HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, February 15, 2019

WATUMISHI 3 MANISPAA YA SONGEA WASIMAMISHWA KAZI KWA KUSABABISHA HASARA YA MILIONI 118

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme ameagiza kusimamishwa kazi mara moja kwa watumishi watatu wa idara ya fedha  wa halmashauri ya Manispaa ya Songea  Mndeme ametoa agizo hilo leo Ijumaa wakati alipohutubia kikao cha Baraza la Madiwani maalum kwa ajili ya kupitisha bajeti ya mwaka 2019/2020 ya Halmashauri ya Manispaa ya Songea.
Amemtaja mtumishi  Mhasibu (Cashier) Juliana Rocky Likunguwala kwa kosa la kusababisha hasara ya shilingi milioni mia moja na kumi na nane ambazo imebainika alizichukua kwa njia ya kutoa risiti bandia za wateja.

 Mkuu huyo wa mkoa amesema mhasibu huyo  kwa kipindi cha miezi mitano tangu Julai 2018 hadi Novemba 2018 ameibia Manispaa ya Songea kiasi cha shilingi milioni 118  za Manispaa ya Songea.  “Mtumishi huyu Juliana Rocky anatuhumiwa kutoa risiti bandia kwa wateja wanaoleta fedha za makusanyo ya mapato ya ndani ili ziingizwe kwenye mfumo wa malipo ya serikali” amesema mkuu wa mkoa. Mndeme amesema uchunguzi uliofanyika ulibaini kuwa mhasibu huyo alishindwa kupeleka fedha benki kwa mujibu wa utaratibu.

“Fedha hizi zilizoibwa zingeweza kujenga zahanati na hata madarasa kusaidia maendeleo ya wananchi ,lakini zimeibwa na mtumishi wa umma kinyume cha utaratibu” Mndeme amesema serikali haitosita kuchukua hatua kali kwa watumishi wanaojihusisha na ubadhirifu. Aidha anatuhumiwa kwa kosa la kuchukua fedha za serikali na kutumia kwenye masuala binasfi kinyume na taratibu na sheria za fedha za umma.

Kufuatia agizo hilo ,mkuu wa mkoa alimwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma SACP Gemin Mushy kumtafuta na kumkamata mhasibu huyO mara moja na kutiwa mahabusu. “RPC  mtafute Juliana popote alipo na umweke ndani masaa 48 akisubiri utaratibu wa kisheria wa kumfikisha mahakamani kutokana na ubadhirifu wa fedha za umma” aliagiza Mndeme. Wakati huo huo Mkuu wa mkoa wa Ruvuma ameagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea  Tina Sekambo kuwasimamisha kazi watumishi wawili wa Idara ya Fedha.

Amewata watumishi hao kuwa ni Mtunza Hazina wa Manispaa ya Songea Denis Mwaitete kwa kosa la kushindwa kusimamamia idara ya fedha hata kupelekea ubadhirifu wa fedha Tsh 118 milioni
Mtumishi mwingine aliyetajwa kusimamishwa kazi ni Mhasibu wa Mapato wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea  Salum Mwaru  kwa kosa la kushindwa kusimamia vema makusanyo ya fedha za mapato ya ndani .

Mkuu wa mkoa Mndeme amechukua uamuzi wa kuwasimamisha kazi watumishi hao kufuatia uchunguzi uliofanywa na timu ya mkoa kuhusu mwenendo wa ukusanyaji mapato ya ndani katika Halmashauri za mkoa wa Ruvuma kutofanya vizuri mwaka 2018/2019
 Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme akizungumza na Madiwani na watendaji wa mitaa na kata wa Manispaa ya Songea leo kuhusu udhibiti wa mapato ya ndani ya serikali.
Sehemu ya Madiwani na watendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea wakifuatilia maelekezo ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma alipowahutubia leo .Lengo la kikoa hicho ni kuelezea umuhimu wa kuongeza kasi ya ukusanyaji mapato ya ndani ya serikali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad