HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 6, 2021

KIBAMBA BADO INA CHANGAMOTO YA MAJI, DAWASA LIMALIZENI

 Na Zainab Nyamka, Michuzi Tv

Mbunge wa Jimbo la Kibamba Issa Mtemvu amesema Kibamba bado kuna changamoto kubwa sana ya maji ya watu kukosa maji ingawa ni eneo lenye miradi mikubwa.

Amewataka wananchi wa Kibamba kuhakikisha wanalinda miundo mbinu ya maji pindi miradi inapopita kwenye maeneo yao kwani inatumia fedha nyingi sana za watanzania.

Ameyasema hayo leo wakati wa Ziara ya kutembelea Kata nne kati ya Sita zinazopatikana kwenye jimbo hilo zinazoongoza kwa changamoto ya maji akiwa ameongozana na madiwani.

Akizungumza baada ya kumaliza kukagua miradi ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (DAWASA)  Mtevu amewataka Dawasa kuhakikisha changamoto ya maji inamalizika ndani ya muda mfupi.

Amesema, tanki la maji linalohudumia Kisarawe na hata maeneo mengine ya Mbezi linapatikana Kibamba lakini wakazi wa eneo hilo wanakaa bila huduma ya maji, hilo haliwezekani lazima maji yafike Kibamba kote.

"Tumezunguka tumeona kuanzia kwenye chanzo cha Changanyikeni, changamoto iliyopo ya watu kukosa maji na ndio maana leo tumeamua kufanya ziara hii nikiambatana na Naibu Mstahiki Meya na madiwani wengine sambamba na mameneja wa Dawasa na wataalamu wake," amesema

"Hii ni ziara nzuri, ya kikazi na hii italeta chachu ukizingatia kuna miradi mikubwa ya maji inakuja ambayo itaondoa tatizo hili nadhani wenyewe mmeona wananchi wakipata shida ya maji na hata kufikia hatua ya kununua mabomba wenyewe na wataalamu wamefika hapo na kutoa elimu," 

Kwa upande wa Mstahiki Meya wa Ubungo, Hassan Mwasha amesema anaona Kata yake ya Msigani ina changamoto ya maji ila imani kubwa inaanza kuonekana baada ya Dawasa kufika katika eneo lao.

Amesema, serikali ya awamu ya tano inahakikisha kero ya maji inaondoka kwenye Jiji la Dar es Salaam na hilo linaenda kufikia ukingoni.

Meneja wa Dawasa Ubungo Gilbert Massawe amewataka wananchi kuendelea kuwa na imani na Mamlaka hiyo kwani wanafanya jitihada kubwa kuhakikisha changamoto ya maji inaisha ndani ya Kibamba na maeneo mengine yote.

Katika ziara hiyo, Mbunge aliweza kuipongeza Dawasa kwa kazi kubwa wanayoifanya na yenye kuonesha tija ya kutaka kuondoa kero ya maji kwa wananchi wake.

Ziara hiyo ilianzia Changanyikeni, na kupita katika kata ya Msigani, Kibamba, Mbezi na Goba.



Mbunge wa Kibamba Issa Mtemvu akiyaonja maji yanayotoka katika moja ya vizimba vinavyopatikana katika kata ya Kibamba yanayotumiwa na wananchi wakati wa ziara yake na madiwani wa Jimbo hilo katika miradi ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA)
Mbunge wa Kibamba Issa Mtemvu akieleza jambo kwa Mameneja wa Dawasa na wataalamh wa Mamlaka hiyo wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi inayopatikana ndani ya Jimbo hilo.
Mbunge wa Kibamba Issa Mtemvu akieleza jambo kwa Mameneja wa Dawasa na wataalamh wa Mamlaka hiyo wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi inayopatikana ndani ya Jimbo hilo.


Meneja wa Dawasa Ubungo Gilbert Massawe akitolea ufafanuzi kwa Mbunge wa Kibamba wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya maji inayopatikana ndani ya Jimbo hilo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad