HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 17, 2021

Zaidi ya wajasiriamali 100 sasa kuanza kumiliki viwanda kupitia mpango wa Kampuni ya Kamal

Mwenyekiti wa Kampuni ya Kamal Bw. Gagan Santosh Gupta akizungumza na wajasiriamali zaidi ya 100 wa kubangua korosho jijini Dar es Salaam jana. Kulia ni Meneja wa Rasilimali watu wa Kampuni ya Kamal, Bi Emma Mwema. 
 
========== ==========    ===========
 
Dar es Salaam. Zaidi ya wajasiriamali 100 sasa watamiliki viwanda vya kubangua korosho.

Upatikanaji wao umewezeshwa na mpango maalumu wa kuongeza ubanguaji wa korosho unaosimamiwa na kampuni ya Kamal ya Jijini Dar es Salaam.

Wajasiriamali hao sasa watapitia katika programu maalumu itakayoendeshwa na Kamal kabla ya kukabidhiwa viwanda vyao vidogo vidogo vya kubangua korosho vitakavyojengwa katika eneo la viwanda la kampuni hiyo linalopatikana Zinga, Bagamoyo.

“Kilichotuleta hapa leo ni mwendelezo wa mradi huu uliozinduliwa mwezi Januari mwaka huu. Tunafurahi kutangaza rasmi kuwa tumefanikiwa kuwapata wajasiriamali zaidi ya 100. Bado tunaendelea kuwakaribisha wengine wenye nia ya kumiliki viwanda vya kubangua korosho,” alisema Mwenyekiti wa Kampuni ya Kamal, Bw. Gagan Santosh Gupta alipokutana na wajarisiamali hao Jijini Dar es Salaam jana.

Kampuni ya Kamal inalenga kutengeneza maelfu ya wajasiriamali wenye viwanda vidogo vidogo vya kubangua korosho ili Tanzania iweze kukuza uwezo wake wa kubangua zao hilo kama ilivyo kwa nchi ya India.

Takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya asilimia 90 ya korosho za Tanzania huuzwa nje ya nchi bila kubanguliwa, jambo ambalo hupoteza ajira na pesa za kigeni ambazo zingepatikana kutokana na mauzo nje ya nchi ya bidhaa ziliyoongezewa thamani.

Akizungumza katika hafla ya mazungumzo kati ya uongozi wa Kampuni ya Kamal na wajasiriamali hao, mjumbe wa bodi ya wakurugenzi wa Taasisi ya Sekta Binafsi (Tanzania Private Sector Foundation - TPSF), Bw. Silvestry Koka alisema mpango huo wa Kamal utasaidia kuongeza idadi ya wajumbe wa sekta ya biashara.

“Hii itasaidia kuweka ukuaji wa pamoja miongoni mwa wafanyabiashara,” alisema.

Bw. Koka, amabaye pia ni Mbunge wa Kibaha Mjini (CCM) na mwenyekiti wa kongani (cluster) ya makapuni (corporate) wa TPSF alisema wafanyabiashara wasisubiri hadi serikali iwaonyeshe chakufanya na badala yake waonyeshe njia ya kile wanachokifanya.

“Rais wetu, Samia Suluhu Hassan, amesema mara kadhaa kwamba anataka kufungua biashara kwa hiyo ni wajibu wetu kuonyesha utayari na mradi huu ni miongoni mwa nyanja muhimu za kuongeza idadi ya Watanzania wanaofanya biashara,” alisema.

Mradi wa kuendeleza ujasiriamali wa kitaifa Tanzania katika sekta ya viwanda vya kubangua korosho umetengenezwa kwa namna ambayo Kampuni ya Kamal itawapatia wajasiriamali wapatao 100 kila kitu wanachokihitaji ili kuendesha viwanda vidogo vidogo zaidi ya 100 vya kuchakata korosho.

Mahitaji hayo ni pamoja na mashine za kuchakata korosho, mashine za kukaushia korosho, mashine za kumenyea, meza za kusagia, umeme, maji pamoja na gharama nyinginezo.

Mjasiriamali atahitaji kuwa na Shilingi milioni 16.92 ambazo zitakuwa sawa na asilimia 20 tu ya jumla ya kiasi cha Shilingi milioni 84.6 zinazohitajika kuendesha kiwanda cha kubangua korosho.

Kiasi kinachobakia cha Shilingi milioni 67.68 ambacho ni sawa na asimilia 80 ya mahitaji kitapatikana kwa kupitia mkopo kutoka benki itakayoshirikiana na Kamal katika kudhamini mradi.

“Kwa hesabu za haraka haraka, kila mjasiriamali ataweza kupata faida ya Shilingi milioni 37.8 kwa mwaka baada ya kutoa gharama zote za uzalishaji,” alisema Bw. Gupta.

Faida ya mjasiriamali itaongezeka na kufikia Shilingi milioni 60 kwa mwaka ifikapo mwaka wa tatu wa usindikaji baada ya kumaliza kulipa mkopo wa benki.

“Ni imani yangu kuwa ili kusaidia katika ujenzi wa uchumi, tunahitaji kuweka mazingira mazuri yatakayowavutia watu wengi kuwa wajasiriamali na hii italeta tija na kasi zaidi katika dhana ya ujenzi wa uchumi wa viwanda,” alisema Bw. Gupta.

Alisema kiwanda cha kwanza katika mradi huo kimeshaagizwa na kipo nchini na kwaba hivi karibuni kitajengwa kwa lengo la kuanza kubangua na kuwapatia wajasiriamali masomo ya vitendo ya jinsi itakavyofanya kazi.

Wajasiriamali watakaopenda kuwa sehemu ya mpango huu watatakiwa kujaza fomu itakayopatikana katika tovuti ya https://kamal-group.co.tz/ ambapo watapata maelezo zaidi kuhusu mradi au kupiga simu kwenda: 0742308439. 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad