HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, July 18, 2019

FINLAND YAIPATIA TANZANIA MSAADA WA SH. BILIONI 24 KWA AJILI YA PROGRAM YA KUPANDA MITI KIBIASHARA

Na Benny Mwaipaja, WFM, Dar es Salaam
Finland imeipatia Tanzania msaada wa Euro milioni 9.4 sawa na zaidi ya shilingi bilioni 24 kwa ajili ya utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Program ya Panda Miti Kibiashara.

Mkataba wa msaada huo umetiwa saini Jijini Dar es Salaam kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Doto James, kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na Kaimu Balozi wa Finland hapa nchini Bw. Kari Leppanen.

“Ninaishukuru Jamhuri ya Finland kwa kutoa msaada huu ukitanguliwa na msaada mwingine kama huo wa Euro milioni 19.5, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 49.8, ambazo Finland ilizitoa kwa ajili ya kutekeleza Awamu ya Kwanza ya Mradi huo kati ya mwaka 2014-2018” alisema Bw. James

Alisema kuwa program hiyo ya Upandaji Shirikishi wa Miti awamu ya Pili, ni mojawapo ya vipaumbele vya juu katika ajenda ya maendeleo ya Serikali, yenye malengo ya kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi.

“Lengo kuu la program hii ni kuchochea upandaji miti endelevu na jumuishi kwa ajili ya kuchangia katika ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini” aliongeza Bw. James

Bw. James alifafanua kuwa program hiyo itasaidia kuongeza mashamba ya misitu itakayoleta faida za kijamii, kimazingira, kifedha katika maeneo ya mradi katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania ikiwemo Ruvuma, Iringa, Njombe na Morogoro

“Program hii pia itaongeza kipato cha wamiliki binafsi wa misitu, Vikundi Vidogovidogo na vya Kati vya Ujasiriamali (SMEs) na Kaya mbalimbali katika eneo la mradi” alisisitiza Bw. James

Alizitaja faida nyingine za mradi kuwa ni pamoja na kuimarisha vikundi wa wapandaji miti kwa kuviwezesha kupata usajili, kuviwezesha kiuongozi na namna ya kujiendesha. 

Aidha, wadau wote wa misitu watajengewa uwezo kupitia upandaji miti na usimamizi wa mashamba hayo, kuongeza uwezo na rasilimali za kudhibiti moto katika mashamba ya miti, kusaidia vijiji kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi na kuongeza ubora wa mazao ya misitu katika mnyororo wa thamani.

Kwa upande wake Kaimu Balozi wa Finland hapa nchini Bw. Kari Leppanen, pamoja na kuipongeza Tanzania kwa ufanisi mzuri katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa program hiyo, alisema Tanzania ni moja ya mataifa yanayofanya vizuri katika usimamizi wa misitu hatua iliyolivutia taifa hilo kushiriki katika kuilinda.

Aliwataka wasimamizi wa program hiyo ya Panda Miti Kibiashara kuhakikisha wanatekeleza ipasavyo majukumu ya usimamizi wa misitu hiyo na hivyo kustawisha hali kijani kwa maendeleo yao na Taifa kwa ujumla.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James walioketi (kulia) na Kaimu Balozi wa Finland hapa nchini Bw. Kari Leppanen, wakisaini hati ya makubaliano ya msaada wa shilingi bilioni 24 ambazo Serikali ya Finland imeipatia Tanzania kwa ajili ya kutekeleza Awamu ya Pili ya Program ya Panda Miti Kibiashara.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James walioketi (kulia) na Kaimu Balozi wa Finland hapa nchini Bw. Kari Leppanen, wabadilishana mikataba ya makubaliano ya msaada wa shilingi bilioni 24 ambazo Serikali ya Finland imeipatia Tanzania kwa ajili ya kutekeleza Awamu ya Pili ya Program ya Panda Miti Kibiashara.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James aliyeketi (kulia) akizungumza na vyombo vya habari wakati wa tukio la kusaini  mkataba wa makubaliano ya msaada wa shilingi bilioni 24 ambazo Serikali ya Finland imeipatia Tanzania kwa ajili ya kutekeleza Awamu ya Pili ya Program ya Panda Miti Kibiashara Leppanen, wabadilishana. Kushoto ni Kaimu Balozi wa Finland hapa nchini Bw. Kari Leppanen.
Kaimu Balozi wa Finland hapa nchini Bw. Kari Leppanen, aliyeketi mbele (kushoto) akizungumza na vyombo vya habari wakati wa tukio la kusaini  mkataba wa makubaliano ya msaada wa shilingi bilioni 24 ambazo Serikali ya Finland imeipatia Tanzania kwa ajili ya kutekeleza Awamu ya Pili ya Program ya Panda Miti Kibiashara Kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WFM)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad