HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, July 6, 2019

DAWASA WAJIPANGA KUWASIMAMIA WAKANDARASI ILI WAMALIZIE MIRADI KWA WAKATI

Zainab Nyamka na Cathbert Kajuna , Globu ya Jamii.

Mkurugenzi wa ukaguzi wa ndani wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) Rosemary Lyamuya amesema wanahakikisha wakandarasi wanafanya kazi kulingana na makubaliano ya mkataba.

Rosemary ameyasema hayo alipotembelea banda la DAWASA lilipo kwenye maonesho ya 43 ya biashara ya kimataifa ndani ya Viwanja vya Mwalimu Nyerere Sabasaba barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam.

Amesema, kazi kubwa inayofanywa na kitengo chao ni kukagua miradi mbalimbali inayosimamiwa na DAWASA ambapo ni miradi ya maji safi na ile ya maji taka.

"Tunakagua miradi yote inayosimamiwa na DAWASA, ile maji safi na maji taka pamoja na kuhakikisha wakandarasi wanafanya kazi kulingana na makubaliano ya mikataba," amesema Rosemary.

Amesema, katika miradi inayokaguliwa na kitengo cha ukaguzi wa ndani (Internal Audit) wanahakikisha miradi inayojengwa na ile iliyomalizika kujengwa inaendana na mkataba pamoja na bajeti iliyopangwa.

Akizungumzia mikataba sita iliyosainiwa mapema wiki hii na Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Cyprian Luhemeja na wakandarasi mbalimbali, Kitengo cha ukaguzi wa ndani  wamejipanga  kusimamia na kukagua miradi yote  na kuhakikisha wakandarasi wanafanya kazi zao na kufuata mikataba inavyosema.

Mbali na hilo, Rosemary ameeleza kuwa inapotokea kuna kuhujumiwa kwenye miundo mbinu ya Dawasa wamekuwa wanatoa ushauri kwenye menejimenti ili wayafanyie kazi.

Ametoa rai kwa wananchi kutoa taarifa pale wanapoona kuna miundo mbinu ya DAWASA inahujumiwa, ikiwemo watu kujiunganishia maji kiholela kwani hilo linasababishia hasara kwa mamlaka na kushindwa kufikia malengo ya asilimia 95 mwaka 2020.
Mkurugenzi wa ukaguzi wa ndani wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es salaam DAWASA Rosemary Lyamuya akizungumza na wanahabari mara baada ya kutembelea banda lao lililopo katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba 2019 yanayofanyika jijini Dar es Salaam ambapo DAWASA wameweka dawati la kuweza kutatua matatizo ya wananchi. Nyuma yake ni Afisa Uhusiano wa DAWASA Joseph Mkonyi.
Mkurugenzi wa ukaguzi wa ndani wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASA) Rosemary Lyamuya (wa kwanza kushoto) akimsikiliza Afisa Ubora Maji wa DAWASA Sizya Mongela wakati akitoa ufafanuzi juu ya kuhifadhi majisafi na salama kwa wananchi waliofika katika banda lao.
Mkurugenzi wa ukaguzi wa ndani wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es salaam DAWASA Rosemary Lyamuya (kulia) akipata maelezo ya vifaa toka kwa wahandisi.
 
Wananchi wakiendelea kupata huduma ndani ya banda la DAWASA katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba 2019.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad