika kulipa ushuru wa maegesho, Ukwepaji kulipa Kodi na kurahisisha ukusanyaji wa ushuru.

“Mfumo huu ni wa Kieletroniki na ni mpya, kwa sasa Wananchi watapata taarifa za kudaiwa ushuru kwa wakati sahihi, Pia Wateja watapatiwa Ankara itakayoonyesha muda, kiasi anachodai, tarehe na eneo husika”, amesema Waziri Ummy.

“Kero kubwa ilikuwa gharama ya maegesho kuwa kubwa, kanuni zimeboreshwa, kwa mfano kwenye Jiji la Dar es Salaam watumiaji watatozwa kulipia kiasi cha Shilingi 500/- kwa saa na kiasi cha Shilingi 2,500/- kwa siku, tofauti na zamani Shilingi 500 /- kwa saa na Shilingi 4,500/- kwa siku”, ameeleza

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor Seff amesema TARURA wanahusika zaidi kwenye eneo la Hifadhi za Barabara zilizo chini ya Wakala huo, amesema nje ya hapo hawahusiki na usimamizi wa ukusanyaji wa malipo ya ushuru.

“Mfano kwa hapa Dar es Salaam, kwenye Kituo cha Mabasi Mbezi Luis, nje ya Hifadhi za Barabara TARURA haiusiki na ukusanyaji ushuru. Hata Mlimani City sisi hatuusiki kabisi katika ukusanyaji ushuru”, amesema Mhandisi Seff

Kuhusu suala la kutotoa risiti, Mhandisi Seff ameeleza kuwa suala hilo watalifuatilia kwa ukaribu ili kuhakikisha Risiti zinatolewa kwa Watumiaji wa maeneo hayo ya maegesho pale watakapolipa ada.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad