NA MWAMVUA MWINYI, PWANI
JESHI la polisi mkoani Pwani, linawashikilia wahamiaji haramu sita
ambao ni raia kutoka nchini Ethiopia kwa kosa la kuingia nchini bila
kibali, huku likikamata watu wengine 29 kwa kujihusisha na matukio ya
uvunjaji nyumba usiku na kuiba.
Watuhumiwa hao wamekamatwa kufuatia msako mkali na oparesheni dhidi ya
vikundi vya vijana wa mitaani wanaojihusisha na wizi kwa
kuvunja, kupora na kukaba raia wema huko wilaya ya kipolisi Chalinze .
Akielezea kuhusiana na matukio hayo,kamanda wa polisi mkoani
Pwani Wankyo Nyigesa alisema baadhi yao walikamatwa wakiwa na mali
kadhaa,madawa ya kulevya aina ya bangi kete 142,puli nne,pombe haramu
ya moshi lita 25 na pikipiki moja.
Anabainisha kwamba, pia kumekamatwa magunia 90 ya mkaa uliovunwa bila
uhalali ,mashuka,raba,vitenge,mafuta ya pikipiki na mafuta ya kula
yanayodaiwa kuingizwa kwa kukwepa ushuru lita 300.
Akizungumzia kuhusu wahamiaji haramu alisema ,watafikishwa katika
idara ya uhamiaji kwa taratibu nyingine za kisheria.
Kamanda huyo alitoa rai kwa jamii ,kuwa itambue uhalifu haulipi na
hauna faida kwani siku za mwizi ni arobaini na akishikwa mtu
akijihusisha na uhalifu atakiona.
Vilevile anawataka walioibiwa kufika katika kituo cha polisi Chalinze
kutambua mali zao .
No comments:
Post a Comment