HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, January 26, 2021

TAKUKURU MANYARA YAANDAA MPANGO KAZI WA MIEZI MITATU

 

 



Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Manyara, Holle Joseph Makungu akizungumza na waandishi wa habari.
………………………………………………………………….
Na Mwandishi wetu, Babati
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Mkoani Manyara, imeandaa mpango kazi wake utakaotekelezwa kwa muda wa miezi mitatu ya kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu.
Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Manyara, Holle Joseph Makungu ameyasema hayo mjini Babati wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Makungu amesema miongoni mwa mpango kazi wao ni kujikita zaidi kwenye kudhibiti miradi ya maendeleo, udhibiti wa madini ya Tanzanite kuhakikisha kanuni za usafirishaji wa madini za mwaka 2019 zinafuatwa.
Amesema pia watafuatilia ukopeshaji wa matrekta yaliyotolewa na shirika la maendeleo la Taifa (NDC) ilikuhakikisha fedha zinarejeshwa na wakulima zaidi wanakopeshwa kupitia fedha hizo.
Amesema watafuatilia pia mikopo ya matrekta toka TIB DEVELOPMENT LIMITED wanawataka waliokopa wafike TAKUKURU baada ya taarifa kutolewa ili wapewe utaratibu wa namna ya kurudisha mikopo hiyo kwa mujibu wa mikataba yao.
“Kwa watakaokaidi watalazimishwa ili mikopo hiyo iwezwe kuwanufaisha pia wakulima wa nchi hii hatimaye tuweze kuondokana na jembe la mkono ambalo tija yake ni kidogo kwa maana ya kilimo tulichokusudia kifanywe na wananchi wetu,” amesema Makungu.
Amesema pia kwenye kipindi hicho watafuatilia hujuma zinazofanywa kwa wakala wa ufundi wa umeme TEMESA kwa maofisa maduhuli kukataa kulipa madeni ya fedha za matengenezo hivyo TEMESA kushindwa kufanya kazi zake ipasavyo na kushindwa kununua vipuri hivyo hupeleka magari kwenye karakana binafsi.
“Mfano ofisi fulani jina linahifadhiwa ambayo kwa mujibu wa kumbukumbu za TEMESA inadaiwa shilingi 89, 591, 175, 39 hayo ni matumizi mabaya ya madaraka, tunatoa hadi Februari 28 mwaka huu wadaiwa wote wa TEMESA Manyara wawe wamelipa na tutaanza uchunguzi kwa maofisa hao wasiolipa tutawachukulia hatua na majina yao tutaweka hadharani,” amesema Makungu.
“Jambo la mwisho ninalotaka wananchi wa mkoa wa Manyara kufahamu ni kuwa tumeanzisha ofisi ya TAKUKURU inayotembea kwa kutenga siku moja kila mwezi na kuwatembelea kwa kuwafuata wananchi mahali walipo na kusikiliza kero zao na kuzitatua,” amesema Makungu.
Amesema kwa kuanzia Januari 18 mwaka huu waliotembelea eneo la kijiji cha Naisinyai Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro na kusikiliza kero mbalimbali za wananchi na kuzitatua.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad