NA DENIS MLOWE, IRINGA
WANAFUNZI wa vyuo vikuu mkoani Iringa wametakiwa kuzingatia zaidi
masomo kuliko kujihusisha na maisha ya starehe ambayo yamekuwa
yakiwagharimu wengi wao kutotimiza ndoto walizojiwekea pindi wafikapo
vyuoni.
Akizungumza katika kongamano kubwa la wanafunzi wa kike wa vyuo vikuu
vilivyoko mkoani hapa makada wa Chama cha Mapinduzi, Naibu Katibu Mkuu
wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Jeska Mbogo amewataka wanafunzi
hao kuzingatia zaidi masomo kuliko kupoteza muda kwenda katika kumbi
za disco na kuwa na mahusiano na wanaume na kusisitiza kuelekeza
akili katika masomo kwa mambo ya kidunia watayakuta .
Mbogo alisema kuwa imekuwa kasumba ya wanafunzi wengi wa kike
kuanzisha mahusiano ambayo hayana faida yoyote katika maisha yao
ambapo baadhi yao wanashindwa kutimiza ndoto zao kutokana na
kujiingiza katika mapenzi katika umri mdogo ama kwa kudanganywa na
makundi rika au kudanganywa kwamba wakijihusha na mapenzi na walimu
watafanya vyema katika mitihani yao.
Alisema kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakijiingiza kwenye mambo ya
anasa na starehe badala ya masomo huku wakisahau kuwa wazazi wao
wanatumia nguvu nyingi katika kuwasomesha kwa gharama kubwa katika
kulipia ada ya masomo na kuja kushawishika na wanaume wasiokuwa na
malengo nao.
Aliongeza kuwa katika maisha ya kila siku endapo unataka kufanikiwa
mwanamke unatakiwa kujitambua nini lengo la kufika chuoni, kujithamini
utu wako, kujielewa na kujiamini kutakuletea mafanikio ambayo
unayataka katika kutimiza ndoto za maisha yako hapo mbeleni.
Mbogo aliwataka wanafunzi hao kujikubali jinsi walivyo kwani ndivyo
Mungu ndivyo alivyowaumba na kuachana na tabia ya kujibadilisha
maumbile kwa kutumia dawa za kachina ili kubadili muonekano wa maumbo
yao ili kuonekana wazuri wakati ni bora kujikubali ulivyo kuliko
kutaka kuisha maisha ya kuwaonyesha watu bila kutambua madhara ya
mbele yatakuwaje.
Katika kongamano hilo, Mbogo alikabidhi kadi zaidi ya 100 kwa
wanafunzi hao kujiunga na Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT) wa CCM
mkoa wa Iringa ambapo wanafunzi hao waliomba kupatiwa mafunzo ya
ujasiriamali katika vyuo wanavyotoka kuweza kujikomboa kiuchumi na
kuwaahidi kuwapatia mafunzo hayo.
Alitoa wito kwa wazazi kutenga muda wa kuwa karibu na Watoto wao na
kuzungumza nao kwani wazazi wengi wamekuwa wako bize kutafuta hela na
kusahau kukaa na kuzungumza na Watoto wao jambo ambalo linazidi
kuendeleza mmomonyoko wa maadili kwa Watoto wao.
Naye Mbunge wa Viti maalum Mkoa wa Iringa, Rose Tweve aliwataka
wanafunzi wa kike kujiamini katika Maisha yao kwani hakuna kitu
kinachoweza kumkomboa mwanadamu kama kujiamini kwani watu wote
waliofanikiwa duniani walijiamini na kuthubutu na ndio maana
wamefanikiwa.
Rose aliwataka vijana hao kutokuwa watu wakulaumu au kulalamika bali
wawe ni watu wa kufanya kazi kwa vitendo kulisaidia Taifa lao kwani ni
fahari sana kusema wewe nimelifanyia nini Taifa lako kuliko kusema
kusema Taifa lako limekufanyia nini .
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Jeska Mbogo akisalimiana na mmoja ya wanawake wa UWT mkoa wa iringa wakati alipofanya ziara ya kikazi mkoani Iringa.
Katibu wa Umoja wa Wanawake Mkoa wa Iringa, Chiku Masanja akiwatambulisha baadhi ya wajumbe wa kamati ya uwt mkoa wa Iringa kwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Jeska Mbogo .
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Jeska Mbogo akizungumza na wajumbe na viongozi wa UWT mkoa wa Iringa.
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Jeska Mbogo , akikabidhi kadi kwa mmoja wa wanafunzi wa kike wa vyuo vikuu mkoani Iringa kujiunga na UWT.
No comments:
Post a Comment