HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, December 14, 2020

WAZIRI AWESO AWATUMBUA WATUMISHI WATATU WA WAKALA WA UCHIMBAJI VISIMA DDCA

 Na Zainab Nyamka, Michuzi Tv


Waziri wa Maji Jumaa Aweso amewasimamisha kazi watumishi watatu wa Wakala wa uchimbaji visima (DDCA) kutokana na  tuhuma za ubadhilifu.

Amesema kuwa, watumishi hao watapangiwa kazi zingine baada ya kushindwa kutekeleza maagizo ya serikali katika utendaji.

Aweso amesema, yapo maovu aliyoyabainisha katika Kitengo cha utafiti wa maji vijijini, Serikali imeweza kuwapatia mitambo minne kwa ajili  ya utafiti wa maji vijijini na zote zimeharibika lakini mkuu wa kitengo ana mitambo inafanya kazi.

Pia, Aweso amesema amewasimamisha kazi wakuu wa Kitengo cha mafundi na manunuzi wote wameondolewa ili DDCA ipate  watu watakaofanya kazi kwa uweledi.

Aidha, Aweso amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji Mhandisi Antony Sanga kufanya uchunguzi wa tuhuma za Chuo cha Maji kuhusu uuzwaji wa nyumba za  chuo kinyume na utaratibu.

Amesema Watumishi hawana nyumba za kukaa, lakini wao kiholela wamejimilikisha, na hili kama Waziri nitasimamia suala hilo ili watumishi wapate nyumba za kukaa.

Amesema, Lengo la serikali kuanzisha kwa Chuo cha maji ni kuzalisha wataalamu watakaosaidia sekta ya maji, kufanya tafiti katika changamoto za maji na miradi mingi vijijini imekuwa ikichezewa katika usanifu na hivyo inakosa kuhimili kwa muda mrefu.

"Mradi umejengwa lakini uendelevu wake umekuwa ni changamoto, ndio maana serikali ilianzisha chuo cha maji ili wataalamu wazalishwe na kusaidia kwenye sekta ya maji," 

"Nawaagiza watu wa Wakala wa maji na usafi wa mazingira Vijijini RUWASA kukaa chini na Chuo cha maji ili kuweza kuwapata wataalamu hao kusaidia sekta ya maji," 

Aweso amesisitiza kuwa serikali inataka wananchi wote wapate huduma ya maji safi na salama ili kutimiza azma ya Rais Dkt John Pombe Magufuli ya kumtua mama ndoo kichwani.
Waziri wa Maji Jumaa Aweso akitembelea ujenzi wa Kituo cha Kusukumia maji (Booster Pump) katika mradi wa maji wa Mkuranga, Mkoani Pwani unaotarajiwa kukamilika Februari 20

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad