HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 19, 2019

4CCP YASAIDIA MRADI WA MAJI GETANYAMBA

WANANCHI 1,000 kati ya wakazi 4,250 wa Kijiji cha Getanyamba Wilayani Mbulu Mkoani Manyara, wamenufaika na mradi mpya wa maji baada ya kuangaika kwa muda mrefu na changamoto ya kuchota maji korongoni. Hata hivyo, mradi huo utawanufaisha watu 1,000 pekee kwenye kijiji hicho chenye wakazi 4,250 na wengine 3,250 bado wataendelea kukabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji.

Mratibu wa pembe nne za utamaduni Haydom (4CCP) Eliminata Awet akizungumza baada ya mradi huo kuzinduliwa na mwenge wa uhuru alisema umewezeshwa na Norwegian Church Aid (NCA). Awet alisema lengo la mradi huo ni kusaidia kupunguza tatizo la maji kwa wananchi hao waliokuwa wanafuata huduma hiyo kwa kuchota maji korongoni umbali wa kilomita tatu hadi tano.

Alisema hadi kukamilika kwa mradi huo umegharimu sh. 61 milioni ambapo 4CCP ilitoa sh51.9 milioni, wananchi wamechangia nguvu zao zilizothaminishwa sh10 milioni na halmashauri ya wilaya ya Mbulu ikatoa wataalamu. "Faida ya mradi huu ni kuwezesha wananchi hao kupata huduma hiyo kwa ukaribu ili waweze kupata muda zaidi wa kufanya shughuli zao nyingine nyingine za kujiletea maendeleo," alisema Awet.

Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru Mzee Mkongea Ally akizungumza baada ya kuzindua mradi huo aliwapongeza wananchi wa kijiji hicho kwa kushiriki kuufanikisha ikiwemo kubeba kokoto na kuzoa mchanga. "Pamoja na hayo nawashukuru viongozi wa wilaya ya Mbulu kwa ushirikiano na jamii kufanikisha maendeleo ila wananchi wa Getanyamba hakikisheni mnautunza vyema mradi huu," alisema Ally.

Mkuu wa wilaya ya Mbulu, Chelestino Mofuga aliwashukuru wadau wa maendeleo 4CCP kwa kufanikisha mradi huo mkubwa wa maji ambao utasaidia jamii ya eneo hilo. "Mara nyingi 4CCP wamekuwa mstari wa mbele kusaidiana na serikali katika kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo kwa wananchi wetu wa Mbulu, nawashukuru sana tutaendelea kuwaunga mkono," alisema Mofuga.

Mkazi wa kijiji hicho Ezekiel Bayo aliipongeza 4CCP na Norwegian Church Aid kwa kuwezesha mradi huo ambao kwa kiasi kikubwa umewakomboa wananchi wa eneo hilo. "Tulikuwa tunategemea kupata huduma ya maji kutoka kwenye korongo la Haydom ambayo hayakuwa masafi wala salama, ila baada ya kuwepo kwa mradi huu jamii ya eneo hili inafaidika," alisema Bayo.
 Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru Mzee Mkongea Ally akipanda mti kwenye mradi wa maji wa Kijiji cha Getanyamba Wilayani Mbulu Mkoan Mkoani Manyara, wenye thamani ya shilingi milioni 61.9 ambapo 4CCP walitoa shilingi milioni 51.9 na wananchi wakachangia nguvu zilizothaminishwa kwa shilingi milioni 10.
Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Getanyamba Wilayani Mbulu Mkoani Manyara wakishuhudia ufunguzi wa mradi wa maji wenye thamani ya shilingi milioni 61.9 ambapo kituo cha pembe nne za utamaduni Haydom kilichangia shilingi milioni 51.9 na wananchi shilingi milioni 10.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad