Veronica Simba – Dodoma
WAZIRI wa Nishati Dkt Medard Kalemani, ameagiza Mkandarasi
anayetekeleza Mradi wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa
Kwanza, mkoani Dodoma akatwe asilimia 10 ya malipo yake kutokana na
kuchelewa kukamilisha kazi hiyo.
Alitoa maagizo hayo, Agosti 12, 2020 baada ya kukagua maendeleo ya
utekelezaji wa Mradi huo katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Chemba.
Akiwa amefuatana na Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga, Waziri
Kalemani aliutaka Uongozi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kukata
kiasi hicho cha malipo ya Mkandarasi husika, ambaye ni Kampuni ya A2Z
Infra Engineering Limited, kuanzia Juni 30, 2020 muda ambao alipaswa
kukamilisha Mradi.
Sambamba na agizo hilo, Waziri pia alimtaka Mkandarasi huyo
kukamilisha kazi ya kuunganisha umeme katika vijiji vyote 66
vilivyobakia kabla ya Septemba 15 mwaka huu, huku akisisitiza kuwa,
hakutakuwa na nyongeza ya muda wala msamaha.
“Asipomaliza ndani ya wakati huo, mchukulieni hatua za kisheria na
kimkataba. Maeneo yatakayobaki, fanyeni ninyi TANESCO kwa pesa hiyo.”
Katika kuhakikisha kazi hiyo inatekelezwa, Waziri alimwelekeza Mkuu
wa Wilaya kushikilia hati za kusafiria za Wakandarasi husika na
kuhakikisha hawatoki nje ya Mkoa wa Dodoma, hadi watakapokamilisha kazi
hiyo.
Aidha, alimwagiza Mkandarasi huyo kuongeza vibarua na magenge, ili aweze kukamilisha kazi kwa wakati.
Vilevile, alimtaka kuondoa mara moja nguzo zote zilizorundikwa chini
na kuzisimika, kuvvuta nyaya na kuwaunganishia umeme wananchi.
“Kiu ya wananchi ni kuona umeme unawaka katika nyumba zao.
Hawependezewi kuona nguzo zikiwa zimerundikana chini, nanyi mkipitapita
pasipo kuwawashia umeme,” alisisitiza Waziri.
Dkt Kalemani alitoa wito kwa Wakandarasi wote nchini, wanaoendelea
kutekeleza Miradi ya REA III, kuhakikisha wanakamilisha ifikapo Septemba
15, 2020.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya alimshukuru Waziri kwa kufuatilia
utekelezaji wa Mradi husika huku akiweka wazi kuwa hana imani na
Mkandarasi huyo kutokana na kutotekeleza majukumu yake ipasavyo.
Aliahidi kufanyia kazi maelekezo yote ya Waziri katika kumsimamia
Mkandarasi ili kuhakikisha anakamilisha kazi hiyo na hivyo wananchi
wapate huduma ya umeme kama ilivyokusudiwa na Serikali.
Mkuu
wa Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma, Simon Odunga (wa pili-kushoto)
akizungumza jambo, wakati wa ziara ya Waziri wa Nishati Dkt Medard
Kalemani (wa pili-kulia) wilayani humo, kukagua utekelezaji wa miradi ya
umeme vijijini, Agosti 12, 2020.
Waziri
wa Nishati Dkt Medard Kalemani (kulia), akitoa maelekezo kwa
Wakandarasi wanaotekeleza Mradi wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu,
Mzunguko wa Kwanza, mkoani Dodoma, Kampuni ya A2Z Infra Engineering
Limited (kushoto) kuhakikisha wanakamilisha kazi hiyo kabla ya Septemba
15, mwaka huu, alipokuwa katika ziara ya kazi wilayani Chemba, Agosti
12, 2020. Kulia kwa Waziri ni Mkuu wa Wilaya hiyo, Simon Odunga.
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani na Ujumbe wake, wakiwa
katika ziara kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, wilayani
Chemba, Mkoa wa Dodoma, Agosti 12, 2020.
No comments:
Post a Comment