HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, December 31, 2018

WAJUMBE WA NEC WARIDHISHWA NA UTEKELEZAJI WA ILANI KAMISHENI YA UTALII ZANZIBAR

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.
WAJUMBE  wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa Zanzibar wamesema CCM itaendelea kuisimamia Serikali ikusanye kwa wingi mapato bila kuruhusu uvujaji wa rasilimali fedha. Wamebainisha kuwa hatua hiyo itasaidia nchi kujitegemea na kuondokana na mfumo wa kutegemea baadhi ya fedha za wadau wa maendeleo zenye masharti yanayokwenda kinyume na Ustawi wa kijamii na Utamaduni wa wananchi wa Tanzania.

Akizungumza kwa niaba ya Wajumbe hao, Mjumbe wa NEC Ndugu Amini Salmin Amour huko katika Kituo cha ufugaji wa Kasa Mnarani Nungwi, ameeleza kwamba endapo Serikali itazidisha kasi ya usimamizi na ubunifu wa vyanzo vipya vya mapato Zanzibar itakuwa miongoni mwa nchi zenye uchumi mkubwa. Ndugu Amini ameeleza kwamba Sekta ya Utalii ni moja ya Taasisi muhimu zinazochangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi wa nchi kupitia fedha za kigeni.

Alisema lengo la ziara hiyo ni kukagua miradi mbali mbali ya maendeleo inayotekelezwa katika Sekta ya Utalii na maeneo ya Uwekezaji kwa lengo la kushauri na kutoa maelekezo kwa baadhi ya sehemu zenye changamoto za kiutendaji. Aliipongeza Kamisheni ya Utalii Zanzibar kwa utendaji wao mzuri uliochangia kuimarika kwa taasisi hiyo na kufanikiwa kutekeleza kwa kiwango kikubwa Ilani ya CCM.

Pamoja na hayo aliwasihi wananchi kuendeleza Utamaduni wa kufanya Utalii wa ndani ili wajionee vivutio mbali mbali vya utalii vilivyopo nchini pamoja na kufahamu historia na hatua za kimaendeleo zilizofikiwa kupitia Sekta ya Utalii nchini.

Pamoja na hayo aliwapongeza Marais wote wawili ambao ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kudhibiti vitendo vya ubadhilifu wa mali za umma huku wakibuni na kutekeleza mikakati ya ukuaji wa Uchumi wa nchi.

Naye Kamishna wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar  Mhe. Khamis Mbeto amesema kamisheni hiyo kwa sasa tayari imevuka malengo ya Utekelezaji wa Ilani ya CCM iliyoelekeza kuwa ifikapo mwaka 2020 Zanzibar itakuwa na Watalii 500,000 ambapi kwa sasa tayari idadi ya Watalii inakaribia kufikia 600,000 kabla ya mwaka 2020.

Ameeleza kuwa lengo la Kamisheni hiyo ni kutengeneza mazingira rafiki ya kukarabati baadhi ya miundombinu iliyopo katika Vivutio vya Utalii nchini ili wageni na wenyeji mbali mbali wanaotembelea maeneo hayo wawe mabalozi wazuri wa kuendelea kutangaza vivutio hivyo kwa wananchi wengine.

Akieleza mikakati mbali mbali ya kiutendaji inayotekelezwa na Kamisheni hiyo, Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar Dkt.Mohamed Khamis amesema kamisheni hiyo inashirikiana vizuri na taasisi za kimataifa zinazoshughulikia masuala ya Utalii ili kupata mbinu za kisasa zitakazoleta ufanisi wa kimaendeleo ndani ya sekta hiyo.

Aliitaja miongoni mwa mikakati hiyo ni uwepo wa Vituo maalum vya Matangazo na Uratibu wa takwimu na taarifa za masuala mbali mbali ya Utalii katika Viwanja vya Ndege pamoja na Bandari Kuu ya Zanzibar Malindi pamoja na Vituo vidogo vidogo katika maeneo mbali mbali nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Masoko wa Kamisheni hiyo, Dkt. Miraji Ussi, alieleza kuwa kamisheni hiyo inafanya ukarabati mkubwa katika Vivutio mbali mbali vilivyopo nchini hasa katika eneo la Kihistoria linalolojulikana kama Bihole lililopo katika Kijiji cha Bungi katika Mkoa wa Kusini Unguja ili wananchi wa maeneo hayo na maeneo mengine wapate sehemu nzuri ya kutembelea na kufanya shughuli za kibiashara.

Dkt. Miraji alifafanua kwamba mpaka sasa tayari wamekamilisha ramani ya ujenzi wa miundombinu ya kisasa kama Soko la ujasiriamali,hoteli na bustani ya kisasa na eneo maalum michezo ya watoto na makumbusho ambayo itakarabatiwa kwa kufuata vigezo vya awali vya eneo.

Wajumbe hao walitembelea maeneo mbali mbali yakiwemo eneo la Uwekezaji wa Hoteli ya Kisasa ya Verde, Uwanja wa Ndege wa Marehemu Mzee Abeid Amani Karume,Bandari Kuu ya Zanzibar, Eneo la Kihistoria la Bihole pamoja na Kituo cha kufuga Kasa kilichopo Nungwi katika Mkoa.
 BAADHI ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar wakisoma machapisho mbalimbali yanayotolewa na Kamisheni ya Utalii hapo katika Kituo cha mawasiliano, Utafiti na Takwimu cha Kamisheni ya Utalii Zanzibar kilichopo  Uwanja wa Ndege wa Marehemu Mzee Abeid Amani Karume Zanzibar.
 WAJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar wakipatiwa maelezo juu ya huduma zinazopatikana katika ukumbi wa mikutano wa Holeli ya Kimataifa ya Verde iliyopo Mtoni Marine Unguja, katika ziara yao ya kukagua Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020 katika Kamisheni ya Utalii Zanzibar.
 WAJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar wakikagua boti na vifaa vya kisasa vilivyopo katika Hoteli ya Kimataifa ya Verde huko Mtoni Marine Zanzibar.
 MKURUGENZI Masoko wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar Dkt. Miraji Ussi akitoa maelezo ya ramani ya ujenzi wa mradi mkubwa wa miundombinu ya kisasa katika eneo la Makumbusho ya Kihistoria la Bihole lililopo Bungi Mkoa wa Kusini Unguja.
WAJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar wakipatiwa maelezo juu ya Mradi wa Ufugaji wa Kasa uko Mnarani Nungwi, ambapo ni sehemu ya mradi unaoendeshwa na wananchi wakishirikiana na kamisheni ya Utalii Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad