HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, March 4, 2020

RC NDIKILO AKABIDHIWA MRADI WA MAJI KISARAWE, AMUOMBA RAIS KUUZINDUA

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amekabidhiwa rasmi mradi wa maji Kisarawe na Mamlala ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam na Pwani (DAWASA) na kumuomba Rais Dkt John Pombe Magufuli kuuzindua.

Hayo ameyasema akiwa anaendelea na ziara yake, Ndikilo ametembelea mradi wa maji Kisarawe akianzia tanki la Kibamba hadi Kisarawe kwenye tenki la kuhifadhia maji.

Ndikilo amemuomba Rais kuuzindua mradi huo ambao umekamilika kama maagizo yake kwa Mamlaka hiyo wakati wa uzinduzi wa Chanzo cha Ruvu Juu  na kuwataka wapeleke maji Kisarawe wameutekeleza ndani ya muda mfupi.

Amesema, angependa kuona Rais anauzindua mradi huo ambao umeondoa kero ya maji ya wananchi wa Kisarawe iliyodumu kwa miaka mingi toka kuanza kwa mji wa Kisarawe mwaka 1907.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi  Cyprian Luhemeja amemkabidhi rasmi mradi huo uliokamilika kwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani wenye thamani ya Bilioni 10.6

Akizungumza na waandishi wa habari,  Luhemeja amesema wameshakamilisha ujenzi wa mradi huo wakitumia miezi 11 na tayari wananchi wameshaanza kupata huduma ya maji safi.

"Mradi huu tulitumia fedha zetu za ndani takribani Bilioni 10.6 na umejengwa kwa kipindi cha muda mfupi sana miezi 11 na maji yanapatikana kwa wingi muda wote,"

"Mahitaji ya wananchi wa Kisarawe ni lita milion 1.2 na tenki linahifadhi maji Lita Milion 6 kwahiyo tumeanza mchakato wa kupeleka maji kwenye eneo la Viwanda na maeneo ya Gongo la Mboto, Ukonga, Banana na maeneo ya jirani,"

Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Jokate Mwegelo ameishukuru serikali ya awamu ya tano na Dawasa kwa kufanikisha upatikanaji wa maji ndani ya Wilaya ya Kisarawe na amewaomba Dawasa kufanikisha upatikanaji wa maji kwenye maeneo ambayo mtandao ws maji haujafika.

Hadi kufikia sasa maunganisho ya wateja wapya 1200 yameshafanyika na wakilaza karibia km 33 za usambazaji wa maji kupeleka kwa wananchi.
 Afisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja akielezea mradi wa Maji ww Kisarawe ulipoanzia katika tenki la maji la Kibamba wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akiwa ameambatana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Theresia Mbando.
 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akielezea jambo kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja wakati wa ziara yake ya kutembelea mradi wa Kisarawe akianzia katika kituo cha kusukuma maji cha Kibamba akiwa ameambatana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Theresia Mbando
Afisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja akimuonesha Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo eneo linalotandazwa mtandao wa usambazaji maji utakaopeleka maji kwenye eneo la Viwanda Kisarawe.
 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo (katikati), Katibu Tawala  wa Mkoa wa Pwani Theresia Mbando, Afisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja wakiangalia katika moja ya chemba inayoruhusu kuingia maji kwenye tenki la Kisarawe yakitokea Tenki la Kibamba.
 Mkurugenzi wa Miundo mbinu na Uwekezaji Mhandisi Ramadhan Mtindasi akimuonesha Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Cyprian Luhemeja eneo litakaloanza kupeleka maji kuelekea Ukonga, Banana hadi Gongo la Mboto.
 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akimtua mama ndoo kichwani kuashiria kuondoa kero ya maji ya muda mrefu katika Mji wa Kisarawe.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Theresia Mbando , Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Jokate Mwegelo, Afisa Mtendaji Mkuu Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja na watendaji wa Dawasa wakati wa ziara ya kutembelea mradi wa maji wa Kisarawe.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad