HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 29, 2019

KAMATI NDOGO YA ARDHI YAKUTANA JIJINI DODOMA KUJADILI MUSTAKABALI WA WANAWAKE KUMILIKI ARDHI NCHINI

Na Anthony Ishengoma
Kamati ya Uwezeshaji Wanawake katika Umiliki na Matumizi ya Ardhi inakaa leo Jijini  Dodoma  kujadili na kuhainisha fursa na vikwazo  vya kuwezesha umiliki wa ardhi kwa wanawake na kupanga mikakati ya kufikia lengo la wanawake kumiliki na kutumia ardhi kwa maendeleo yao.

Akifungua Kikao cha Kamati hiyo mapema leo Jijini Diodoma Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Patrick Golwike amewaambia wajumbe wa kamati hiyo kuwa kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kinajaadili namna bora ya kuwawezesha wanawake kumiliki na kutumia  ardhi katika kujiletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aidha Golwike ameongeza kuwa pamoja na kuwepo kwa sheria na jitihada mbalimbali kutoka kwa wadau wa kusaidia wanawake kunufaika na ardhi bado kuna vikwazo vinavyoathiri wanawake kumiliki ardhi kwa sababu mbalimbali zikiwemo mila na desturi, ufahamu mdogo wa umiliki ardhi ikiwemo ukosefu wa dhamana za kiuchumi.

Golwike amewataka wajumbe wa kamati hiyo kupitia kwa Taasisi wanazotoka kuwa wabunifu wakwenda na ubunifu wa sayansi na teknolojia katika kuwawezesha wanawake kumiliki na kutumia ardhi kama njia ya kujikwamua kiuchumi.

Akitoa ufafanuzi kwa vyombo vya habari vilivyotaka kujua hasa lengo la Kamati hiyo ndogo ya Ardhi Mkurugenzi wa Idara ya Jinsia wa Wizara ya Afya Idara Kuu Maeandeleo ya Jamii Julius Mbilinyi amesema kuwa Kamati hii iliundwa ili kufikia Malengo Endelevu na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano kwa kuhakikisha wanawake wanapata fursa ya kumiliki ardhi na kuitumia kujiletea maendeleo.

Aidha Mbilinyi ameongeza kuwa kamati ndogo ya ardhi imejiwekea mikakati ya kuhakikisha wanawake wanaondokana  na  vikwazo vya muda mrefu kama vile mila na desturi ili waweze kutumia fursa ya kumiliki ardhi na kuitumia kujiendeleza kiuchumi na kuwa Sehemu ya uchumi mpana wa Nchi yetu.

‘’Suala kubwa sio umiliki wa ardhi kwa wanawake lakini pia ni kuangalia namna bora wanawake hawa wanaitumia fursa ya mali hisa ya ardhi kujiletea maendeleo ili wawe sehemu ya uchumi mpana wa Taifa letu”. Aliongeza Mbilinyi.

Wakati huohuo Marry Ndalo kutoka Shirika la Kimataifa la Care ameongeza kuwa Kamati hiyo kimsingi inawakutanisha wadau kutoka Mashirika yasiyo ya Kiserikali na kuwaweka pamoja kujadiliana masuala ya ardhi lakini pia kupata taarifa kuhusu idadi ya Wanawake wanaomiliki ardhi na wasio miliki ardhi ili kuweka wanawake katika mjadala wa ardhi ambao inaajiri wanawake wengi.
 Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Patrick Golwike kulia pamoja na Mwakilishi kutoka Shirika la Kimataifa la Care Marry Ndalo wakiwa tayari kwa ufunguzi wa kikao cha Kamati Ndogo ya Ardhi kujadili suala la umiliki wa ardhi kwa wanawake mapema leo Jijini Dodoma.
  Mkurugenzi wa Idara ya Jinsia wa Wizara ya Afya Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Julius Mbilinyi kushoto pamoja na Mwakilishi kutoka Shirika la Kimataifa la Care Marry Ndalo wakiwa tayari kwa ufunguzi wa kikao cha Kamati Ndogo ya Ardhi kujadili suala la umiliki wa ardhi kwa wanawake mapema leo Jijini Dodoma.
 Picha ya pamoja ya Kamati ndogo ya Ardhi mara baada  ufunguzi wa kikao cha Kamati Ndogo ya Ardhi kujadili suala la umiliki wa ardhi kwa wanawake kilichofanyika katika ofisi mpya za Wizara ya Afya zilizoko Mtumba Jijini Dodoma.
Baadhi ya Washiriki wa Kamati ndogo ya Ardhi inayokutana leo Jijini Dodoma kujadili suala la umiliki wa ardhi kwa wanawake katika ukumbi wa Wizara ya Afya Mtumba Jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad