HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, January 4, 2019

AGIZO LATOLEWA KWA WANAOJENGA JENGO LA WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI KUENDELEA KULIPWA KWA WAKATI

 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akipewa maelezo ya ujenzi wa jengo la wizara na Mkandarasi Msimamizi wa SUMA JKT Injinia David Pallangyo, katika Mji wa Serikali Jijini Dodoma
Baadhi ya wafanyakazi wanaojenga jengo la Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika Mji wa Serikali Jijini Dodoma wakiendelea na hatua mbalimbali za ujenzi wa jengo hilo.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega, amemtaka mkandarasi SUMA JKT anayejenga jengo la wizara hiyo katika Mji wa Serikali Jijini Dodoma, kuhakikisha anaendelea kuwalipa wafanyakazi wanaojenga jengo hilo kwa wakati pamoja na kuhakikisha ubora wa jengo hilo unaendana na thamani hali pesa.

Mhe. Ulega amesema hayo leo (04.01.2019) mara baada ya kufika katika mji huo uliopo Kata ya Mtumba, kwa ajili ya kufanya tathmini ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la awali la Wizara ya Mifugo na Uvuvi na kuonesha kuridhishwa na kasi ya ujenzi inavyoendelea na kumtaka mkandarasi kukamilisha ujenzi huo kwa wakati.

“Unamlipa mtu kabla jasho lake halijakauka palepale unakuwa tayari umeshampa ndiyo dini inavyosema, ni jambo jema sana maana hawa mafundi wanasema wanalipwa kwa wakati, sisi muda wowote tutakuwa tunakuja hapa tunataka hii kazi imalizike kwa wakati na kwa viwango” Amesema Mhe. Ulega.

Mhe. Ulega amefafanua kuwa siyo jambo jema endapo kutatokea taarifa mara baada ya kumalizika kwa mradi wa ujenzi wa jengo la Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kuwa wafanyakazi waliokuwa wakijenga jengo hilo wanamdai mkandarasi ilhali wizara imemlipa pesa zote mkandarasi huyo SUMA JKT ili aweze kufanya kazi kwa wakati.

Kwa upande wake Mkandarasi Msimamizi wa SUMA JKT Injinia David Pallangyo ambaye anasimamia ujenzi wa jengo la Wizara ya Mifugo na Uvuvi amesema ujenzi wa jengo hilo unaenda kwa kufuata mpangilio wa ratiba wa shughuli kwa kila tarehe na kwamba hadi kufikia mwisho wa mwezi Januari mwaka huu jengo litakuwa katika hatua za mwisho.

Ziara ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega kufanya tathmini ya ujenzi wa jengo la wizara katika Mji wa Serikali jijini Dodoma ni mwendelezo wa ziara za viongozi wa juu wa wizara zenye lengo la kuhakikisha jengo hilo la awali la wizara ambalo limetengewa Shilingi Bilioni Moja kutoka serikali kuu linakamilika kwa wakati na kuanza kutumika.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad