HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, September 11, 2020

Benki ya NMB yadhamini CDF Trophy Cup 2020 kwa Sh. Mil. 40

Benki ya NMB imetangaza kudhamini Michuano ya Gofu - Kombe la Mkuu wa Majeshi ‘CDF Trophy Cup 2020’, inayotarajia kufanyika siku ya Septemba 19 na 20 mwaka huu, kwenye Viwanja vya Gofu Lugalo jijini Dar es Salaam.

Akitangaza udhamini huo wenye thamani ya Shilingi Milioni 40, katika hafla iliyofanyika Makao Makuu ya Klabu ya Gofu Lugalo, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa NMB, Omary Mtiga alisema udhamini wao unatokana na kutambua thamani ya michezo ikiwemo gofu.
Mwenyekiti wa Klabu ya Lugalo Brigedia Mstaafu Michael Luwongo (wa pili kutoka kulia ) akipokea mfano wa hundi ya shilingi Milioni 40/- kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Omari Mtiga, iliyotolewa na Benki hiyo kwa ajlli ya udhamini wa michuano ya Gofu  ya Mkuu wa Majeshi. Kushoto ni Nahodha wa timu ya Gofu ya NMB, Michael Misabo na kulia ni nahodha wa timu ya Gofu Lugalo, Captain Japhet Massawe.


Alisema ya kuwa, NMB kama taasisi kinara ya kifedha nchini, inafurahishwa na aina ya ushirikiano uliopo kati yao na Klabu ya Gofu Lugalo inayoandaa michuano hiyo na kwamba udhamini wao huo ni wa sita mfululizo tangia mwaka 2014 na unaakisi nafasi ya Benki hiyo katika maendeleo ya michezo Tanzania.

Tunafurahishwa na aina hii ya ushirikiano baina yetu na waandaaji, ambao hauishii tu katika kudhamini CDF Cup, bali pia unaoifanya NMB kuwa na nyota wengi wa gofu wanaounda timu yetu, ambayo nayo itashiriki michuano hiyo,” alisema Mtiga.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Klabu ya Gofu Lugalo, Brigedia Jenerali Mstaafu Michael Luwongo, aliishukuru NMB kwa namna inavyojitoa katika kusaidia ukuaji wa michezo nchini, hasa CDF Cup inayoratibiwa na kuendeshwa na klabu yake. Alisema wanatarajia kuwa na washiriki wengi mwaka huu, kutokana na mwitikio aliouona, kwani hadi wanakabidhiwa hundi ya udhamini na NMB, kuna jumla ya washiriki 110 waliojiandikisha, ikiwa imesalia wiki moja kabla ya kuanza kwa michuano hiyo.

“Tayari washiriki 110 wamejisajili hadi sasa kutoka klabu mbalimbali nchini, zikiwemo Lugalo, Dar Gymkhana, Arusha Gymkhana, Zanzibar Gymkhana, NMB na nyinginezo, na tunatoa wito washiriki wajitokeze zaidi na wazazi wawalete watoto wao kushiriki,” alisema Luwongo.

Naye nahodha wa Klabu ya Gofu ya NMB, Michael Misabo, alisema kuwa nyota wa timu yake wako tayari kushindania na hatimaye kutwaa ubingwa wa CDF Trophy, kwani wamejiandaa vya kutosha kuhakikisha wanafanya vyema katika kinyang’anyiro hicho.

“Katika CDF Cup 2020, NMB sio tu wadhamini wakuu wa mashindano, bali pia ni washiriki tuliojiandaa kuchuana na tunaingia tukiwa na uhakika wa kufanya makubwa na kutwaa ubingwa wa jumla,” alisema Misabo mbele ya wanahabari waliohudhuria hafla hiyo.

Kwa upande wake, nahodha wa Klabu ya Gofu Lugalo, Japhet Masai, alisema kama timu wamejiandaa vya kutosha na kwamba maandalizi ya jumla ya michuano yanaendelea vyema na kwamba Ijumaa Septemba 18 kutafanyika utangulizi kwa nyota wa kulipwa kuchuana.

“Nyota wa kulipwa watatangulia kuchuana Ijumaa ya Septemba 18, kisha ufunguzi rasmi Jumamosi na kuhitimisha michuano Jumapili kwa nyota wa ngazi mbalimbal kutoana jasho katika Divisheni za A, B na C kwa watoto, wanaume na wanawake, pamoja na nyota wa ridhaa,” alifafanua.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad