HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 17, 2021

WAZIRI LUKUVI AAGIZA UPIMAJI ENEO LA MGOGORO NA KUTOA ONYO KWA WAVAMIZI WA ARDHI

 

Na Munir Shemweta, DODOMA

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ameagiza wananchi 1,672 waliovamia maeneo na kuyaendeleza katika mtaa wa Mbuyuni kata ya Kizota mkoani Dodoma kupimiwa na kumilikishwa kulingana na jinsi walivyoendeleza kuonya tabia ya baadhi ya wananchi wanaovamia maeneo.

Aidha, ameagiza vyombo vya ulinzi na usalama mkoani Dodoma kuwachukulia hatua za kisheria watu 51 waliobainika kuhusika katika uuzaji maeneo kwa wananchi huku wakijua hawana umiliki wala mamlaka ya kufanya hivyo kwa mujibu wa sheria.

Akizungumza na wananchi wa mtaa wa Mbuyuni leo tarehe 16 Agosti 2021 Lukuvi alisema, uamuzi huo wa kuwabakisha wananchi waliovamia unafuatia ripoti aliyopewa na timu aliyoiunda kuchunguza mgogoro huo uliodumu kwa takriban miaka minne.

"Ninaagiza wananchi 1,672 waliovamia na kufanya maendelezo wapimiwe na kumilikishwa kulingana na ukubwa wa eneo la kila mmoja na yale maeneo ya wazi yaliyopimwa basi wapewe viwanja wananchi wengine 671’’ alisema Lukuvi.

‘’Maeneo mengi yanamilikiwa kwa hati na mtu anayejenga eneo la mtu ni mvamizi na wengi hapa mtaa wa Mbuyuni mna sifa ya uvamizi na hata kama mtu hajaendeleza muda mrefu siyo sifa ya uvamizi’’ alisema Waziri wa Ardhi.

Timu iliyoundwa kuchunguza mgogoro huo ilipewa maelekezo ya kupokea na kusikiliza changamoto zote katika mtaa wa Mbuyuni, kubainisha aina ya vyanzo vya migogoro pamoja na kutambua uhalali wa nyaraka za umiliki.

Pia Tume hiyo ilikuwa na kazi ya kuhakiki hali ya maenedelezo yaliyofanyika, kubainisha majina na jinai iliyofanyika na mwisho kutoa mapendekezo kwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Kwa mujibu wa Lukuvi, wananchi wote watakaomilikishwa maeneo waliyoyaendeleza watatakiwa kulipa gharama za urasimishaji na wengine kulipa gharama kidogo za kufidia maeneo waliyovamia kwa lengo la kufidia waliochukuliwa maeneo yao kupata maeneo mengine.

Kuhusu maeneo ya viwanda, Waziri Lukuvi alitaka maeneo hayo kubaki kama yalivyopangwa na kuagiza wamiliki wake kuomba ujenzi wa viwanda kwenye ofisi ya Mkurugenzi wa jiji la Dodoma ndani ya siku tisini na wasipofanya hivyo watanyang’anywa maeneo hayo kwa mujibu wa sheria.

Aidha, Waziri Lukuvi aliwaaasa wananchi wa Dodoma kuhakikisha hawafanyi ujenzi wowote bila kupata kibali sambamba na kununua maeneo bila kuuliza mamlaka husika kwa kuwa kutofanya hivyo kunaweza kusababisha kuuziwa maeneo yaliyopangwa kwa matumizi ya huduma za jamii.

"Msijenge wala kunumua eneo bila kuulizia mamlaka husika na ujenzi lazima uwe na kibali maana mamlaka ya upangaji ni ya jiji la Dodoma" alisema Lukuvi.

Mkuu wa mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka alimuahidi Waziri Lukuvi kusimamia utekelezaji wa maagizo yote yaliyopendekezwa kwenye ripoti na kumtaka mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri kuhakikisha anasimamia na kutatua changamoto zote za ardhi badala ya kuacha changamoto kupelekwa ofisi ya Mkuu wa mkoa.

Mmoja wa wananchi wa mtaa Mbuyuni katika kata ya Kizota aliyejitambulisha kwa jina la Mtumishi Yohana ameunga mkono uamuzi wa Waziri Lukuvi kwa kueleza kuwa ana imani sasa haki itatendeka katika eneo hilo.

Naye Bi. Zainabu Almasi mbali na kushukuru uamuzi wa Waziri Lukuvi alisema, bado kuna kero nyingine haijaenda sawa kutokana na kudai kuwa na eneo lilichukuliwa bila kulipwa fidia.

"Ninashukuru kwa uamuzi huu wa Waziri Lukuvi lakini kuna kero nyingine haijenda sawa, nimeporwa eneo langu na kujengwa na tajiri usiku na mchana nimenyanyasika" alisema Bi. Zainabu.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi akimpa maelekezo Mkuu wa mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka alipokwenda kuatatua mgogoro katika Mtaa wa Mbuyuni kata ya Kizota mkoani Dodoma jana Agosti 16, 2021. Kulia ni Mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad