HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, February 6, 2019

KAMPUNI YA UTURUKI YAONESHA NIA KUWEKEZA KATIKA SEKTA ZA UCHUKUZI, UTALII, NISHATI, USAFIRI WA ANGA NA UJENZI

Na OWM, DODOMA.
Kampuni ya MNG Group of Companies ya nchini Uturuki imeonesha nia ya kufanya uwekezaji mkubwa nchini katika sekta mbalimbali; zikiwemo sekta za Uchukuzi, Utalii, Nishati na Usafiri wa Anga.

Uwekezaji huo umebainishwa na Mwenyekiti wa Bodi ya MNG Group of Companies, Mehmet Gunal, wakati alipokutana na  Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Mhe. Angellah Kairuki (Mb), jijini Dodoma, tarehe 5 Januari 2019.

Waziri Kairuki amebainisha kuwa nia ya serikali ya awamu ya tano ni kuhakikisha uwekezaji wenye tija nchini, na kwa kutumia mfumo wa sera ya  Ushirikiano baina ya sekta Binafsi na Umma inahakikisha inavutia wawekezaji zaidi nchini.

“Tunazo fursa na miradi inayohitaji mitaji ya uwekezaji hapa nchini, jukumu letu ni kuhakikisha wawekezaji mnapata mazingira wezeshi katika fursa na miradi mnayotaka kuwekeza ili nchi iweze kupata tija kutokana uwekezaji huo” Amesisitiza  Mhe. Kairuki.

Akiongea katika kikao hicho mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya MNG Group of Companies, Mehmet Gunal, amefafanua kuwa , Kampuni hiyo iko tayari kuwekeza nchini katika Sekta mbalimbali, kwa kuwa wamevutiwa na mazingira ya uwekezaji ya hapa nchini.

Aidha, Gunal alifafanua kuwa wamejipanga kutumia  fursa na miradi yenye kuhitaji uwekezaji nchini ili kuweza kufanya uwekezaji mkubwa , pia alisema kampuni yake ipo tayari kuwekeza hata kwa mfumo wa sera ya ushirikiano baina ya Sekta ya Binafsi na Umma au kuwekeza wao wenyewe.

Kampuni ya MNG Group of Companies inao uzoefu katika masuala ya uwekezaji kwa miaka 42 katika mabara matatu Duniani, ikiwa  imejikita katika uwekezaji  kwenye sekta sita na tayari hadi hivi sasa imetekeleza miradi zaidi ya mia mbili  katika mabara hayo.

Baadhi ya Miradi ambayo imetekelezwa na Kampuni hiyo ni pamoja na , Bwawa la kufua Umeme la Chief Dam la nchini Algeria,  Ujenzi wa uwanja wa Ndege wa Kimataifa  KOTOKA (terminal III),  wa  nchini Ghana, Ujenzi wa makao makuu  ya na Benki ya Halk nchini Uturuki.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi, Isack Kamwelwe, Wataalamu wa masuala ya Uwekezaji na maendeleo ya Sekta Binafsi   wa Ofisi ya Waziri Mkuu, pamoja na wataalam kutoka   Kituo cha Uwekezaji nchini.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki akiongea na wawekezaji toka nchini Uturuki katika Kampuni ya MNG Group of Companies, wakati walipofanya kikao ofisini kwake juu ya fursa na miradi ya uwekezaji nchini tarehe 5 Januari, 2019, jijini Dodoma.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Mhe. Angellah Kairuki akiwasikiliza wataalamu wa masuala ya uwekezaji wa Ofisi ya waziri Mkuu wakati wa kikao na wawekezaji toka nchini Uturuki katika Kampuni ya MNG Group of Companies (hawapo pichani), wakati walipofanya kikao ofisini kwake juu ya fursa na miradi ya uwekezaji nchini  tarehe 5 Januari, 2019, jijini Dodoma.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji),  Angellah Kairuki  pamoja na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi, Isack Kamwelwe, wakiwa katika kikao na wawekezaji toka nchini Uturuki katika Kampuni ya MNG Group of Companies wakati walipofanya kikao juu ya fursa na miradi ya uwekezaji nchini tarehe 5 Januari, 2019, jijini Dodoma.
 Wawekezaji toka nchini Uturuki katika Kampuni ya MNG Group of Companies wakifuatilia kikao na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki  (hayupo pichani), wakati walipofanya kikao juu ya fursa na miradi ya uwekezaji nchini, tarehe 5 Januari, 2019, jijini Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki  akimkabidhi Kitabu chenye Fursa na Miradi yenye Uhitaji Mitaji ya Uwekezaji nchini , Mwekezaji toka nchini Uturuki ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya  Kampuni ya MNG Group of Companies mara baada ya kufanya kikao juu ya fursa na miradi ya uwekezaji nchini tarehe 5 Januari, 2019, jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad