Mratibu
wa Kitaifa wa Zao la Korosho kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo TARI
Naliendele, Dkt.Geradina Mzena, akitoa mada kwenye mafunzo ya kilimo
bora cha korosho yaliyotolewa jana kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Mji
Mdogo wa Gairo kwa Maafisa Ugani na Wakulima kutoka Halmashauri 7 za
Mkoa wa Morogoro.
Mtafiti
Mwandamizi na Mdhibiti wa visumbufu vya wadudu na magonjwa kwenye zao
la korosho, kutoka Tari- Naliendele Dkt.Wilson Nene, akitoa mada kwenye
mafunzo hayo.
Mtafiti kutoka Tari- Naliendele Programu ya Zao la Korosho, Kasiga Ngiha, akitoa mada kuhusu Agronomia ya korosho.
Washiriki wakiwa katika mafunzo hayo.
Mkuu wa Kituo cha Morogoro kutoka Bodi ya Korosho, Luseshelo Silomba akizungumza kwenye mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea.
Afisa Kilimo wa Wilaya ya Gairo, Eunice Kyungai akizungumza kwenye mafunzo hayo.
Washiriki wakiwa katika mafunzo hayo.
Afisa Kilimo na Mratibu wa Zao la Korosho Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro,Isabella Chilumba akizungumza.
Mafunzo yakiendelea.
Mjadala ukiendelea.
Washiriki wakiwa kwenye mafunzo hayo.
Mkulima Elizabeth Senyagwa kutoka Gairo, akishiriki moja ya mjadala kwenye mafunzo hayo kwenye mafunzo hayo.
Afisa Kilimo Abilah Samli kutoka Kilosa akizungumza kwenye mafunzo hayo.
Mkulima kutoka Dumila, Samwel Dede akishiriki moja ya mjadala kwenye mafunzo hayo.
Godwin Myovela na Dotto Mwaibale.
TAASISI
ya Utafiti wa Kilimo Nchini (TARI) kupitia Kituo chake cha Naliendele
kimewataka wakulima wote wa zao la korosho kubadilika na kuanza kulima
kilimo cha biashara kwa kuzingatia 'agronomia' stahiki ili kuongeza tija
na ubora wa zao hilo.
Sambamba
na hilo kituo hicho kimetoa angalizo kwa wakulima na wadau wa korosho
kuhakikisha wanaepuka udanganyifu wowote wanapohitaji huduma ya mbegu
bora ya zao hilo, badala yake wawasiliane na Maafisa Kilimo wa eneo
husika ili kupata maelezo ya namna ya upatikanaji wake .
Mratibu
wa zao hilo kitaifa kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo Tari Naliendele
Dkt.Geradina Mzena aliyasema hayo kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Mji
Mdogo wa Gairo jana wakati akifungua mafunzo ya kilimo bora cha zao la
korosho kwa maafisa ugani na wakulima kutoka Halmashauri 7 za Mkoa wa
Morogoro.
"Tari
Naliendele hatuuzi mbegu kwa fedha taslimu, lazima uwe na namba ya
malipo 'control number' na endapo ukiuziwa mbegu na mtu yeyote kwa fedha
taslimu ujue umeibiwa. Korosho ni zao la kudumu, lina mfumo wake na
kamwe usijaribu kupanda mbegu usiyoijua." alisema Mzena.
Alisema
mbegu bora ya zao hilo na aina zake huzalishwa na Kituo cha Utafiti wa
Kilimo cha Tari Naliendele pekee na sio kwingineko, hivyo wakulima
wanapaswa kuwa makini ili kwa pamoja kuweza kuinua ubora wa zao hilo na
kujihakikishia uwepo wa soko lake kitaifa na kimataifa.
Aidha
Mtafiti huyo na Mgunduzi wa zao hilo Dkt.Mzena alisema ili kubaini kama
mbegu ya korosho husika ina ubora ni sharti idadi ya punje za korosho
ziwe chini ya 200 kwa kilo moja na sio zaidi ya hapo.
Mratibu
huyo kitaifa alifafanua kwamba kilo moja ya zao hilo inaposheheni punje
zaidi ya 200 hudhihirisha wazi kuwa ubora wa mbegu hiyo una mashaka na
mkulima husika anapaswa kufika Tari Naliendele ili kupatiwa mbegu
mbadala zenye ubora.
Hata
hivyo akizungumza mbele ya wakulima na maafisa ugani, Mzena ambaye pia
ni Mratibu wa Utafiti na Ubunifu kutoka Kituo cha Tari Naliendele
alibainisha kuwa pamoja na mambo mengine korosho ambayo hulimwa na
takribani watanzania laki 283 nchini ina faida kubwa katika kuongeza
kipato cha kaya na kuondoa umasikini.
Alisema
Mtanzania yeyote atakayelima korosho ndani ya mikoa rafiki takribani 17
inayostawisha zao hilo ni dhahiri atajipatia pesa za kutosha kutokana
na ukweli kwamba zao hilo lina nguvu na utajiri mkubwa, tofauti na mazao
mengine. Kikubwa ni kuzingatia kanuni bora za kilimo.
"Korosho
haijawahi kukosa soko la uhakika, na zaidi inamfumo wa soko
linaloeleweka unaoitwa stakabadhi ghalani na kukuwezesha kukopesheka
kupitia taasisi za fedha." alisema.
Mzena
alisisitiza kwa wale walio mbali na vituo vya Tari wakihitaji huduma ya
mbegu bora wamuone Afisa ugani wa eneo lake ili hatimaye awasiliane na
Tari Naliendele ili kuepuka hasara ya mkulima kuuziwa mbegu na
viuatilifu feki.
"Mbegu
za zao hili la kimkakati na aina zake zinazozalishwa na kituo chetu
zinavumilia ukame, magonjwa, visumbufu vya wadudu na zinatoa mazao
mengi." alisema Mzena.
Kwa
upande wake Mtafiti mwingine wa zao hilo wa kituo hicho Kasiga Ngiha
alisema kwa sasa wataalamu wa kituo hicho wanapita maeneo mbalimbali
nchini kutoa elimu ya kuongeza ubora na uzalishaji wa zao la korosho kwa
tija na ustawi.
Mtafiti
Mwandamizi na Mdhibiti wa visumbufu vya wadudu na magonjwa kwenye zao
hilo, Dkt.Wilson Nene alisema kituo hicho kinatoa mafunzo hayo lengo ni
kuwawezesha wakulima na maafisa ugani kuwatambua wadudu waharibifu,
magonjwa na namna ya kukabiliana nayo ili kufikia shabaha tarajiwa
kutoka tani laki tatu zinazozalishwa kwa sasa kufikia tani milioni 1
ifikapo 2023.
"
Korosho inafaida nyingi ikiwemo baada ya kusindika tunazalisha bidhaa
kama korosho karanga, na bibo lake hutumika kutengeneza bidhaa ya juisi,
mvinyo, ethanol na malisho ya mifugo." alisema Nene.
Alisisitiza
kimsingi mafunzo hayo yanalenga kutoa teknolojia ya mbinu bora na za
kisasa za uzalishaji wa zao la korosho kwa kuzingatia wapi mkulima
atapata mbegu bora, namna ya kuandaa shamba, kuchimba mashimo, kupanda
na kupalilia hatimaye mavuno yake.
Kituo
cha Tari Naliendele pamoja na mambo mengine kimepewa majukumu ya
kitaifa ya kutafiti, kustawisha na kuongeza tija na thamani kwenye mazao
ya korosho na mbegu jamii ya mafuta-ikiwemo ufuta, karanga na alizeti.
No comments:
Post a Comment