HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, January 21, 2020

IOM na Uhamiaji Tanzania zashirikiana kuendesha Mafunzo Mpakani mwa Tanzania na Kenya

Shirika la Umoja wa Mataifa la Wahamaji (IOM) kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji wameendesha mafunzo ya elimu kwa umma mapema mwezi huu kuhusu masuala ya uhamiaji mipakani katika kijiji cha Jasini kilichopo katika kata ya Mayomboni, Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga.

IOM Tanzania inatekeleza miradi mingi hapa Afrika hususani nchini Tanzania na sasa wakishirikiana na Idara ya Uhamiaji Tanzania wanatekeleza mradi huu wa kampeni ya utoaji elimu kwa umma kuhusu masuala ya kiuhamiaji mipakani ikiwa na lengo kuu la kutatua changamoto wanazokutana nazo wananchi waishio mipakani na kuwajengea uwezo ili kuwa na uhusiano mzuri wa kuwezesha ulinzi na usalama na hatimae kupambana na uhalifu unaotokea mipakani.

Akifungua rasmi mafunzo hayo ya kuwajengea uwezo wawakilishi wa wananchi, Mkuu wa Wilaya ya Mkinga Yona Maki amelishukuru Shirika la Umoja wa Mataifa la Wahamaji (IOM) na Idara ya Uhamiaji Tanzania kwa kuwaletea fursa hiyo ya mafunzo kwa wananchi wake ili kusaidia kupunguza vitendo vya kihalifu vinavyotokea katika mpaka wa Kenya na Tanzania.

Vitendo hivyo vya kihalifu vinasababishwa na kutokuwa na elimu sahihi ya jinsi ya kuishi mipakani na namna ya kuwabaini wahamiaji haramu ambao wanaweza kuhatarisha usalama wa Taifa na wananchi kwa ujumla.

“Tunapoishi mipakani kuna shughuli nyingi zinafanyika, wengine mnasafirisha magendo, wengine mnasafirisha wahamiaji haramu ili kujipatia fedha, lakini leo wamekuja wataalamu wetu na wanatufundisha madhara ya kufanya shughuli haramu kama hizo ni kosa la jinai hivyo yazingatieni sana mafunzo haya kwa faida ya kizazi cha sasa na baadae” alisema Bwana Maki.

Aidha ameendelea kuishukuru serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuiwezesha Idara ya Uhamiaji kuendelea kutekeleza majukumu yake ipasavyo ikiwa ni pamoja na utoaji elimu kwa umma na wanavyoshirikiana kwa karibu na shirika hili la IOM jambo ambalo limesaidia sana kupungua kwa vitendo vya kihalifu katika mipaka ya nchi yetu hasa katika Mkoa wa Tanga.

“IOM na Idara ya Uhamiaji Wamekuwa ni wadau wetu wakubwa sana kwani wameendelea kutuletea mafunzo kama haya kwa zaidi ya mara tatu sasa wanafika katika maeneo yetu ya Wilaya ya Mkinga na kutupa elimu hii muhimu sana” alisema.
Kwa upande wake Afisa Uhusiano kutoka Idara ya Uhamiaji Makao Makuu Mrakibu Msaidizi, Azizi Kirondomara akitambulisha mada zilizofundishwa alisema washiriki wamefundishwa aina za uhalifu unaovuka mipaka, usafirishaji haramu wa binadamu, usafirishaji kimagendo, ugaidi usafirishaji silaha haramu, uingizaji bidhaa feki, utakatishaji fedha, madawa ya kulevya, uhalifu wa kimtandao, na taratibu za kuingia nchini.

Aidha amebainisha madhara yanayoweza kutokea endapo wahamiaji haramu watapenya na kuingia hapa nchini, ambapo hupelekea kuhatarisha usalama wa Taifa, kuongeza mzigo serikali katika utoaji wa huduma za jamii, kuongezeka kwa vitendo vya kihalifu, kupungua kwa nafasi za ajira, kuchochea migogoro baina ya wafugaji na wakullima na pia wahamiaji holela kushiriki katika chaguzi mbalimbali za serikali.

Afisa uhamiaji mfawidhi wa kituo cha uhamiaji Horohoro, Mrakibu Singwa Mokiwa alibainisha kwamba wasafirishaji wakubwa wa wahamiaji haramu katika wilaya ya Mkinga ni madereva Bodaboda ambao hutumia vipenyo ikiwemo eneo la kijiji cha Jasini hivyo elimu hiyo imefika wakati muafaka ambapo itawasaidia madereva hao kutimiza wajibu wao bila kuvunja sheria na kuilinda nchi yao dhidi ya wahamiaji haramu.

Mrakibu Mokiwa ametoa wito kwa wananchi kwamba mlinzi namba moja wa mipaka ni mwananchi mwenyewe hivyo wananchi wanatakiwa kuwa na uzalendo na nchi yao kwa kuwafichua wahamiaji haramu ikiwemo kutoa taarifa kwa mamlaka husika.

Washiriki wa Mafunzo hayo waliotoka katika makundi mbalimbali ya kijamii walikuwa na matarajio ya kujua sheria za kuishi mipakani, kujua muhusika wa kwanza wa uhamiaji haramu, jinsi ya kumtambua mhamiaji haramu na madhara ya kupitisha wahamiaji haramu katika mipaka ya nchi yetu.

Yote hayo yalipatiwa ufumbuzi na wakufunzi Mrakibu Msaidizi wa Uhamiaji Azizi Kirondomara kutoka Kitengo cha Uhusiano Uhamiaji Makao Makuu, Bi Lucy Mseke Afisa Mradi Msaidizi IOM Tanzania na Bwana David Lukiri Kutoka Shirika la umoja wa mataifa la Wahamaji IOM.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad