HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 23, 2021

VIONGOZI NKASI SIMAMIENI MIRADI ILI IWE ENDELEVU- LT. MWAMBASHI

 

 

Kiongozi wa Mbio Maalum za Mwenge  wa Uhuru Luteni Josephine Mwambashi amewaelekeza viongozi wa wilaya ya Nkasi kuongeza kasi katika usimamizi wa miradi ya maendeleo iwe endelevu kufuatia serikali na wananchi kutoa fedha nyingi.

Ametoa kauli hiyo wakati Mwenge wa Uhuru ulipofanya kazi ya kutembelea, kuzindua na kukagua miradi ya ujenzi wa zahanati kijiji cha Masheta, barabara za Namanyele Mjini, mradi wa maji wa kijiji cha Kantawa na shamba bora la mfano la kahawa kijiji cha Kasu.

Luteni Mwambashi alibainisha lengo la mbio za Mwenge wa Uhuru kuwa ni kukagua na kuona namna nguvu za wananchi zinavyofanya kazi ikiwemo fedha zinazotolewa na serikali ili kuhakikisha zinatumika kwa ajili ya kuongeza kasi ya maendeleo ya wananchi.

“Mwenge wa Uhuru unaagiza viongozi wa wilaya hii kuhakikisha mapungufu yaliyojitokeza kwenye usimamizi wa miradi baadhi ikiwemo mitaro ya barabara za Nkasi kujaa uchafu hatua za kusafisha kuanzia leo zianze mara moja” alisisitiza Luteni Mwambashi.

Aidha Kiongozi huyo wa Mwenge wa Uhuru akiwa katika zahanati ya kijiji cha Mashete aliuagiza uongozi wa halmashauri ya Nkasi kujenga haraka kichomea taka ili kudhibiti uchafu kusambaa pia kuwekwa kwa  marumaru kwenye sakafu za zahanati hiyo kabla mwezi Octoba haujaisha.

Akizungumza kuhusu maelekezo hayo ,Mkuu wa Wilaya ya Nkasi Peter Lijuakali alisema atasimamia kwa karibu utekelezaji wa maagizo na ushauri uliotolewa na mbio za Mwenge wa Uhuru ili wananchi wawe na uhakika wa upatikanaji huduma.

Lijuakali aliongeza kusema mwenge wa uhuru ukiwa wilaya ya Nkasi umezindua miradi (3), umeweka jiwe la msingi (1) na umekagua miradi (4) ambapo yote imegharimu shilingi 1, 388, 630,068.

Mkuu huo alitaja mchanganuo wa gharama hizo kuwa halmashauri imechangia shilingi 24,300,900, wahisani shilingi 4,526,000, wananchi shilingi 66,004,600 na serikali kuu imetoa shilingi 1,293,798,568 ivyo kufanyia juma ya fedha zote kuwa shilingi 1,388,630,068.

Mwenge wa Uhuru umekamilisha mbio zake mkoa wa Rukwa leo ambapo ulikimbizwa kwenye wilaya za Sumbawanga, Kalambo na Kasi na kesho utakabidhiwa kwa uongozi wa mkoa wa Katavi.

Mbunge wa Nkasi Kusini Vicent Mbogo akiwa amebeba juu ndoo ya maji mara baada ya Mwenge wa Uhuru kuzindua mradi wa maji mserereko katika kijiji cha Kantawa wilaya ya Nkasi.
Shamba la mfano la mkulima Mfwele Farm lenye ukubwa wa ekari 1.7 ambalo amepanda miche bora ya kahawa 1250 ambalo Mwenge wa Uhuru umelikagua lililopo kijiji cha Kasu ambalo linatumika kama shamba darasa kwa wakulima wengine.
Mkuu wa Wilaya ya Nkasi Peter Lijuakali (kulia) akishukuru mara baada ya Kiongozi wa Mbio Maalum za Mwenge wa Uhuru Luteni Josephine Mwambashi (kushoto) kukagua shamba la ekari 1.7 la mfano la kahawa katika kijiji cha Kasu.
Baadhi ya nyumba nne za walimu wa shule ya sekondari Milundikwa zilizojengwa kwa shilingi milioni 129 ambapo serikali ilitoa shilingi milioni 100 kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) mwaka 2018 . Nyumba hizo zimezinduliwa na Mwenge wa Uhuru ulipotembelea wilaya ya Nkasi.


( Habari na Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa)

 

 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad