HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, January 10, 2019

Dkt. Kalemani aridhishwa na kasi ya uboreshaji wa kituo cha umeme cha Zuzu

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani ameeleza kuridhishwa kwake na kasi ya kampuni ya KEC ya nchini India ambayo imepewa kazi ya kujenga miundombinu ya umeme katika Kituo cha kupooza umeme cha Zuzu, Dodoma ambacho kinachoongezewa megawati 400 mbali  ya megawati 48 za sasa.

Dkt. Kalemani ameyasema hayo leo jijini Dodoma baada ya kufanya ziara ya kukagua vituo mbalimbali vya kupooza umeme ikiwemo cha Msalato, Mnadani na Zuzu ambapo aliambatana na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, watendaji kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wizara ya Nishati.

Hata hivyo, Dkt Kalemani ameeleza kuwa, mkandarasi huyo anapaswa kukamilisha kazi hiyo mwezi januari mwakani ili kuweza kuboresha zaidi hali ya upatikanaji umeme jijini Dodoma ambapo kazi ya uunganishaji umeme kwa wananchi inaendelea na hivyo kuongeza matumizi ya nishati hiyo muhimu.

Dkt. Kalemani amesema kuwa,  mkandarasi huyo anafanya kazi tatu ambazo ni kushusha umeme kwa kV 400 katika kituo hicho, kujenga kituo cha kupoza umeme cha uwezo wa megawati 400 na kusambaza umeme katika maeneo mbalimbali mkoani Dodoma.

Ameongeza kuwa, mkandarasi huyo alianza kazi hiyo mwezi Machi mwaka 2018 ambapo gharama ya mradi huo ni Dola za Marekani milioni 53 ambazo zimetolewa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania, Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA).

Aidha, baada ya kukagua vituo hivyo vya kupooza umeme, Dkt Kalemani amewaagiza TANESCO kuhakikisha kuwa kila kituo kinakuwa na fundi sanifu atakayekuwa kituoni kwa masaa 24 ili inapotokea hitilafu ya umeme, iweze kutatuliwa kwa haraka.

Vilevile, Dkt Kalemani ameagiza kuwa, kila kituo kiwe na vifaa vya ziada vya umeme badala ya kusubiri kuagiza vifaa hivyo mara linapotokea tatizo hali inayopelekea wananchi kukosa umeme na kueleza kuwa ifikapo mwezi Machi mwaka huu atakagua utekelezaji wa agizo hilo na Meneja ambaye hatatekeleza, atachukuliwa hatua.

Aidha ametoa agizo kwa TANESCO kuweka walinzi katika miundombinu ya umeme kwani kumekuwa na matukio ya baadhi ya wananchi kuhujumu miundombinu hiyo kwa namna mbalimbali ikiwemo kukata nguzo za umeme na pia ametoa wito kwa wananchi kuwa walinzi wa miundombinu husika.

Katika ziara hiyo pia Waziri wa Nishati alizungumza na wafanyakazi wa TANESCO katika kituo cha kupoza umeme kilichopo mjini Dodoma ambapo pamoja na kuwapongeza kwa kazi wanazofanya, alionya kuwa, katika mwaka 2019, mfanyakazi atakayeonekana amefanya uzembe utakaopeleka kukosekana kwa umeme, atachukuliwa hatua.
 Baadhi ya mitambo ya umeme katika kituo cha kupooza umeme cha Zuzu jijini Dodoma.
 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa kwanza kushoto) akizungumza na wafanyakazi wa TANESCO katika kituo cha Mjini Dodoma mara baada ya kukagua miundombinu ya umeme katika Kituo hicho. Wa pili kushoto ni Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga.
 Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga (kushoto) akitoa maelezo kwa Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani kuhusu mitambo ya umeme katika kituo cha kupoza cha Mjini Dodoma.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akikagua maendeleo ya ujenzi wa vituo vya kupooza umeme katika eneo la zuzu Jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad