HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 22, 2021

TANROADS SAFISHENI MADARAJA KABLA YA MVUA- PROF. MBARAWA

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, amewataka mameneja wa Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), kuhakikisha wanaondoa mchanga  na takataka chini ya  madaraja ili mvua  zitakaponyesha kuepuka mafuriko.

Amewataka kutumia daraja la Kiyegeya kama funzo katika kuhakikisha wanasimamia vema miundombinu ya barabara na madaraja nchini kote ili kuepuka athari zinazoweza kuzuilika.

Akikagua maendeleo ya ujenzi wa daraja la Kiyegeya ambalo ujenzi wake umefikia asilimia 81, Prof. Mbarawa amemtaka mkandarasi anayejenga daraja hilo kulikamilisha haraka kabla ya msimu wa mvua kuanza.

“Daraja hili ni muhimu kwa uchumi wa nchi yetu kwani licha ya kuunganisha Mikoa ya Dar es salaam, Pwani na Morogoro na Mji mkuu Dodoma pia ni  kiungo muhimu  kwa mikoa ya Kanda ya Ziwa, na nchi jirani za Rwanda na Burundi na ambazo hutegemea sana barabara hii katika usafirishaji wa abiria na mizigo”, amesema Prof Mbarawa.

Waziri huyo ameitaka TANROADS kuimarisha   kitengo chake cha ufuatiliaji ili kubaini barabara na madaraja yenye viashiria vya kubomoka na kuvikarabati kwa wakati.

Naye, Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoani Morogoro, Mhandisi Baraka Mwambage, amemhakikishia  Prof. Mbarawa kuwa ujenzi wa mradi  huo umefikia asilimia 80,  na kwamba kazi ya  kuchimba msingi, nguzo zote 270, nguzo za juu mbili, na ujenzi wa kitanda cha daraja umekamilika.

Amesema kazi ya kujenga barabara za maingilio yenye urefu wa kilomita moja inaendelea na imekamilika kwa asilimia 65.

Ujenzi wa daraja jipya la Kiyegeya unafuatia kubomoka kwa daraja la zamani takribani miezi 18 iliyopita na hivyo kusababisha Serikali kujenga daraja la muda katika eneo hilo ambalo linaendelea kutumika hadi sasa.

Mwonekano wa Daraja la Kiyegeya linalounganisha mkoa wa Morogoro na Dodoma ambalo  ujenzi wake  umefikia asilimia 81 na linatarajiwa kukamilika  mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka  huu.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (katikati), akikagua Mpangokazi wa ujenzi wa daraja la Kiyegeya ambalo  Ujenzi wake unatarajia kukamilika mwezi Oktoba mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad