HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, January 18, 2019

Kilimanjaro Marathon yazinduliwa rasmi Moshi

Mbio maarufu za Kilimanjaro  Premium Lager Marathon 2019 zimezinduliwa rasmi kimkoa katika viwanja vya Kibo Palace Homes, Mjini Moshi  kwa kushirikisha viongozi mbalimbali, wadhamini, Chama Cha Riadha Mkoa wa Kilimanjaro (KAAA), waandaaji wa mbio hizo na wadau mbalimbali.

Akizindua mbio hizo, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mh. Anna Mghwira aliwapongeza wadhamnini na waandaaji wakiongozwa na Kilimanjaro Premium Lager 42km, Tigo-21km Grand Malt 5km  na wadhamini wengine wa meza za maji kwa kazi nzuri na kusema wamezifanya mbio hizi ziwe maarufu zaidi na pia wameendelea kuutagaza Mkoa wake wa Kilimanjaro. 

Mkuu huyo wa Mkoa aliipongeza Kilimanjaro Premium Lager kwa kutoa hamasa kwa watanzania ambapo mwanaume na mwanamke wa kwanza kumaliza mbio za kilometa 42 atapata Sh milioni 1.5 kila mmoja na wa pili watapata Sh milioni 1 kila mmoja. “Hii iwe changamoto kuwafanya watanzania wakimbie kwakasi zaidi ili washinde hata zawadi nyingine kubwa zinazotolewa na waandaaji.

Alitoa wito kwa wafanya biashara kutumia fursa hii vizuri kwani wakati huu wa Kilimanjaro Marathon ndio muda wa kufanya biashara tofauti tofauti. “Wenye mahoteli anzeni kufikiria kutoa ofa mbalimbali ili washiriki watenge muda zaidi wa kukimbia lakini pia kufanya utalii na wenye mabaa na makampuni mbalimbali mnaweza kuandaa promosheni ya wiki nzima kutangaza biashara zenu 

Alipongeza wadhamini wengine wakiwemo KK Security, Keys Hotel, Kilimanjaro Water, TPC Sugar, Simba Cement, AAR, Kibo Palace, Barclays Bank na Precision Air na waandaaji  Wild Frontiers, Deep Blue Media na Executive Solutions ambao ni waratibu wa kitaifa.

Akizungumza katika uzinduzi huo Meneja Mauzo na Usambazaji wa TBL, Mwamba Stanslaus alisema Kilimanjaro Premium Lager inajivunia kudhamini mbio hizo kwa miaka 17 sasa kutokana na weledi na uzoefu mkubwa wa waandaaji ambao wamefanya mbio hizo ziwe maarufu sana na moja ya matokeo makubwa nchini huku mwaka huu kauli mbiu ikiwa ‘Mbio ya Watu.’

Alisema kwa mwaka huu, Kilimanjaro Premium Lager imejiandaa vizuri kwani itatoa zawadi zenye thamani ya Tsh milioni 20 ambapo mshindi wa kwanza wa mbio za kilometa 42 kwa upande wa mshiriki mwanaume na mwanamke watapata tsh milioni 4 kila mmoja lakini pia imetoa ofa ya milioni tano kwa watanzania watakaomaliza wa kwanza na wa pili ambapo mwanaume wa kwaza na mwanamke watapata sh milioni 1.5 kila mmoja na wa pili watapata Sh milioni 1 kila mmoja.

Alisema mbio maarufu zakilometa 5 maarufu kama Fun Run, zinazodhaminiwa na Grand Malt pia zitafanyika ambapo watu wa rika zote wanaruhusiwa kushiriki. “Hizi ni mbio za kujifurahisha kwa hivyo watu wa rika zote wanakaribishwa kushiriki ili pia iwe kama sehemmu ya mazoezi huku wakipata kinywaji chao cha Grand malt chenye afya tele,” alisema na kuongeza kuw ambi hizo zimeendelea kuwa maarufu.  

Kwa upande wake, Meneja wa Tigo Kanda ya Kaskazini, Lilian Mwalongo alisema: “Tigo tunajivunia kuwa wadhamini wakuu wa mbio maarufu za Tigo Kili Half Marathon kwa mwaka wa nne mfululizo. Tukiongoza sokoni kwenye mageuzi ya maisha ya kidijiti yakiwamo masuala ya fedha, tunafurahi kwa mara nyingine tena kuwezesha usajili na malipo kwa washiriki kwenye mashindano hayo yajayo kupitia kwa huduma zetu kamilifu za fedha - Tigo Pesa.  

Alisema kwamba kwa miaka kadhaa sasa, Tigo Pesa imethibitishwa kuwa bora zaidi na mfumo wa kuaminika wa malipo kwa wanariadha wote wenye nia kutoka sehemu yoyote nchini.  “Zaidi ya hapo, tunakaribisha kila mmoja kwa ajili ya kupata kumbukumbu za mashindano hayo na kutumia wengine kupitia mtandao wenye kasi zaidi Tanzania wa 4G+,” akasema.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Kili Marathon Race John Addison, kuna mipango ya kusisimua kwa ajili ya mbio hizo za mwaka huu, ikiwa ni pamoja na wikiendi ya sherehe itakayokuwa ikifanyika mjini Moshi, bustani mwanana ya Kilimanjaro Lager kwenye uwanja mbio zitakakomalizikia pamoja na ubunifu mwingine kadhaa kama picha kwa ajili ya njia maalumu kwa kila mshiriki wa marathion na half marathon.

“Washiriki waendelee kujisajili kupitia mtandao na kufanya malipo kwa kutumia credit card kupitia  www.kilimanjaromarathon.com  au kupitia TIGO Pesa -  Pigal *149*20# kisha fuata maelekezo,” alisema na kuongeza kwamba washiriki wajisajili mapema ili kuepuka usumbufu kwani usajiliutafungwa Februari 7,2019 au nafasi zitakapojaa.
 Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mh. Anna Mghwira akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mbio maarufu za Kilimanjaro  Premium Lager Marathon 2019 katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya Kibo Palace Homes, Mjini Moshi.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira  (wa pili kushoto) na Meneja Mauzo na Usambazaji wa Kampuni ya Bia Tanzania, Mwamba Stanslaus wakionesha nembo ya Mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon 2019 ili kuashiria uzinduzi wa mbio hizo kimkoa. Wengine kutoka kushoto ni , Meneja wa Tigo Kanda ya Kaskazini Lilian Mwalongo, Mwenyekiti wa Chama Cha Riadha Mkoa wa Kilimajaro Livingstone Mtacha, mwakilishi kutoka Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi Jaffar Kiongo, Mkuu wa wilaya ya Moshi Kippy Warioba, Ofisa Mkuu wa Mauzo na Masoko wa Kibo Palace Patricia Maina na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi, Raymond Mboya. Uzinduzi huo ulifanyika katika viwanja vya Kibo Palace Homes Mjini Moshi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad