HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 12, 2019

SERIKALI KUWAJENGEA UWEZO MAKANDARASI WA NDANI

Na Siti Said
Serikali kuptia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) imesema kuwa ina mpango wa kuwajengea uwezo makandarasi wa ndani ili waweze kutekeleza kazi zao na kuongeza ushindani katika soko la ajira.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Arch. Elius Mwakalinga, jijini Dodoma wakati akifungua kikao kilichoshirikisha wakurugenzi wa Wizara na Taasisi zake pamoja na makandarasi kutoka katika mikoa mbalimbali nchini.
Katibu Mkuu huyo, amesema kuwa Serikali kupitia Wizara yake itaanza kuwawezesha makandarasi hao kwa kuwashirikisha kwenya miradi michache mikubwa ya Wizara inayojengwa na makandarasi wa nje ili kupata taaluma na ujuzi kutoka kwao. 

“Nimeamua kuitisha kikao hiki ili kuwaeleza mikakati ya Serikali ya kuwajengea uwezo na kujadili kwa pamoja changamoto zenu na hatimae kuzitafutia ufumbuzi”, amesema Katibu Mkuu Mwakalinga.
Aidha, amefafafanua kuwa mkakati huo umeanza ndani ya Wizara kwa kuwapeleka watumishi 44 kwenye miradi nane ya ujenzi inayotekelezwa nchini ikiwemo mradi wa daraja la Selander ambapo watumishi hao watashiriki mwanzo hadi mwisho wa utekelezaji wa miradi hiyo. 

Ameongeza kuwa lengo la kufanya hivyo ni kupata wataalamu wazalendo katika miaka ijayo ili nao kutoa elimu walioipata kwa wenzao na hatimaye kupata wataalamu wengi wazalendo watakaosaidia kukuza uchumi wa nchi na kulinda maslahi mapana ya Taifa.
Kwa upande wake, Mhandisi Oscar Lisi kutoka mkoani Mwanza, amemuomba Katibu Mkuu Mwakalinga kuwa mkali na kuchukua hatua katika suala la rushwa kwani amesema kuwa sekta hiyo haiendelei na haikui kutoka na kuingiliwa na rushwa.

Pia mkandarasi huyo ameiomba Serikali kulegeza masharti yaliyomo kwenye mikataba ya zabuni kwani masharti mengi yanaonekana kumnyima fursa mkandarasi wa ndani katika zabuni zinazotangazwa na Serikali.
Naye, Mhandisi kutoka Mbeya, Shakira Kiwanga, amemuomba Katibu Mkuu Mwakalinga, kuwasaidia kuzungumza na mabenki ili kuweza kupata mikopo ambayo itasaidia kuinua na kukuza mitaji yao kwani wengi wao wana hali duni.

Mkutano huo umeshirikisha Makandarasi kutoka mikoa mbalimbali nchini lengo likiwa ni kupata taarifa na mikakati ya Serikali kuhusu taaluma yao.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga, akisikiliza na kunukuu hoja za Makandarasi wa ndani katika kikao cha Katibu Mkuu huyo na makandarasi hao kilichofanyika jijini Dodoma.
 Makandarasi wa ndani kutoka katika mikoa mbalimbali nchini wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga, katika kikao cha Katibu Mkuu huyo na makandarasi hao kilichofanyika jijini Dodoma.
 Mkandarasi wa ndani Valiana Pascal kutoka Mkoa wa Iringa akitoa hoja kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga, katika kikao cha Katibu Mkuu huyo na makandarasi hao kilichofanyika jijini Dodoma.
Makandarasi wa ndani kutoka katika mikoa mbalimbali nchini wakiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga mara baada ya kumaliza kikao cha Katibu Mkuu huyo na makandarasi hao kilichofanyika jijini Dodoma. PICHA NA WUUM

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad