Na Teresia Mhagama, Katavi
Imeelezwa kuwa, Serikali imetenga fedha za ndani, kiasi cha Dola za
Marekani milioni 70 kwa ajili ya kazi ya ujenzi wa njia ya kusafirisha
umeme ya msongo wa kV 132 kutoka Tabora hadi Katavi ambayo itawezesha
Mkoa wa Katavi kuunganishwa na gridi ya Taifa.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani mkoani
Katavi wakati alipofanya ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya umeme
katika Wilaya ya Mpanda, Nsimbo na Tanganyika ambapo aliambatana na
Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Amos Makalla.
“Serikali imeamua kujenga mradi huu ili Mkoa wa Katavi uachane na
kutumia umeme wa mafuta ambao ni ghali kwani shilingi milioni 21
zinatumika kila wiki kuendesha mitambo hii, hivyo gharama za
uendeshaji zinakuwa kubwa tofauti na mapato yanayoingia.” Alisema Dkt.
Kalemani.
Alieleza kuwa, njia hiyo ya umeme ya kV 132 itakuwa na urefu wa
kilometa 284 na inatarajiwa kukamilika mwezi Juni mwaka 2020 kwani
taratibu za ujenzi zimeshaanza.
Akiwa katika kituo cha kuzalisha umeme cha Mpanda, Dkt Kalemani
alisema kuwa, mwaka jana kituo hicho kilikuwa na mashine mbili zenye
uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 2.6 lakini mwaka huu imeongezwa
mashine ya tatu na kufanya kituo hicho kuwa na uwezo wa megawati 3.75,
hivyo kukidhi mahitaji ya umeme ya Mkoa wa Katavi kwa sasa.
Aidha, Dkt Kalemani aliwapongeza wafanyakazi wa TANESCO katika Kituo
hicho kwa kutumia shilingi milioni 100 tu kwa kazi ya uboreshaji wa
kituo pamoja na uhamishaji wa mashine hiyo ya tatu ya kufua umeme
ambayo ilikuwa wilayani Loliondo.
“ Nataka niwapongeze watumishi hawa wa TANESCO kwani Mkandarasi kutoka
Uholanzi alisema kuwa gharama atakayotumia kwa ajili ya kazi hiyo ya
uhamishaji wa mashine ni shilingi bilioni mbili lakini niliagiza
wataalam wetu kuwa tuihamishe wenyewe na wametumia shilingi milioni
100 tu.” Alisema Dkt Kalemani.
Katika ziara yake wilayani Nsimbo, Waziri wa Nishati alikagua kazi ya
usambazaji umeme katika Kijiji cha Kapalala ambapo pia aliwasha umeme
katika Kijiji hicho na kumuagiza mkandarasi kampuni ya CRCC kupeleka
umeme katika vitongoji vyote vya Kijiji hicho.
Vilevile, katika ziara yake wilayani Tanganyika, Dkt Kalemani alikagua
kazi ya usambazaji umeme katika Kijiji cha Mchakamchaka na Ifukutwa na
kuwasha rasmi umeme katika Vijiji hivyo.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa pili kutoka kushoto) na Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Amos Makalla (wa kwanza kushoto) wakiwa katika Mkutano na wananchi wa Kijiji cha Kapalala (hawapo pichani) wakati walipofika kijijini hapo kukagua kazi ya usambazaji umeme vijijini.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (kushoto) akizungumza na Bi. Salma Karamba, mkazi wa Kijiji cha Ifukutwa wilayani Tanganyika Mkoa wa Katavi ambaye ameunganisha umeme kwenye nyumba yake kupitia mradi wa usambazaji umeme vijijini wa Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akikata utepe kuashiria kuwashwa rasmi kwa umeme katika Kijiji cha Ifukutwa wilayani Tanganyika Mkoa wa Katavi.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani ( wa pili kushoto) akikagua
mitambo ya umeme wa mafuta katika kituo cha kuzalisha umeme cha Mpanda
wilayani Katavi. Kituo hicho kinazalisha umeme wa kiasi cha megawati
3.5.
No comments:
Post a Comment