HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, March 26, 2019

KIWANDA CHA UNGA WA MUHUGO CHA KISASA CHAZINDULIWA NCHINI


 Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa (MB) akivuta pazi pamoja na mwenyekiti wa kampuni ya Cassava Starch of Tanzania Corporation, Gerald Billet kuashiria ufunguzi wa kiwanda cha unga wa muhogo cha CSTC katika kijiji cha mbalala mkoani Lindi.
 Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa akikata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua kiwanda cha kampuni ya Cassava Starch of Tanzania Corporation (CSTC) cha unga wa muhogo wenye kiwango cha juu katika kijiji cha mbalala, kata ya Nyegedi, mkoani Lindi. Wengine kutoka kulia ni Mhe. Omary Mgumba (MB), naibu waziri wizara ya kilimo, mkuu wa wilaya ya Lindi, Mhe. Shaibu Ndemanga, mwenyekiti wa kampuni ya CSTC bwana Gerald Billet, Balozi wa ufaransa nchini Tanzania, Mhe. Frederic Clavier, Mkurugenzi mtendaji wa CSTC bwana Christophe Gallean na mbunge wa jimbo la Mtama mkoani Lindi, Mhe. Nape Nnauye.
 Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa (MB) kiwasha mashine ya mihogo wakati wa ufunguzi wa kiwanda cha unga wa muhogo cha kampuni ya CSTC mkoani Lindi. 
 Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa (MB) kipewa maelezo kuhusu taratibu za kiwanda cha unga wa muhogo baada ya kukifunguwa rasmi katika kijiji cha Mbalala, mkoani Lindi.
Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa (MB) akiangalia mihogo inavyopita kwenye mashine wakati wa ufunguzi wa kiwanda cha unga wa muhogo cha kampuni ya CSTC mkoani Lindi.


KIWANDA cha kisasa cha kuzalisha unga wa muhogo wenye kiwango cha juu cha kampuni ya ulimaji na usindikaji muhogo ya Tanzania ijulikanayo kama Cassava Starch of Tanzania Corporation – CSTC kimefunguliwa rasmi na Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (MB) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo Christophe Galléan.

Kiwanda hicho ambacho ni cha aina ya kipekee katika soko la Tanzania kina uwezo wa kuzalisha zaidi ya tani 1 ya unga wa Muhogo wenye kiwango cha juu ndani ya saa  moja na kadiri ya tani 6,000 kwa mwaka.

Akifunguwa kiwanda hicho Waziri Mkuu alitoa pongezi kwa kampuni hiyo kwa kuchangia juhudi za serikali katika kuinua uchumi kupitia viwanda. Aliipongeza kampuni hiyo kwa uwekezaji mkubwa waliotekeleza katika mkoa wa Lindi kwa kujenga kiwanda hicho cha kisasa ambacho kitaendeleza kilimo cha muhogo na pia kutoa ajira kwa wakazi wa mkoa huo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa CSTC, Christophe Galléan alisema "Tunafurahi kuanzisha rasmi kiwanda cha kwanza cha ubora wa hali ya juu na cha kisasa nchini Tanzania. Tunajivunia sana uwepo wa kiwanda hiki na taswira inayoipa kampuni yetu ya CSTC, mkoa wa Lindi na Tanzania kwa ujumla. Tunashukuru sana kwa ushirikiano wa serikali chini ya uongozi wa Rais John Magufuli, na utekelezaji wako Waziri Mkuu Kassim Majaliwa. "

Cassava Starch of Tanzania Corporation iilianzishwa miaka saba iliyopita ikiwa na makao yake makuu mkoani Lindi ikiwa na lengo kuu la kuuza ndani na nje ya nchi unga wa muhogo wenye ubora wa hali ya juu kabisa. Kiwanda hicho ambacho kipo kimkakati karibu na bandari ya Mtwara kitakuwa na uwezo wa kusafirisha bidha zake katika masoko muhimu duniani yakiwemo ya Afrika ya Mashariki na Kusini, Mashariki ya Kati, Marekani na Ulaya.

Mfumo wa utendaji wa CSTC ni kukuza mazao yenye ubora wa hali ya juu katika mashamba makubwa yenye ufanisi na kusimamiwa na CSTC. Vilevile kusindika mazao yote katika kiwanda kilichopo eneo la karibu, Mfumo huu wa utendaji unaofuatwa na CSTC wa kuzalisha mazao na kuwa na kiwanda cha usindikaji ni wa kipekee katika soko la unga wa muhogo la Afrika. 

CSTC ilianza kufanya kazi mwaka 2012 nchini ikiwa na wafanyakazi zaidi ya 400 ambao kati yao asilimia 97 ni Watanzania. "Tunaendelea kuongeza wafanyakazi, kutoa mafunzo na kuendelea kutoa fursa kwa vijana wengi za uongozi katika ngazi zote za uendeshaji kuanzia kiwandani, mashambani na katika shughuli za utawala" alisema Mr Galléan.

Kampuni ya CSTC ina mpango wa kujenga kiwanda cha kusindika wanga kutoka kwenye muhogo katika siku za usoni na kiwanda hicho kitategemea kutoa ajira zaidi kwa Watanzania. Mipango hii itanufaisha jamii kwa ajira, miundo mbinu na huduma za kijamii ambazo zinaendelea kutolewa katika vijiji mbali mbali mkoani Lindi. Kwa kuanzia, CSTC imewekeza katika elimu kwa kujenga darasa la shule ya msingi,ujenzi wa barababara na kukarabati miundombinu ya maji katika kijiji cha Lipome.

Hapo baadaye, CSTC itaanzisha mpango wa wakulima wadogo ambao utahusisha utoaji mafunzo kwa wakulima ili wajifunze njia mpya na za kisasa za kilimo, kuanzia maandalizi sahihi ya ardhi kwa ajili ya kuweza kuzalisha mazao bora na kuongeza mavuno ya mazao yao.  Lengo la programu hii pia ni kuwawezesha wakulima wadogo kuweza kuzalisha mazao kwa gharama nafuu na hivyo kuongeza ushindani wao katika soko la muhogo.
 
"Inashurtisha katika usindikaji wa mazao kufanyika ndani ya masaa 24 baada ya mavuno. CSTC inaanzisha  mpango huo wa kutoa mafunzo ya kilimo kwasababu miundombinu katika mavuno ni muhimu sana. Tunatafuta washirika ambao tutatekeleza nao mradi huu na kuweka malengo sahihi ili kuweza kufaidisha sekta ya kilimo katika kanda hii,” alisisitiza Mkurugenzi Christophe Galléan.

Christophe Gallean pia alimalizia kwa kuishukuru serikali kwa ushirikiano wake kwa CSTC na kueleza kuwa ana shauku kubwa kuanza upanuzi wa viwanda na mashamba ya kampuni hiyo hapo baadaye.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad