HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 23, 2021

Milioni 700 za ujenzi wa barabara vijijini , Karagwe wamshukuru Rais Samia


Serikali imetoa Shilingi milioni 700 kusaidia ukarabati wa barabara za vijijini katika jimbo la Karagwe mkoani Kagera ili kuboresha miundombinu ya jimbo hilo hatua inayosaidia kurahisisha mawasiliano na kuboresha huduma za kijamii jimboni humo.

 

Akiwa ziarani jimboni humo kukagua miundombinu ya barabara zinazokarabatiwa, Mhe. Innocent Bashungwa amesema fedha zilizotolewa kwa ajili ya ukarabati wa barabara jimboni humo zitumike kulingana na malengo yaliyokusudiwa kwa kuzingatia matumizi sahihi ya fedha zilizotolewa.

 

Mhe. Bashungwa amewahimiza wabunge wenzake mkoani Kagera kuwa mstari wa mbele kufanya ukaguzi wa mara kwa mara ili fedha iliyotolewa na Serikali kwa ajili ya kuboresha barabara za vijijini zifanye kazi iliyokusudiwa kufikia malengo ya kuwahudumia wananchi kwa kuboresha uchumi wao na taifa kwa ujumla.

 

“Sisi tunamshukuru Mhe. Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kutupa kiasi hiki kikubwa cha fedha ili tuboreshe barabara kwenye majimbo yetu lakini wito wangu ni kwamba hawa wataalumu wasisubiri mbunge aende site ili kuwaambia eneo fulani mlitakiwa muweke mataleo au mitaro ya maji ili yasiaharibu barabara, wataalamu wenyewe wanatakiwa wajue tangu wanaposanifu ujenzi husika” alisema Mhe. Bashungwa.

 

Akizungumzia hatua hiyo meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini TARURA wilaya ya Karagwe Bw. Kalimbula Malimi amesema baada ya ziara hiyo sehemu zote zilizoainishwa ambazozinahitaji marekebisho zitafanyia kazi haraka iwezekanavyo.

 

Katika ziara hiyo Mhe. Bashungwa aliambatana na Madiwani wa kata mbalimbali, watendaji wa TARURA na TANROAD ambapo ameleza kushutushwa kwake na namna mkandarasi anayetekeleza ukarabati wa barabara yenye urefu wa kilometa 96 inaanzia kata ya Nyakahanga kwenda kata za Nyabiyonza, Bweranyange, Nyakakika, Nyakabanga, Kibondo mpaka Lukanja ambayo imejengwa bila kuweka matoleo ya maji na mitaro ya barabara.

 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi wa wilaya ya Karagwe akiwemo diwani wa kata ya Nyakakika Mhe. Exsavery Buguzi wameeleza matarajio yao kuwa kukamilika kwa barabara hiyo kutaongeza urahisi wa shughuli za biashara kwa maana ya usafiri na kusafirisha mizigo kati ya wakazi wa mkoa wa Kagera na nchi jirani ya Rwanda kupitia kivuko cha  Bweranyange ambacho kinaziunganisha nchi hizo mbili kwa usafiri wa majini.

 

Vile vile, wakazi wa Karagwe wanaamini kukamilika kwa barabara hiyo kutaongeza urahisi kwa watalii kufanya shughuli za utalii wilayani humo katika mbuga mpya mbalimbali ikiwemo, Karagwe, Lumanyika, Ibanda na Burigi Chato.

Mbunge wa jimbo la Karagwe Mhe. Innocent Bashungwa katikati aliyevalia kofia ya kijani akionesha moja ya eneo linalohitaji kufanyiwa marekebisho wakati alipofanya ziara ya kukagua mwenendo wa ukarabati wa barabara yenye urefu wa kilometa 96 inayofanyiwa ukarabati katika jimbo lake. Wa kwanza kushoto ni meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini TARURA wilaya ya Karagwe Kalimbula Malimi, wa pili ni diwani wa kata ya Nyakakika Mhe. Exsavery Buguzi na wa kwanza kulia ni Ivo Ndisanye Katibu wa mbunge na Samson Mushi mkaguzi wa barabara mkoa wa Kagera TANROADS.
Mkaguzi wa barabara mkoa wa Kagera TANROADS Samson Mushi akimuelezea jambo

 Mbunge wa jimbo la Karagwe Mhe. Innocent Bashungwa katikati aliyevalia kofia ya kijani wakati alipofanya ziara ya kukagua mwenendo wa ukarabati wa barabara yenye urefu wa kilometa 96 inayofanyiwa ukarabati katika jimbo la Karagwe mkoani Kagera.

Mbunge wa jimbo la Karagwe Mhe. Innocent Bashungwa aliyevalia kofia ya kijani akihoji jambo kwa wataalam wa TANROAD na TARURA wakati wa ziara yake ya kukagua mwenendo wa ukarabati wa barabara yenye urefu wa kilometa 96 inayofanyiwa ukarabati katika jimbo la Karagwe.
Mbunge wa jimbo la Karagwe Mhe. Innocent Bashungwa katikati aliyevalia kofia ya kijani akiwasikiliza wakazi wa Kata ya Nyabiyonza wakati wa ziara yake ya kukagua mwenendo wa ukarabati wa barabara yenye urefu wa kilometa 96 inayofanyiwa ukarabati katika jimbo lake.
Baadhi ya barabara inayofanyiwa ukarabati kwa kiwango cha Moramu kuanzia kata ya Nyakahanga kwenda kata za Nyabiyonza, Bweranyange,  Nyakakika, Nyakabanga, Kibondo mpaka Lukanja .

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad