HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, March 5, 2019

Serikali Yajipanga Kuziwekea Mikataba Taasisi Zake

Na Jacquiline Mrisho - MAELEZO
Serikali kupitia wizara ya maji imejipanga kuleta utaratibu wa kuziwekea mikataba ya utendaji kazi taasisi zilizopo chini ya wizara hiyo ili kuimarisha usimamizi wa sekta ya maji katika ngazi mbalimbali nchini.

Hayo yamezungumzwa leo Jijini Dodoma na Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa wakati alipokuwa akifungua mkutano uliowahusisha  Makatibu Tawala wa Mikoa nchini kwa ajili ya kujengeana uelewa wa pamoja kuhusu uendeshaji mpya wa sekta ya maji kufuatia kupitishwa kwa sheria mpya ya Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira Sheria Namba 5 ya mwaka 2019.

Prof. Mbarawa amesema kuwa wizara imeamua kuja na mikataba hiyo itakayokuwa na malengo maalum ya kuzipima taasisi kwa kila mwaka mmoja ambapo nia ya serikali sio kumkomoa mtendaji bali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma iliyokusudiwa.

“Mamlaka hizi zikisimamiwa kwa malengo zitafanya kazi vizuri zaidi na zitakuwa na uwezo mkubwa wa kujiendesha pia kupimana utendaji kazi ni jambo zuri kwa sababu tukifanya kazi kimazoea mamlaka na taasisi zetu hazitoweza kufanya kazi vizuri wala kuimarisha utoaji wa huduma za maji safi na salama kwa wananchi wetu,” amesema  Prof. Mbarawa.

Ameendelea kusema kuwa, mkutano huo ni sehemu ya utekelezaji wa agizo la Mhe. Rais Magufuli alilolitoa mwezi Mei, 2018 kuhusu mfumo wa uendeshaji wa sekta ya maji ambapo aliagiza sekta ya maji isimamiwe na wizara moja ili kurahisisha usimamizi na uwajibikaji wa watendaji.

Nae Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Prof. Kitila Mkumbo amefafanua kuwa Sheria ya Huduma za Maji na Usafi wa Mazingira Namba 12 ya mwaka 2009 imepitiwa na kutungwa upya na kwa sasa inajulikana kama Sheria ya Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira ya mwaka 2019 ambapo kikubwa katika sheria hiyo ni kuanzishwa kwa Wakala wa Maji Vijijini.

“Haitawezekana kukamilisha mipango ya sekta ya maji bila ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa hivyo kupitia mkutano huu Makatibu Tawala watapata nafasi ya kupitia na kuielewa sheria mpya kwa kina na kubaini nafasi zao katika usimamizi na uendeshaji wa sekta ya maji kwenye sheria hii," amesema Prof. Mkumbo.

Kuanza kutumika kwa sheria hiyo mpya kutaimarisha mfumo wa utoaji huduma za maji na usafi wa mazingira nchini, kutaongeza ufanisi na uwajibikaji katika kutoa huduma za maji, kutaimarisha ujenzi na usimamizi na uendeshaji wa miradi ya maji, kutachochea utendaji katika sekta  nyingine na kuongeza mchango wa sekta ya maji katika uchumi wa nchi.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Prof. Kitila Mkumbo akizungumza na Makatibu Tawala wa Mikoa nchini (hawapo pichani) walioshiriki katika mkutano wa kujengeana uelewa wa pamoja kuhusu uendeshaji upya wa sekta ya maji kufuatia kupitishwa kwa sheria mpya ya Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira Sheria Namba 5 ya mwaka 2019. Ufunguzi huo umefanyika leo Jijini Dodoma.
 Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa akizungumza wakati akifungua mkutano uliowahusisha Makatibu Tawala wa Mikoa nchini kwa ajili ya kujengeana uelewa wa pamoja kuhusu uendeshaji upya wa sekta ya maji kufuatia kupitishwa kwa sheria mpya ya Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira Sheria Namba 5 ya mwaka 2019. Ufunguzi huo umefanyika leo Jijini Dodoma.
Mwenyekiti wa Makatibu Tawala wa Mikoa nchini, Mama Rehema Madenge akitoa neno la shukrani baada ya Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa kufungua mkutano huo.
 Baadhi ya Makatibu Tawala wa Mikoa nchini na wafanyakazi wa Wizara ya Maji waliohudhuria katika mkutano huo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad