HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, March 12, 2021

Serikali kwa kushirikiana na wadau washauriwa kutoa elimu kuhusu afya ya sikio

 

Jane Edward, Michuzi TV, Arusha.

Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali  wameshauriwa kutoa elimu ya kutosha juu  ya afya ya sikio  ili kuondoa kuwepo kwa changamoto ya usikivu  ambayo imekuwa ni changamoto kubwa hasa kwa watoto.

Hayo yalisemwa Jana na  Mhadhiri mwandamizi chuo kikuu huria Cha Tanzania ,ambaye pia ni Mkuu wa kitengo kinachosimamia huduma kwa watu wenye ulemavu ,Dokta Cosmas Mnyanyi wakati akizungumza katika siku ya afya ya sikio duniani iliyofanyika katika chuo Cha ualimu Patandi.

Alisema kuwa, Kuna haja kubwa Sana ya wadau mbalimbali wakiwemo  wataalamu na watafiti waliobobea katika maswala ya usikivu kuhakikisha kwa pamoja wanatoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa afya ya sikio kwani bado ni changamoto na kupelekea watu kuendelea kuathirika.

Dkt  Mnyanyi alisema kuwa, tatizo la kutokusikia bado ni changamoto kubwa kwa mkoa wa Arusha ambapo walioathirika zaidi ni watoto kutokana na kutokuwepo kwa umakini kwa wazazi wao ,hivyo aliwataka wazazi kupeleka watoto way kupima afya ya sikio ili waweze kupata tiba mapema kabla tatizo halijawa kubwa zaidi.

Naye Daktari bingwa wa maswala ya  masikio,pua,na koo kutoka hospitali ya KCMC ,Dokta Kenneth Mlay alisema kuwa, baada ya kufanya upimaji kwa watoto na watu wazima wamegundua kuwepo kwa tatizo kubwa la usikivu hasa kwa watoto ambapo wengi wao hawajijui kuwa na tatizo hilo.

Alisema kuwa,wamegundua watoto wengi wana matatizo ya kupasuka kwa ngoma ya sikio ,hivyo waliwaomba wazazi pindi watoto wanapozaliwa  kuwapeleka mara kwa mara kupima masikio  ili  waweze kupata tiba mapema kabla tatizo  halijawa kubwa.

Naye Mratibu wa mradi wa ushirikiano Kati ya chuo Cha  ualimu Patandi na shirika la Sintef la Norway ,Isaack Myovela alisema kuwa, mradi huo umejikita katika kusaidia watoto wenye changamoto ya usikivu Tanzania ili waweze kushiriki vyema katika tendo la ujifundishaji na ufundishaji.

Myovela alisema kuwa,wameweza kutembelea shule za msingi 9 kwa mkoa wa Arusha na 4 Kilimanjaro ambapo wameweza kufanya utafiti na kugundua tatizo la  usikivu kwa watoto bado ni kubwa Sana ,hivyo kwa pamoja wanatakiwa kushirikiana kati yao na wazazi kujua umuhimu wa kutunza masikio ili kuondokana na changamoto za usikivu inayowakumba watoto wengi.


 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad