HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, September 29, 2020

JAJI MMILLA ATAKUMBUKWA KWA KUJITOA KWAKE , MWILI WAKE WAZIKWA GOBA JIJINI DAR

  

Na Mary Gwera na Lydia Churi-Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amemuelezea Marehemu Jaji Bethuel Mmilla kuwa alikuwa ni mchapakazi na atakumbukwa kwa utendaji kazi wake wa kujitoa na ushirikiano.

Mwili wa aliyekuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Bethuel Mpakani Kasefu Mmilla umezikwa jana nyumbani kwake Goba Michungwani jijini Dar es salaam baada ya kuagwa katika viwanja vya Karimjee na baadaye kufanyiwa Ibada katika kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (K.K.K.T) Usharika wa Mwenge jijini Dar es salaam.

Akizungumza katika hafla ya kuuaga mwili wa marehemu Jaji Mmilla aliyefariki usiku wa Septemba 24, Jaji Mkuu alisema wasifu wa marehemu Jaji Mmilla ni mfano mzuri wa namna alivyowatumikia zaidi walio wengi kuliko alivyojitumikia kwa maslahi yake binafsi au maslahi ya familia yake.

“Wasifu wake unaonyesha kuwa kila kituo katika utumishi wake wa Mahakama, amekuwa ni wa kutumikia, anayetoa, na asiye wa kutumikiwa,” alisema Mhe. Jaji Mkuu.

 
Aliongeza kuwa Maamuzi yaliyotolewa na marehemu Jaji Mmilla yatabaki kuwa mifano hai ya mambo yote aliyoyaamini na kuyatekeleza kwa vitendo. Alisema marehemu atakumbukwa pia kwa ucheshi na utani wake wa mara kwa mara ambao uliwasaidia waheshimiwa Majaji wa Rufaa kusahau angalau kidogo, maswala magumu ya kisheria na kimaamuzi.

Kwa upande mwingine, Mhe. Jaji Mkuu amewashukuru madaktari, wahudumu wote wa Hospitali ya Jeshi Lugalo, Hospitali ya Taifa Muhimbili na wale wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiongozwa na Prof. Mohamed Janabi kwa kuwa karibu na marehemu.

Akitoa salaam kwa niaba ya Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija alimuelezea Marehemu Jaji Mmilla kuwa alikuwa ni kiongozi mwenye ushirikiano mkubwa na wenzake na aliyekuwa akiwatia moyo katika kazi mbalimbali za utoaji haki.

Naye Mwenyekiti wa chama cha wanasheria Tanzania (Tanganyika Law Society) Mhe. Dkt. Rugemeleza Nshalla amewashauri Majaji na Mahakimu kuandika hukumu zenye mguso chanya katika maisha ya watu na utawala wa sheria.

“Marehemu Jaji Mmilla aliandika hukumu nyingi ambazo zitatumika kama rejea kwa wanafunzi wanaosoma sheria nchini, Mahakimu pamoja na Majaji” alisema Dkt. Nshalla.

 
Dkt. Nshalla pia aliwaasa familia ya marehemu kwa kuwasahuri kuishi kwa kupendana na kushirikiana ili kuyaenzi mazuri aliyoyafanya marehemu Jaji Mmilla.

Mazishi ya Marehemu Jaji Mmilla yalihudhuriwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Majaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi, Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, wadau mbalimbali pamoja na watumishi wa Mahakama.

Jaji Mmilla alifariki dunia usiku wa Septemba 25, 2020 katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Awali marehemu alilazwa katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo jijini Dar es salaam Septemba 23, 2020 alipokuwa akipatiwa matibabu na baadaye kuhamishiwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) alipofariki dunia.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad