HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, June 19, 2020

WAANDISHI WA HABARI WAOMBWA KUANDIKA MAMBO MAZURI YANAYOFANYWA NA SERIKALI


Rais wa Muungano wa klabu za Waandishi wa Habari(UTPC)Tanzania Deo Nsokolo kulia, akikabidhi vifaa mbalimbali vya kujikinga na ugonjwa wa Covid 19 unaosababishwa na virusi vya Corona ikiwemo Sanitizer,sabuni ya maji,na Barakoa kwa Mwandishi wa Habari wa kituo cha ITV Mkoani Ruvuma Emmanuel Msigwa wakati wa mafunzo ya siku moja kwa waandishi wa Habari wa mkoa wa Ruvuma juu ya kujilinda,kutambua na kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo,mafunzo yaliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari wa mkoa wa Ruvuma.katikati Katibu msaidizi wa Chama hicho Ngaiwona Mkondola.

Rais wa Umoja wa klabu za Waandishi wa Habari Tanzania(UTPC)Deo Nsokolo akiongea na waandishi wa Habari wa mka wa Ruvuma(hawapo Pichani)jana wakati wa mafunzo ya kuwajengea uelewa waandishi hao juu ya ugonjwa wa Covid 19 unaosababishwa na virusi vya Corona mafunzo yaliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari wa mkoa huo sambamba na utoaji wa vifaa mbalimbali ikiwemo Sanitizer,Barakoa na Sabuni kwa Waandishi wa Habari,katikati Katibu Mkuu wa Chama hicho Andrew Chatwanga.
Picha na Mpiga Picha Wetu,

RAIS wa muungano wa klabu za waandishi Tanzania(UTPC) Deo Nsokolo, ametoa wito kwa waandishi wa habari nchini kuipenda nchi yao, kuwa wazalendo na kuandika mambo mazuri yaliyofanywa na Serikali, badala ya kutumia kalamu zao kukosoa utendaji wa Serikali iliyopo madarakani.

Amesema hayo jana, wakati akiongea na waandishi wa Habari wa mkoa wa Ruvuma katika mafunzo ya kuwajengea uwezo, na jinsi ya kujilinda na ugonjwa wa mapafu makali Covid 19 unaosababishwa na virusi vya Corona, mafunzo yaliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari mkoa wa Ruvuma.

Kwa mujibu wa Nsokolo, sio dhambi hata kidogo mwandishi wa habari kusifia na kupongeza kazi mbalimbali zilizofanywa na Serikali na kusisitiza kuwa,habari za kweli zitawafanya kuheshimiwa, kupendwa na jamii na Serikali.

Aidha Nsokolo, amewaasa waandishi, kuhakikisha wanashirikiana katika majukumu yao ya kila siku badala ya kuchukiana kutokana na tofauti zao za kipato na elimu.

Alisema, kama wana taaluma wanapaswa kuungana na kuepuka chuki baina yao kwani kutokana na unyonge wao, umoja miongoni mwao ndiyo silaha pekee itakayowasaidia kufikia malengo waliyonayo katika maisha yao ya kila siku.

Amewataka waandishi wa Habari hapa nchini kuboresha mahusiano yao na kuandika habari sahihi ambazo zitawezesha wananchi kupata taarifa hasa wakati huu Taifa linapokaribia kufanya uchaguzi Mkuu wa Madiwani,Wabunge na Rais.

Amewatahadharisha waandishi kujiepusha kuandika habari za uongo na zinazo chochea chuki dhidi ya mgombea au chama chochote cha siasa kwani kitendo hicho ni kosa kisheria.

Pia, amewasisitiza waandishi kuendelea kuchukua tahadhari juu ya ugonjwa wa Corona kwa kuwa wao ni kati ya kundi kubwa linalokutana na watu wengi kila siku,hivyo ni muhimu kujiepusha na hatari ya kupata ugonjwa huo.

Amewaomba kuandika habari sahihi juu ya ugonjwa huo ili kuwasaidia wananchi kupata taarifa muhimu dhidi ya ugonjwa wa Covid 19.

Awali katibu wa chama cha Waandishi wa Habari mkoani Ruvuma Andrew Chatwanga alisema, chama hicho kimeandaa mafunzo hayo kama hatua ya kuwajengea uelewa waandishi wa habari juu ya ugonjwa wa Corona.

Alisema, waandishi ni watu ambao kila siku wanakutana na watu tofauti,kwa hiyo mafunzo hayo yatawasaidia namna ya kuepuka, kujikinga na kuchukua tahadhari ya kukabiliana na maradhi hayo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad