HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, July 10, 2020

SERIKALI YAAGIZA KUBORESHWA KWA VIWANGO.VYA HUDUMA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA DODOMA


Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ameuagiza Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kuboresha huduma za tiba kwa wananchi wanaofika kupata huduma za afya katika hospitali hiyo.

Prof. Makubi ametoa maagizo hayo kufuatia ziara ya kushtukiza aliyoifanya kwenye Hospitali hiyo na kushuhudia changamoto mbalimbali ikiwemo baadhi ya wagonjwa kuchelewa kupewa huduma, Madaktari bingwa kutowaona wagonjwa kwa wakati na huduma za vipimo kuchelewa.

“Yapo mazuri tumeona mnayofanya kwa wananchi na tunawapongeza, ila lazima kuangalia upande wa pili ambao wananchi wanayataka, kwa yale mapungufu tuliyoyaona tungependa kuona yanaboreshwa haraka ili hospitali hii iwe ya mfano kwa hospitali zote za rufaa za mikoa kwa kutoa huduma zilizo bora”.

Prof. Makubi amesema hospitali hiyo inatakiwa kuonesha mfano kuanzia utoaji wa huduma bora kwa mteja pamoja, kupunguza muda wa wagonjwa kusubiri huduma, upatikanaji wa wauguzi na mabingwa wanapohitajika na usafi wa wodi kwani ndiyo chachu ya wananchi wengi kufika hapo na kupata huduma kabla hawajapewa rufaa ya kwenda Hospitali kubwa kama Benjamin Mkapa.

Aidha, Mganga Mkuu huyo ameutaka uongozi na watumishi wa hospitali hiyo kutambua majukumu yao kwa kuonesha kuwajali wananchi wote na kuwataka kuweka utaratibu usio na usumbufu kwa wagonjwa na kupatiwa huduma kwa wakati.

Prof. Makubi alionyesha kusikitishwa alipokuta wodini baadhi ya wagonjwa wamelazwa na hawajaonwa na Mabingwa kwa zaidi ya siku tatu, wauguzi wakiwa hawajaambatana na madaktari katika kuzungukia wagonjwa huku madaktari wa vitendo (interns) wakifanya “procedures” peke yao bila uangalizi na baadhi ya wagonjwa wengine wakiwa wamelazwa chini wakati vitanda viko wazi pamoja na mazingira ya wodi hayakuwa ya kuridhisha na kukosekana kwa mpangilio wa vifaa (5S)

“Lazima watumishi mjitambue mko wapi kwani awamu hii ni ya kuwajali wanyonge na kufanya kazi kwa bidii ndio kanuni ya awamu hii hapa kazi tu”. Alisisitiza Prof. Makubi.

Prof. Makubi ameelekeza madaktari wa hospitali hiyo kufanya kazi kwa ushirikiano na wauguzi katika kuwahudumia wagonjwa katika wodi, kuleta mabadiliko kwa kutengeneza miongozo mbalimbali ya kusimamia huduma na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kila mwananchi anayefika hospitalini hapo ahudumiwe kwa wakati na huduma inayostahili.

Kwa upande mwingine Mganga Mkuu huyo wa Serikali ameitaka hospitali hiyo kuboresha idara ya huduma kwa wateja (Customer Care) kwani hakuna mgonjwa anayependa kuchelewa kupata huduma hivyo lazima kutoa huduma bora na zinazohitajika kwa wananchi wote.

Prof. Makubi ameelekeza Uongozi wa Hospitali kuhakikisha mashine za maabara ambazo zimeishiwa vitendanishi, zinaanza kufanya kazi haraka.

"Ni vizuri mkapunguza muda wa kusubiri majibu ya vipimo vya damu, X-ray, ultrasound, na Moyo na vipimo vingine".Alielekeza Prof. Abel Makubi.

Prof.Makubi aliagiza Hospitali zote nchini zifanyie kazi changamoto alizoziona hapo Dodoma, na akaagiza Idara ya ukaguzi wa huduma bora kutoka wizarani wafanye ufuatiliaji wa utoaji wa huduma mikoani, wilayani na Vituo vya afya kila mwezi na kutoa taarifa kwake.
Prof. Makubi akiangalia duka la dawa lililopo hospitalini hapo akiwa na wakurugenzi wa wizara ya Afya
 Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akiangalia moja ya mashine zilizopo kwenye maabara ya hospitali hiyo
 Mganga Mkuu wa Serikali akitazama moja ya faili la mgonjwa aliolazwa kwenye wodi hiyo ambapo alibaini mapungufu.
 Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akikagua wodi ya wanaume iliyoko hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma.Kushoto ni Muuguzi Mfawidhi wa hospitali hiyo Stanley Mahumbo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad