HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, May 15, 2019

RAIS DKT. SHEIN AZUNGUMZA NA UONGOZI WA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO ZANZIBAR IKULU NDOGO KIBWENI ZANZIBAR

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa uchumi wa Zanzibar umeendelea kuimarika sambamba na ukusanyaji mzuri wa mapato na matumizi yake.

Hayo aliyasema leo, katika ukumbi wa Ikulu ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango wakati ilipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuipongeza Wizara hiyo ya Fedha na Mipango kwa kuendelea kusimamia vyema kuimarika kwa uchumi wa Zanzibar pamoja na mapato na matumizi yanayofanyika.

Alieleza kuwa katika ukusanyaji wa mapato licha ya udogo wake Zanzibar lakini inaonekana ni jinsi gani ilivyopiga hatua na kuweza kupata mafanikio makubwa yanayoonekana.

Hata hiyo, Rais Dk. Shein Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi na watendaji wa Wizara hiyo kuendelea kushirikiana kwa pamoja na kusaidia sambamba na kuaminiana ili mafanikio zaidi yaweze kupatikana.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi wa Wizara hiyo kutoa taarifa kwa wananchi juu ya uendelezaji na mafanikio ya miradi ya Kuimarisha Huduma Za Jamii Mijini (ZUSP) ili wawwze kuelewa namna Serikali yao inavyojitahidi katika kutatua changamoto zilizopo na mafanikio yaliokwisha kupatikana sambamba na matarajio.

Kwa uapande wa ujenzi wa bandari ya Mafuta na Gesi asilia huko Magapwani Rais Dk. Shein alieleza hatua zinazoendlea kuchukuliwa na Serikali huku akieleza ujio wa ujumbe kutoka nchini Indonesia ambao utakuwepo nchini kuanzia Mei 16 hadi Mei 20 kuja kuangalia mradi huo na namna ya kuendeleza ushirikiana na Zanzibar katika uendelezaji wa mradi huo.  
Mapema Waziri wa Fedha na Mipango Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa akitoa taarifa fupi ya Wizara hiyo alieleza kuwa tathmini ya mwenendo wa Uchumi wa Zanzibar inaonesha wazi kwa viashiria vyote kwamba uchumi wake ni imara na unakuwa kwa kasi iliyokusudiwa.

Alieleza kuwa katika mwaka wa 2018 pato la halisi la Taifa lilikwua kwa TZS 2874 Bilioni ikilinganishwa na TZS 2684 bilioni kwa mwaka 2017, sawa na ukuaji wa asilimia 7.1.

Aliongeza kuwa ukuaji wa uchumi kwa mwaka 2018 umetokanja na mambo mengi yakiwemo kuongezeka kwa idadi ya watalii waliofika nchini kwa asilimia 20.1 kufikia watalii 520,809 mwaka 2018  kutoka watalii 433,474 mwaka 2017.

Jengine ni kuongezeka kwa usafirishaji wa zao la mwani, kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao ya chakula, kuongezeka kwa shughuli za sekta  ndogo ya usafirishaji pamoja na kuongezeka kwa muda wa kukaa wageni hasa watalii.

Pamoja na hayo, Balozi Ramia alieleza kuwa jambo la kwanza kabisa kwa umuhimu wake ni kuendelea kuwepo kwa hali ya Amani na utulivu mkubwa hapa nchini hali iliyowapa fursa nzuri wananchi kufanya shughuli zao za maendeleo kwa ufanisi. 

Ne Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza Wizara hiyo kwa mafanikio makubwa iliyopata sambamba na uwasilishaji mzuri wa Mpango Kazi wake.

Nao uongozi wa Wizara hiyo ulieleza mafanikio na matarajio ya miradi ya Kuimarisha Huduma Za Jamii Mijini (ZUSP) ambayo tayari baadhi yake imeshakamilika na mengine imo ukingoni kukamilika kwa upande wa Unguja na Pemba.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Uendelezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) Salum Nasor alieleza mikakati ya uwekezaji inavyotekelezwa huku Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) Juma Ameir akieleza hatua za ujenzi wa Makao Makuu ya Benki hiyo unaoendelea huko Malindi mjini Zanzibar.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein alikutana na uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale chini ya Waziri wake Mahmoud Thabit Kombo ambapo katika taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019 alieleza kuwa Wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii imefanikiwa kuandaa tamasha la Urithi wa Utamaduni wa Mtanzania (Urithi Vestival).


Aidha, alieleza kuwa wizara imepokea vifaa vya kisasa vya kazi za Digitali na kuhuisha nyaraka zilizochakaa kutoka kwa Washirika wa Maendeleo wa Serikali ya Oman vyenye thamani ya zaidi ya TZS 89,204,100 ambavyo ni kwa ajili ya kuhuisha na kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka kwa matumizi ya sasa na baadae.

Pia, waziri Kombo alieleza kuwa Wizara hiyo imeandaa kwa mara ya kwanza kwa kushirikiana na sekta binafsi Tamasha la Utalii la Zanzibar ambalo lilifunguliwa rasmi na Rais Dk. Shein Novemba 17 mwaka jana 2018 katika hoteli ya Verde Mtoni Zanzibar.

Sambamba na hayo, Waziri huyo alieleza mafanikio ya Wizara kwa kuwasiliana na Kampuni ya DSTV ambayo inarusha matangazo yake karibu duniani kote, ambapo hatua za kufungua ofisi hapa Zanzibar zimekamilika ambapo hivi sasa wanafanya matengenezo ya jingo la ofisi lililopo Mlandege Unguja hatua ambayo pia itopanua soko la ajira katika tasnia ya utangazaji.

Nae Rais Dk. Shein kwa upande wake aliipongeza Wizara hiyo kwa mafanikio yaliopatikana pamoja na kupongeza hatua zilizochukuliwa hadi kufikia Kampuni ya DSTV kurusha matangazo ya Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) moja kwa moja.
 RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein, azungumza na Uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, katika mkutano wa Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa kipindi cha Julai 2018 hadi March 2019, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar, kulia Katibu Mkuu Kiongozi Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee , Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Balozi Mohammed Ramia Abdulwawa. (Picha na Ikulu) 
 WAZIRI wa Fedha na Mipango Zanzibar Balozi Mohammed Ramia Abdulwawa (katikati) akisoma taarifa ya mpango kazi ya Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar wakati wa mkutano huo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein, uliofanyika katika Ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar kulia Katibu Mkuu Kiongozi Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee. 
 RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, katika mkutano wa Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa mwezi wa Julai 2018 hadi March2019, uliofanyika katiuka ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.15-5-2019.
 KATIBU Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar Ndg. Khamis Mussa akisoma ripoti ya Matumizi na Mapato ya Wizara yake wakati wa Mkutano wa Utekelezaji wa Mpango Kazi kwa mwezi Julai 2018 hadi March2019, uliofanyika katuika ukumbi Mdogo wa Ikulu Kibweni Zanzibar. 
 KATIBU Mtendaji Tume ya Mipango Zanzibar Ndg. Juma Reli akichangia wakati wa mkutano wa Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu  Ndogo Kibweni Zanzibar, 
 MKURUGENZI Mtendaji wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar Bi. Sabra Issa Machano, akichangia wakati wa mkutano huo wa Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar kwa mwezi wa Julai 2018 hadi March 2019, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.
 MKURUGENZI Mtendaji wa Benki ya Watu wa Zanzibar Ndg. Juma Ameir Hafidh, akichangia wakati wa mkutano huo wa Utekelezaji wa Mpangio Kazi wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, uliofanyika Ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.


MAOFISA wa Idara mbalimbali za Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar wakifuatilia mkuttano huo wa Utekelezaji wa Mpango Kazi kwa mwezi Julai 2018 hadi March 2019, uliofanyika ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.(Picha na Ikulu)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad