HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, December 21, 2018

WAZAZI WATAKIWA KUWA JIRANI NA WATOTO WAO ILI WASIJIINGIZE KATIKA MAOVU

Na Dotto Mwaibale
WAZAZI nchini wametakiwa kuwa jirani na watoto wao jambo litakalosaidia kupunguza ndoa za utoto na kujiingiza katika vitendo viovu kama matumizi ya dawa za kulevya.

`Mwito huo umetolewa na Diwani wa Kata ya Temeke, Faisal Hassan wakati wa hafla ya kuzindua Taasisi ya Tanzania Kwanza Foundation (TAKWAFO) uliofanyika Mtaa wa Ruvuma Mwembe Yanga jijini Dar es Salaam juzi.

" Mnajua wazazi ndio wanaochangia asilimia 70 ya watoto wao kujiingiza katika vitendo visivyofaa zikiwemo ndoa za utotoni kwa kuwa wao ndio walezi wa kwanza wa watoto hao" alisema Hassan.

Alisema katika suala la malezi ya watoto si la serikali peke yake bali ni la kila mmoja wetu hivyo uanzishwaji wa taasisi hiyo katika Kata ya Temeke ni hatua kubwa ya maendeleo pia itakuwa ni mkombozi kwa vijana kutokana na shughuli zake kujikita zaidi kusaidia vijana na kuwa Temeke ina changamoto kubwa kwa vijana kujihusisha na vitendo viovu.

Alisema wao wakiwa viongozi wanakila sababu ya kuunga mkono taasisi hiyo ambapo amewataka wajiunge katika vikundi waweze kupata mikopo kwani katika Manispaa ya Temeke zimetengwa sh.milioni 40 kwa ajili ya kuwakopesha vijana, walemavu na wanawake hivyo amewataka wachangamkie fursa hiyo.

Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Hidaya Shomvi alitaja shughuli wanazozifanya kuwa ni kutoa elimu ya uzazi salama,kulea watoto Yatima, kuzuia ndoa za utotoni na kutoa elimu jinsi ya  kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya na utunzaji wa mazingira na kuwa taasisi hiyo ipo mikoa yote ya Tanzania Bara.

Alitaja changamoto kubwa walionayo ni kuwa na makazi ya kudumu ya kulelea watoto yatima na ukosefu wa pesa ambapo aliwaomba wadau mbalimbali kusaidia taasisi hiyo.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Ruvuma, Simba Ulanga, alisema ujio wa taasisi hiyo katika eneo hilo ni faraja sana kwao kutokana na shughuli za ujasiriamali zinazofanywa na taasisi hiyo kwani wananchi watapata fursa ya kujifunza kazi mbalimbali kama usindikaji wa karanga, kutengeneza batiki na vyungu vya kuoteshea maua badala ya kukaa bure bila ya kazi.
 Diwani wa Kata ya Temeke,Faisal Hassan (kushoto), akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Taasisi ya Tanzania Kwanza Foundation (TAKWAFO) uliofanyika Mtaa wa Ruvuma Mwembe Yanga jijini Dar es Salaam jana. Kulia ni Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Hidaya Shomvi na Mwenyekiti wa Serikali aMtaa Matumbi, Khatibu Lindi.
 Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Hidaya Shomvi , akizungumza na waandishi wa habari.
 Baadhi ya watoto wanaosaidiwa na taasisi hiyo wakiwa kwenye hafla hiyo.
 Msanii Hemed Mwelevu akitoa burudani kwenye uzinduzi huo.
 Bidhaa zinazotengenezwa na wajasiriamali wa taasisi hiyo.
 Msanii Happynes Starley, akitoa burudani.
 Wananchi wakiwa katika hafla hiyo.
 Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Ruvuma, Simba Ulanga, akizungumza katika hafla hiyo.
 Mjasiriamali Habiba Shaban akizungumza.
 Diwani Faisal Hassan, akisalimiana na wananchi baada ya kufika kwenye hafla hiyo.
 Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Hidaya Shomvi akiteta jambo na mgeni rasmi Diwani wa Kata ya Temeke, Faisal Hassan na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Matumbi, Khatibu Lindi.
 Keki ya uzinduzi wa taasisi hiyo ikikatwa.
Halfla ikiendelea


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad