Katibu
Mkuu Wizara ya Kilimo Bwana Gerald Kusaya (pichani) akitoa maelekezo ya
serikali kuisimamisha Taasisi ya STAWISHA kuendelea kutekeleza shughuli
zake ndani ya eneo la Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) Uyole.Wizara
ya Kilimo( TZ) na ile ya Uholanzi iliingia makubaliano ya kuzalisha zao
la viazi mviringo mwaka 2018 lakini mkataba huo hauonyeshi uwepo wa
STAWISHA .
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.
Gerald Kusaya muda mfupi uliopita; ameagiza kusimamishwa mara kuanzia
leo tarehe 21 Julai, 2020 kwa shughuli za Taasisi ya Kuendeleza zao la
Viazi Mviringo (STAWISHA) ya Jijini Mbeya.
Mradi wa kuendeleza viazi mviringo
unaotekelezwa na Taasisi ya STAWISHA upo ndani ya eneo la Taasisi ya
Utafiti wa Kilimo, Uyole (TARI – Uyole) baada ya kujiridhisha kuwa kuna
dalili za ufisadi na ukiukwaji wa makubaliano ya msingi kati ya
Serikali ya Tanzania na Uholanzi ya mwaka 2018.
Katibu Mkuu Gerald Kusaya
ameyasema hayo muda mfupi baada ya kuongea na Wanahabari katika Ofisi za
Wizara ya Kilimo Jijini Dodoma na kubainisha kuwa Watendaji wa Taasisi
ya STAWISHA wamekiuka lengo kuu la makubaliano katika ya Serikali ya
Tanzania na Serikali ya Uholanzi.
Katibu Mkuu Gerald Kusaya
ameongeza kuwa Mkataba wa makubalio (MoU) kati ya Wizara ya Kilimo
(Tanzania) pamoja na mbia mwenza; Wizara ya Kilimo Chakula na Maliasili
ya Uholanzi ilikuwa ni kuendesha shughuli za utafiti wenye lengo la
kuongeza tija na uzalishaji wa viazi mviringo lakini Watendaji wa
Taasisi ya STAWISHA hawakuwa wakiendesha shughuli za utafiti.
“Katika MoU hakuna neno lililotaja
kuhusu kampuni ya STAWISHA na kuwa eneo wanalotumia kuzalisha mazao kwa
sasa ni mali ya umma. Suala la kuomba kibali cha ujenzi ndani ya eneo
la TARI Uyole na kutumia jina la STAWISHA bila kibali cha Wizara ni kosa
na siwezi kufumbia macho“ alisisitiza Kusaya
Mambo mengine ambayo yamekiukwa na
Watendaji wa Taasisi ya STAWISHA ni pamoja kuendesha shughuli za
uzalishaji wa mazao ya ngano, mahindi jambo ambalo ni kinyume cha lengo
la msingi.
Jambo lingine ni pamoja na
Watendaji wa Taasisi ya STAWISHA kusajili Jina la Taasisi hiyo BRELA kwa
jina la STAWISHA bila kuzingatia kuwa ni huo ni wa ushirikiano kati ya
Serikali hizo mbili kupitia Wizara zao za Kilimo.
Katibu Mkuu Kusaya ameongeza kuwa
STAWISHA haijajiri Mtumishi yeyote wa Wizara ya Kilimo pamoja na kutotoa
hesabu zake kwa Wizara ya Kilimo na kwa Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa
Hesabau za Serikali kwa kipindi cha zaidi ya miaka miwili kwa ajili ya
ukaguzi.
“STAWISHA imefungua akaunti mbili
NMB Mbalizi na watia saini wote ni Watumishi wake. Maana yake Serikali
haijui kiasi gani cha fedha kimeingia kwa kipindi cha toka mwaka 2018
hadi sasa na udhibiti wake upoje”. Amesema Katibu Mkuu Kusaya.
Katibu Mkuu ameongeza kuwa
Watendaji wa STAWISHA waliomba kibali kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu
ndani ya eneo la TARI Uyole huku wakijua wazi kuwa katika mkataba wa
makubaliano ya Serikali hizo mbili hakuna mahali ambapo Taasisi hiyo
STAWISHA imetajwa.
Kufuatia maleozo hayo Katibu Mkuu
Kusaya ametoa maagizo mawili kama ifuatavyo;kwanza kwa kuwa eneo hilo la
ekari 70 ni mali ya serikali amemwagiza Mkurugenzi Mkuu wa TARI
Dkt.Geoffrey Mkamilo kuwasiliana na Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya
kubadilisha kibali cha ujenzi kutoka STAWISHA kuwa TARI Uyole ili
kuepusha mgogoro siku za usoni
Pili, kuanzia leo tarehe
21.07.2020 kampuni ya STAWISHA isimamishe shughuli zote ndani ya eneo la
TARI Uyole na kuondoa mabango yake haraka kwani katika mkataba
uliosaini na serikali ya Uholanzi hautambua kampuni hiyo.
Tatu, Mtendaji Mkuu wa STAWISHA
aandike barua NMB Mbalizi kusimamisha akaunti zote za fedha kufanya kazi
hadi pale majadiliano na Seriklai ya Uholanzi yatakapokamilika kuhusu
uhalali wake.
“Mimi kama Katibu Mkuu Kilimo,
nataka kupata uhalali wa STAWISHA kufanya kazi ndani ya mkataba wetu na
serikali ya Uholanzi.Lengo serilaki inataka kuona manufaa yaliyolengwa
kupatikana kwa zao la viazi yanafikiwa huku tukidumisha mahusiano mema
na serikali ya Uholanzi” Kusaya alisisitiza.
Katibu Mkuu amesema atawasiliana
na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo ya Uholanzi kuhusu masuala yote
yanayoendelea ndani ya makubaliano ya ushirikiano na Serikali ya
Uholanzi.
No comments:
Post a Comment