HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, May 12, 2019

WAGANGA WA JADI WILAYA YA TUNDURU WACHANGAMKIA VITAMBULISHO VYA WAJASIRIAMALI

Waganga 150 wa Tibaasili na Tibambadala   wilaya ya Tunduru,katika mkoa wa Ruvuma tayari wameshapatiwa  vitambulisho vya wajasiriamali vilivyotolewa na Rais Dkt John Magufuli.

Mratibu wa Tiba asili na Tiba Mbadala wa wilaya ya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole alisema,  idadi hiyo inaweza ikawa imeongezeka hadi kufikia mwishoni mwa wiki iliyopita kwa kuwa  waganga wengi wanakata vitambulisho kwa Watendaji wa vijiji na kata.

Alisema, waganga hao wameitikia  agizo la Serikali Dkt John Magufuli ambapo  kuanzia sasa ni marufuku kwa Waganga wa Tiba Asili na Tiba Mbadala kufanya kazi zao bila ya kuwa na vitambulisho vya Wajasiriamali na vibali vinavyotolewa na Serikali.

Alisema, Serikali inamtaka  kila Mganga kuwa na kitambulisho hicho  ili kumwezesha kufanya kazi zake kwa amani na kuwataka wale ambao wamejificha mashambani au kufanya kazi zao porini kujisalimisha haraka.

Alisema, suala la  vitambulisho vya Wajasiriamali na vibali vya Serikali  halina mjadala  ni lazima wahusika wote watekeleze ili kuondokana na usumbufu unaoweza kujitokeza.

Alisema, kimsingi Serikali inatambua sana kazi hizo na kusisitiza kuwa,wakati umefika kila mmoja kutekeleza na kufuata sheria bila shuruti  badala ya kusubiri hadi  kutiwa nguvuni na vyombo vya dola.

Dkt Kihongole alisema, wanaendelea na msako wa kuwatafuta Waganga ambao hawana vibali vya Serikali  popote walipo na kila atakayekutwa akifanya shughuli zake kinyume na maagizo ya Serikali atachukuliwa hatua.

Mwenyekiti wa Chama cha Waganga wa Tiba asili na Tiba Mbadala  kata ya Misechela Halmashauri ya wilaya ya Tunduru Nampesya Kaweje alisema,mbali na vitambulisho hivyo kuwasaidia katika majukumu yao, vimewaletea heshima kubwa katika jamii ambayo hapo awali iliwaona kama wababaishaji ambao wanajipatia fedha kwa njia  ya udanganyifu. 

Alisema, tangu Serikali iwapatie vitambulisho  hivyo wamekuwa na Uhuru  na amani kubwa na hata wale waliokuwa wakifanya kazi zao porini ambako sio sehemua salama  sasa wamesogea maeneo ya mjini ambako kuna mazingira rafiki na salama kwa wateja wao.

Amempongeza Rais Dkt John Magufuli kwa kazi nzuri anayofanya ya kuimarisha na kuboresha huduma mbalimbali za kijamii na  kutambua kazi zinazofanywa na Waganga wa Tiba asili  na Tiba Mbadala ambazo zimewafanya nao kuwa sehemu ya Wajasiriamali wanaopaswa kuchangia Uchumi wa Nchi kutokana na kipato wanachopata.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Mganga wa Tiba asili na Tiba Mbadala   Bimwana Aziz, ameiomba Serikali kuandaa utaratibu ambao utawanufaisha na kupata kipato   cha kutosha kulingana na kazi wanazo fanya, kwani licha ya kutoa Tiba nzuri kwa wateja  lakini baadhi yao wamekuwa wajanja na kushindwa kutumiza ahadi wanazo ahidi mara wanapofanikiwa jambo lililo changia waganga wengi kubaki maskini.

“tunaiomba Serikali itusaidie kuweka utaratibu mzuri ambao utatuwezesha na sisi kunufaika na jasho letu,kwa muda mrefu tunafanya kazi ya kuwasaidia watu ambao wanakwenda kunufika na kutajirika kutokana na Tiba na maombi yetu lakini sisi waganga tuna hali ngumu sana ya maisha”alisema Bimwana.

Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji cha Liwanga Dau Nguche alisema,wameanza kutekeleza agizo la Mkuu wa wilaya ya Tunduru Juma Homera linalokaza Waganga wa Tiba asili wenye vitambulisho vya wajasiriamali kutozwa fedha.
Mratibu wa Tiba Asili na Tiba Mbadala katika Hospitali ya wilaya ya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole akiongea na Waandishi wa Habari Ofisini kwake jana kuhusiana na Waganga wa Tiba asili na Tiba mbadala walivyochangamkia vitambulisho vya wajasiriamali vilivyotolewa na Rais Dkt. John Magufuli.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad