HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, March 7, 2019

WAZIRI KIGWANGALA ATOA MSIMAMO VITA DHIDI YA UJANGILI, ASEMA ASKARI WANAOLINDA HIFADHI WANAFUATA SHERIA.

Waziri wa Maliasili na Utalii,  Dkt. Hamisi Kigwangala amewataka Watanzania kuondokana na dhana iliyojengeka miongoni mwao kuwa watumishi wa Wizara hiyo hususan  wahifadhi wa  wanyamapori na Misitu  ni watu katili  wanaowatesa Wananchi.

Kauli hiyo ameitoa leo wakati akifungua mkutano wa 26 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika katika Chuo cha Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi jijini Mwanza.

Amesema watumishi hao ni watu wenye utu na weledi wa hali ya juu na wanaozingatia  sheria katika kutimiza majukumu yao na hulazimika kutumia nguvu wakati wakipambana na majangili wanaokutwa katika maeneo ya hifadhi wakifanya vitendo vya ujangili.

‘’ Ulinzi wa Rasilimali za nchi ni jukumu letu sote, wizara imepewa dhamana ya kusimamia na kuongoza kwa niaba ya watanzania, kama kuna watumishi wa Wizara hii wanaowanyanyasa wananchi naomba walete ushahidi kwetu ili tuwachukulie hatua’’ amesema Dkt. Kigwangala.

Waziri Kigwangala amesikitishwa na idadi ya watumishi walipoteza maisha kwa ajali na wengine kuuwawa na majangili wakati wakipambana nao katika maeneo yote ya hifadhi  nchini na kutoa wito kwa wananchi wote wenye taarifa au ushahidi juu ya vitendo vyovyote vya kihalifu kuziwasilisha katika mamlaka zinazohusika.

Amesema kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaojihusisha na vitendo vya ujangili na uhalifu katika maeneo ya hifadhi na wale wote wanaoshirikiana na makundi ya watu wenye nia ovu ya kukwamisha juhudi za uhifadhi wa rasilimali za Taifa.

Ametoa wito kwa wananchi kuheshimu sheria za uhifadhi na kuepuka kuvamia maeneo ya hifadhi kwa shughuli za kijamii na ufugaji akitoa wito kwa viongozi mbalimbali wa Siasa kuunga mkono juhudi za wizara za ulinzi wa maeneo ya hifadhi kwa kuwaelimisha wananchi wanaowaongoza kujiepusha na vitendo vya uvamizi wa maeneo ya hifadhi badala ya kuwatetea.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Prof.Adolf Mkenda akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho amesema kuwa jumla ya watumishi 23 walifariki dunia  wakati wakitekeleza majukumu ya uhifadhi   na   5 walijeruhiwa na majangili wakiwa kazini.

Prof. Mkenda amesema kuwa waliofanya vitendo hivyo  hawaitakii mema Tanzania na ni maadui wa shughuli za uhifadhi nchini akiongeza kuwa Serikali itaendelea kusimama na kuwatetea watumishi na askari wa wanyamapori wanaotimiza majukumu yao kwa kuzingatia sheria.
 Katibu Mkuu wa  Maliasili na Utalii Prof, Adolf Mkenda akizungumza na watumishi wa Wizara hiyo (hawapo Pichani) wakati wa ufunguzi wa baraza la 26 la Wafanyakazi wa Wizara hiyo liliofanyika  leo Jijini Mwanza.

 Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangala akisisitiza jambo  wakati akizungumza na Watumishi wa Wizara hiyo kuhusu umuhimu wa kutekeleza maagizo kwa wakati yanayotolewa na Viongozi wa Wizara hiyo katika kikao cha Baraza la 26 la  Wafanyakazi wa Wizara hiyo  kilichofanyika leo Jijini Mwanza.
 Naibu Waziri wa  Maliasili na Utalii Mhe,Constantine Kanyasu akizungumza na Watumishj wa Wizara  hiyo katika kikao cha Baraza la 26 la  Wafanyakazi kilichofanyika leo Jijini Mwanza.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla, Naibu Waziri  wa Wizara, Mhe, Constantine Kanyasu wakiwa wameshikana na watumishi wengine  hukuwakiimba wimbo wa mshikamano Daima katika Kikao cha Baraza la 26 la Wafanyakazi kilichofanyika leo jijini Mwanza.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akiwa ameambatana na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Constantine Kanyasu wakati akikagua gwaride la Jeshi Usu katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Pasiansi.
Wafanya kazi wa  Maliasili na Utalii wakiimba wimbo wa mshikamano Daima katika Kikao cha Baraza la 26 la Wafanyakazi wa Wizara hiyo kilichofanyika leo jijini Mwanza.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad