HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, April 21, 2020

SERIKALI KUTOA USHIRIKIANO KWA WAWEKEZAJI WATAKAO JITOKEZA KUTENGENEZA BARAKOA NA VITAKASA MIKONO


 Waziri wa Viwanda na Biashara,  Innocent Bashungwa (katikati) akisikiliza kwa makini maelezo ya eneo la uzalishaji kutoka kwa Msimamizi wa Mradi wa Uzalishaji Vitakasa mikono kutoka Kampuni ya Total, Umesh Ankoleker (kulia) leo Aprili 20, 2020 alipokua katika ziara ya Jijini Dar es Salaam ya kutembelea Viwanda vinavyozalisha Barakoa na Vitakasa Mikono.
 Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa (katikati) akipata ufafanuzi kuhusu matumizi ya mashine ya Cherehani katika utengenezaji wa Barakoa kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Uchapishaji cha Five stars, Ashik Abbas Karim (kushoto), leo Aprili 20, 2020 alipokua katika ziara ya Jijini Dar es Salaam ya kutembelea Viwanda vinavyozalisha Barakoa na Vitakasa Mikono.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa (kulia) akipata ufafanuzi kuhusu mtambo wa kutengeneza Barakoa kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Uchapishaji cha Five stars, Ashik Abbas Karim (kushoto), leo Aprili 20, 2020 alipokua katika ziara ya Jijini Dar es Salaam ya kutembelea Viwanda vinavyozalisha Barakoa na Vitakasa Mikono.

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa amebainisha kwamba Serikali imejipanga kuzalisha zaidi ya Barakoa Milioni tatu na nusu kwa mwezi ili kukidhi mahitaji ya Watanzania wote.

Hayo ameyasema leo Aprili 20, 2020 alipokua katika ziara ya Jijini Dar es Salaam ya kutembelea Viwanda vinavyozalisha Barakoa (face mask) na Vitakasa mikono (Hand sanitizer) ambapo kwa siku ya leo ziara hiyo imefanyika katika Kiwanda cha Uzalishaji cha Prestine, Kiwanda cha Uchapishaji cha Five stars na Kiwanda cha Uzalishaji Mafuta na Vilainishi cha Total.

Waziri Bashungwa ameeleza kwamba Uzalishaji wa Barakoa za kutosha kwa sasa ni muhimu sana na Serikali inahakikisha kwamba Viwanda hivi vinapata malighafi ya kutosha ili viendelee kuzalisha vizuri.

“Kiwanda cha Prestine sasa hivi kinatengeneza Barakoa elfu thelathini kwa siku (30,000) lakini baada ya vifaa kuingia kitazalisha elfu hamsini kwa siku (50,000) na Kiwanda cha Five Star kitazalisha barakoa laki moja kwa siku (100,000) hivyo kwa ujumla Viwanda hivi vitazalisha barakoa zisizopungua milioni tatu na nusu kwa mwezi mmoja (3,500,000) hii ni hatua muhimu sana.”alisema Waziri Bashungwa.

Akizungumza kuhusiana na ziara yake katika Kiwanda cha Total Waziri Bashungwa ameeleza kwamba Uongozi umekubali kushirikiana na Serikali katika kuzalisha vitakasa mikono na tayari maandalizi ya awali yamefanyika ikiwa ni pamoja na kuangalia sehemu ambayo itatumika kwa ajili ya uzalishaji.

“Baada ya kuangalia Kiwanda na eneo maalumu ambalo wamelitenga kwa ajili ya uzalishaji wa vitakasa mikono, na kwa uwezo wa kiwanda hiki kwa siku kitakua na uwezo wa kutengeneza lita elfu sita (6000) ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kudhibiti ugonjwa huu.” Aliongeza Waziri Bashungwa.


Katika hatua ya mwisho Waziri Bashungwa ametoa wito kwa watanzania “Natoa wito kwa wazalishaji wengine kujitokeza na Serikali tutawapa ushirikiano wa kipekee, Pia Tuendelea kuzingatia melekezo na kanuni za kujikinga na Maambukizi ya virusi vya Corona (COVID -19).”

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad