HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, April 14, 2019

Benki ya CRDB yatangaza ufanisi mwaka 2018 huku faida yake ikiongezeka maradufu

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela akizungumza wakati wa Benki hiyo ikitangaza faida nono ya TZS 64.1 bilioni ambayo ni ongezeko la asilimia 77% kutoka TZS 36.2 bilioni iliyoipata mwaka 2017, katika hafla fupi iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Serena, jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki.

Benki ya CRDB imetangaza faida nono ya TZS 64.1 bilioni ambayo ni ongezeko la asilimia 77% kutoka TZS 36.2 bilioni iliyoipata mwaka 2017.

Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema ongezeko la faida hiyo limetokana na kuimarika kwa mazingira ya biashara na jitihada binafsi za benki kutoa huduma zinazokidhi mahitaji na matarajio ya wateja.

“Mwaka 2018 ulikuwa wa mafanikio kwa Benki ya CRDB. Mapato na faida yetu viliongezeka kutokana na kuimarika kwa mapato halisi ya riba na mapato halisi yasiyo ya riba. Tulifanikiwa pia kuongeza kiwango cha mikopo huku tukishusha uwiano wa mikopo chechefu.
Mkurugenzi wa Fedha wa Benki ya CRDB, Frederick Nshekanabo akifafanua jambo kwa wadau na wanahabari wakati Benki hiyo ikitangaza faida nono ya TZS 64.1 bilioni ambayo ni ongezeko la asilimia 77% kutoka TZS 36.2 bilioni iliyoipata mwaka 2017, katika hafla fupi iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Serena, jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki.

Mikopo tuliyotoa kwa wateja iliongezeka sambamba na amana za wateja huku tukiwafikia wateja wapya kupitia huduma za kidijitali kama vile SimBanking, SIMAccount, mawakala wetu wa CRDB Wakala na kuanzisha mfumo mpya wa baadhi ya matawi yetu madogo kuendeshwa na mawakala binafsi. Tukiwa na mtaji wa kutosha pamoja na ukwasi unaokidhi mahitaji ya uendeshaji, tumeuanza mwaka 2019 tukiwa na uwezo wa kuwapa wateja wetu huduma bora zaidi na kuongeza thamani kwa wadau wetu,” amesema Nsekela.

Akieleza zaidi kuhusu mafanikio hayo, Nsekela alisema: “Tunajivunia ukweli kwamba tupo kwenye uelekeo mzuri kufanikisha malengo yetu tuliyojiwekea. Lengo si kutyafikia tu, bali Tunakusudia kuyavuka. Tutaongeza kasi zaidi ya utendaji hususani katika ubunifu na utoaji wa huduma za kidijiti zenye ubora wa juu. Tutaendelea kuimarisha na kupitia mara kwa mara mifumo yetu ya utoaji huduma kwa wateja ili kuhakikisha kuwa tunakidhi mahitaji ya soko.”
Mwaka 2018, mapato halisi ya riba ya Benki ya CRDB yaliongezeka kwa TZS 33.1 bilioni na kufika TZS 442.8 bilioni kutoka TZS 409.7 bilioni za mwaka 2017 ambalo ni ongezeko la asimia 8.1 lililotokana na kuimarika kwa mapato ya riba sambamba na kupungua kwa gharama za riba.

“Tumejipanga kutoa huduma kwa namna inayohamasisha uwajibikaji miongoni mwa mteja wetu ndio maana tunajielekeza zaidi kuwapa elimu ya fedha ili kurahisisha jinsi wanavyoweza kukopa na kurejesha kwa wakati,” amesema Bwana Nsekela.

Katika mwaka huo, uwiano wa jumla ya mikopo na mikopo Benki isiyolipika au chechefu ulipungua kwa asilimia 4.1 na kufika asilimia 8.5 kutoka asilimia 13.6 uliokuwapo mwaka2017. “Tumepunguza uwiano huo mpaka wastani wa asilimia 8 na tunataka ushuke mpaka chini ya asilimia 5 mwakani. Hili litawezekana kwa kunyumbua utaratibu wa marejesho ya wateja na kusimamia kw aukaribu mikopo tunayoitoa,” amesema mkurugenzi.
Mkurugenzi wa Masoko, Utafiti na Huduma kwa Wateja wa Benki ya CRDB, Tully Esther Mwambapa akitoa muongozo katika hafla hiyo.

Bwana Nsekela alifafanua kwamba kupungua kwa uwiano wa mikopo isiyolipika ni ishara dhahiri ya kuimarika kwa utoaji na ukusanyaji wa mikopo kulikowezeshwa kwa kiasi kikubwa na kuanzishwa kwa dawati la Usimamizi wa Mali na matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa kukusanya marejesho (e-collect) ambao unaratibu na kufuatilia taarifa za wateja.

“Mfumo wa kielektroniki wa kukusanya marejesho unaturahisishia kufuatilia mwenendo wakopaji wetu hivyo kutuweka jirani zaidi na wateja wetu jambo linalomaanisha tunaweza kushauri wakati wowote inapoonekana una dalili ya kufanya vibaya kuepuka mikopo isiyolipika,” amesema.

Ndani ya mwaka huo vilevile, mali za Benki ziliongezeka kwa asilimia 2.3 kutoka TZS 5.9 trilioni Desemba 2017 hadi TZS 6 trilioni mwaka 2018. Ongezeko hilo, tunaamini limetokana na mpango mkakati wa Benki kuongeza kiasi cha mikopo inachotoa ili kuimarisha mapato yatokanayo na riba.

Maeneo muhimu ya ufanisi wa mwaka 2018

· Amana za wateja ziliongezeka kwa asilimia 7.8 na kufika TZS 4.66 trilioni kutoka TZS 4.33 trilioni za mwaka 2017.

· Thamani ya mali za benki ilikua kwa asilimia 2.3 na kufika TZS 6 trilioni kutoka TZS 5.9 trilioni za mwaka 2017.

· Mapato ya riba yaliongezeka kwa asilimia 4.6 hadi TZS 586.3 bilioni kutoka TZS 560.3 bilioni za mwaka 2017.

· Mapato halisi ya riba yaliongezeka kwa asilimia 8.1 na kufika TZS 442.8 bilioni kutoka TZS 409.7 bilioni za mwaka 2017.

· Faida ghafi iliongezeka kwa asilimia 85 na kufika TZS 99.1 bilioni kutoka TZS 53.6 bilioni ya mwaka 2017.

· Faida halisi (baada ya kodi) ilikua kwa asilimia 77 ikifika TZS 64.1 bilioni ikilinganishwa na TZS 36.2 bilioni za mwaka 2017.

· Mikopo iliyotolewa kwa wateja wetu iliongezeka kwa asilimia 8 na kufika TZS 3.1 trilioni ikilinganishwa na TZS 2.9 trilioni iliyotolewa mwaka 2017.







No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad