HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, April 16, 2019

PSSSF Yawalipa Wastaafu 9900

Na Jacquiline Mrisho - MAELEZO

Mfuko mpya wa Hifadhi ya Jamii wa PSSSF umekamilisha kulipa malimbikizo ya deni la wastaafu wapatao 9971 lililorithiwa kutoka katika mfuko wa PSPF.

Hayo yamesemwa leo Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Mussa Sima alipokuwa akimuwakilisha Waziri mwenye dhamana ya Mifuko ya Jamii kujibu swali la Mbunge wa Mbozi, Mhe. Paschal Haonga lililohoji juu ya muda gani wastaafu katika Halmashauri za Wilaya nchini watalipwa fedha zao.

Sima amesema kuwa mfuko huo umekamilisha mfumo wa ulipaji mafao utakaowezesha kufanya malipo katika ngazi ya Mkoa na hivyo kuwezesha mfuko kulipa mafao ndani ya muda uliowekwa kisheria wa siku 60 tangu mwanachama anapowasilisha madai.

"Hadi kufikia Februari 2019, mfuko wetu umetoa kiasi cha shilingi Bilioni 888.39  kwa ajili ya kuwalipa wastaafu waliotoka katika mfuko wa PSPF", alisema Sima.

Akizungumzia kuhusu tetesi za Serikali kutumia vibaya fedha za PSPF, Sima amesema kuwa mifuko hiyo inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ambayo inasimamia muundo wa utawala na mfumo wa maamuzi na usimamizi wa uwekezaji wa fedha za mfuko, hivyo, si kweli kwamba Serikali inaweza kuingilia uendeshaji wa mifuko ya hifadhi ya jamii au kufanya maamuzi ya uwekezaji.

Aidha, Sima amefafanua kuwa sheria za mifuko hiyo  chini ya Kanuni Namba 24 na 25 ya Kanuni mpya za Mafao ya Hifadhi ya Jamii za Mwaka 2018 zimetoa wigo mpana zaidi kwa wanachama waliochangia kwa miaka isiyopungua 10 kuweza kupata huduma hiyo tofauti na awali.

Naibu Waziri huyo aliongeza kuwa mifuko hiyo inaendelea kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wanachama wake kupitia vikundi vya kuweka na kukopa katika maeneo ya kazi, mifuko hiyo inaweza kutoa mikopo kwa SACCOs hadi asilimia 10 ya rasilimali za mfuko.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad