HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, February 22, 2021

CRDB kuwapa wateja wake mkono wa pole hadi Sh milioni 15

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

 

Benki ya CRDB imeendelea kutoa mafao ya gharama za mazishi na mkono wa pole kwa wateja wake wa ndani na nje ya nchi kati ya Sh milioni 2 hadi 15 kwa matatizo ya misiba au ajali.

 

Mafao hayo yanatolewa kupitia huduma ya bima ambatanishi ya maisha iliyozinduliwa na benki hiyo mwishoni mwa mwaka jana ijulikanayo kama 'KAVA Assurance'.

 

Akizungumza leo Februari 21, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni Tanzu ya Bima ya CRDB, Wilson Mzava, amesema waliangalia soko na kubaini kuna uhitaji ndipo walipoamua kutengeneza huduma hiyo ya KAVA Assurance.

 

"Tuliona wateja wetu walikuwa wanahitaji kitu cha ziada zaidi, tuliona pia wateja wetu wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) walikuwa na changamoto nyingi hasa pale mwenzao mmoja anapokuwa amefariki. Pia tukaangalia mtu akifungua akaunti katika Benki ya CRDB tunampa nini cha tofauti ili kumtofautisha na benki nyingine.

 

"Timu ya kitengo cha bima katika Benki ya CRDB ilikaa chini na kuamua kutengeneza bidhaa ambayo tutaiongezea thamani katika akaunti ya mteja wetu," amesema Mzava.

 

Akifafanua amesema mteja mwenye akaunti katika benki hiyo ikitokea akafariki benki itatoa mkono wa pole wa Sh milioni 2 na kwa wateja maalumu (Premier) benki itatoa Sh milioni 5 wakati wale wenye akaunti ya Tanzanite wanaoishi nje ya nchi watapewa Sh milioni 5.

 

Aidha amesema kama mteja mwenye akaunti ya Tanzanite akifia nje benki itagharamia kusafirisha mwili kutoka kwenye nchi aliyofia kuja Tanzania kwa gharama isiyozidi Sh milioni 15.

 

"Ni rahisi sana kuwa na KAVA Assurance kinachotakiwa ni kufungua akaunti ya CRDB kisha utaanza kufurahia haya mafao. Wale wanaopata Sh milioni 2 pia kama amepata ajali na kupata ulemavu wa kudumu tunatoa mkono wa pole wa Sh milioni 2.

 

"Kuna ambao tayari wana familia ameoa au ameolewa, ile milioni 2 inakuwa 'extended' kwa mke au mume, wale wenye Premier Account tuna extend tena milioni 5 kwa mke wa mume," amesema.

 

Amesema ili kupata mafao hayo kinachotakiwa ni kwenda katika tawi lililo karibu akiwa na kibali cha mazishi na vitambulisho ambapo atajaza fomu na kuambatanisha uthibitisho kisha atalipwa mafao yake ndani ya saa 72.

 

"Huna haja ya kufunga safari kuja makao makuu au kwenda nje ya mkoa mwingine, nenda kwenye tawi lililo karibu. Kutoa taarifa tangu janga lilipotokea isizidi miezi sita na kuleta viambatanisho vyote isizidi miezi tisa.

 

"Kitu ambacho tunakiangalia ni kuwa na mteja wakati wa nyakati ngumu kwahiyo hii 'product' inakuja kumfariji mteja na tunataka ifike mahali wananchi wajue kabisa kwamba CRDB ipo na itasaidia kutoa rambirambi," amesema Mzava.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad