HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 6, 2021

Teknolojia Kuboresha Maombi ya Leseni Huduma za Mawasiliano

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dk.Faustine Ndugulile pamoja na Waziri wa Habari, Utamduni,Sanaa na Michezo Innocent Bashungwa wakiwa katika uzinduzi wa Mfumo wa Uombaji leseni kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) uliofanyika jijini Dar es Salaam.Waziri wa Habari, Utamduni,Sanaa na Michezo Innocent Bashungwa akizungumza kuhusiana na mapinduzi ya Sekta ya Utangazaji pamoja na Mfumo wa Uombaji leseni kwa njia ya Mtandao utapolea mapinduzi makubwa nchini.


Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dk.Faustine Ndugulile akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mfumo wa utoaji wa leseni kwa njia ya Mtandao wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imeanza kutumia Mfumo mwingine wa Maombi ya leseni kwa kundi la leseni kubwa; mfumo huo unamuwezesha muombaji wa leseni kuwasilisha maombi yake ya leseni kwa Mamlaka hiyo bila kulazimika kufika ofisini na kukutana ana kwa ana na maafisa wa leseni.

Mfumo huo laini wa maombi ya leseni (License Management System) unatarajiwa kuzinduliwa siku ya Jumamosi Tarehe 31 Julai mwaka huu na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile (Mb) akiwa sambamba na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Innocent Bashungwa Mawaziri ambao kwa pamoja wizara zao zinasimamia sekta za Mawasiliano na Utangazaji kupitia Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA).

Mfumo huo mpya wa maombi ya leseni kupitia tovuti ya TCRA ambayo ni www.tcra.go.tz utasaidia kuongeza ufanisi wa upatikanaji leseni kwa wateja wanaonuia kutoa huduma za Mawasiliano na utangazaji, kurahisisha mchakato wa mteja kupata huduma za leseni, utaokoa muda wa muombaji leseni, utaokoa gharama za ufuatiliaji kwa mwombaji mpya wa leseni au anaetaka kuhuisha leseni yake, utaongeza ufanisi kwa pande zote mbili yaani Mamlaka inayotoa leseni na mwombaji, utaongeza uwazi kwa kuwa utamwezesha mwombaji wa leseni kupata mrejesho moja kwa moja kwenye simu yake ya kiganjani au kupitia barua pepe juu ya hatua zote na maendeleo ya uchakataji wa leseni aliyoomba na kumwezesha Mwananchi kuendelea na shughuli za maendeleo badala ya kufuatilia leseni.

Makundi ya leseni yanayopatikana kwenye mfumo huu ambao mwombaji ataweza kuwasilisha maombi yake bila kulazimika kufika katika ofisi za TCRA ni pamoja na Leseni za pamoja ikihusisha leseni za Huduma ya Maudhui (Content Services), Huduma ya Mtandao (Network Services), Huduma ya Mifumo Tumizi (Application Services) na Miundombinu ya Mtandao (Network Facilities).

Leseni nyingine ni Leseni ya Huduma za Vifurushi na Vipeto, Leseni ya Mtumiaji wa Masafa, Leseni ya Matengenezo na Usimikaji, Leseni ya Uagizaji Nje na Usambazaji, Rasilimali za Utoaji Namba, Leseni ya Huduma za Posta kwa Umma na Leseni ya Vifaa Vilivyoidhinishwa.

Hatua ambazo mwombaji wa leseni husika atapaswa kufuata ni pamoja na kutembelea tovuti ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ambayo ni www.tcra.go.tz kisha kugonga kiunga cha Utoaji Leseni na kisha kubofya kiunga cha Mfumo wa Kuomba leseni ambacho kitampeleka moja kwa moja kwenye ukurasa wenye fomu za kujaza ili aweze kupatiwa leseni anayohitaji kwa ajili ya kutoa huduma za Mawasiliano.

Hatua za maombi ya leseni za Mawasiliano kwa kundi la leseni kubwa (Individual License) zitasalia kama ilivyokuwa awali ambapo baada ya mwombaji kuwasilisha maombi yake kupitia Mfumo wa Maombi ya Leseni, itafuata hatua ya kutoa tangazo kwa umma kualika maoni ya wananchi juu ya mwombaji leseni, kisha tathmini kufanyika juu ya ombi lililowasilishwa, mwombaji kualikwa kutoa wasilisho la huduma ya Mawasiliano anayotarajia kuitoa na kisha hatua ya uidhinishaji leseni na hatimae mteja kupatiwa leseni.

Hatua hii inakuja ikiwa ni mkakati wa serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kurahisisha utaratibu wa upatikanaji huduma za leseni na kuweka mazingira rafiki zaidi kwa wawekezaji katika sekta ya Mawasiliano, sekta ambayo inatoa mchango chanya katika ukuaji wa maendeleo ya taifa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad