HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, December 20, 2018

TAANET WAIOMBA SERIKALI KUTUNGA SERA JUU YA KUDHIBITI MATUMIZI MABAYA YA POMBE

Na, Khadija Seif, Globu ya jamii
   MTANDAO wa Mashirika ya kupambana na matumizi mabaya ya pombe nchini (TAAnet) imetoa wito kwa Serikali kutunga sera juu ya kudhibiti matumizi mabaya ya pombe katika mkutano uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi zao Mwenyekiti wa Mtandao wa Mashirika ya kupambana na Matumizi mabaya ya pombe (TAAnet) Sophia Komba amepongeza serikali kwa uamuzi waliochukua kutokana na kuzuia na kupiga maarufu juu ya uuzwaji na utumiaji wa pombe aina ya kiroba ambayo ilikua ikiua nguvu kazi ya vijana wengi Kwenye jamii kutokana na kuathirika kiakili na kimwili na kufanya vijana kuwa tegemezi na kutojihusisha na kujenga Taifa hasa kiuchumi.


Komba ameeleza kuwa matumizi mabaya ya pombe inajumuisha pombe za aina zote za kisasa pamoja na za kienyeji ambazo  zina madhara kwa jamii kutokana na kusababisha ajali barabarani, familia kutengana, kusababisha magonjwa kama shinikizo la damu , kisukari, na madhara mengine ya kiafya.


Amesema kuwa "Pombe ya kienyeji inaathiri afya ya watumiaji na watengenezaji kutokana na maandalizi ya kilevi hicho kuwekwa viungo ambayo ni hatarisha kiafya  na kupelekea afya zao kuwadhaifu " amesema Komba .Kwa upande wa Mwenyekiti wa chama cha Afya jamii (TPHA) Dk. Mashombo Mkamba amesema jamii inaathirika sana kutokana na matumizi mabaya ya  pombe na Kwa sasa hata baadhi ya wajawazito wanajihusisha na unywaji wa pombe tatizo linalopelekea hata kizazi kitakachozaliwa kuathirika sehemu za ubongo .

Hata hivyo Mkambala ametoa ufafanuzi juu ya magonjwa ambayo siku hadi siku yanazidi kukua kwa kasi kutokana na unywaji wa pombe kama saratani, kisukari, shinikizo la damu pamoja na maambukizi ya UKIMWI kutokana na kukosa umakini wakati wa wanywaji  wanapokutana kimwili na kufanya ngono zembe pasipo kumakinika pindi pombe inapowazidia (kulewa).


Amefafanua kuwa "kwa sasa mnywaji hatoweza kuona madhara ya kiafya kwa haraka lakini kadri siku zinavosonga ndo jinsi miili yetu inazidi kushambuliwa na magonjwa na hata kupeleka kuhatarisha maisha kiujumla" ameeleza.


Aidha amesema kuwa ni vizuri serikali ikatunga sera ambayo itasaidia jamii kupiga vita kabisa unywaji wa pombe unaohatarisha maisha au usio salama ili kupunguza vifo vitokanavyo na matumizi mabaya ya pombe kwani vifo vingi vinatokana na pombe, japo baadhi ya Mashirika yanisisitiza kunywa pombe kistaarabu.


Aidha Katibu wa Mtandao wa kudhibiti matumizi mabaya ya pombe (TAAnet) Alistair Elias amefafanua zaidi kuwa Mtandao umeweza kushirikisha viongozi wa dini ili kutoa elimu na kuwahimiza watu kuacha pombe ili kuweza kusukuma gurudumu la maendeleo katika jamii na Taifa kiujumla kwani mtandao peke yake hawawezi kutoa elimu na kufikia kwa asilimia zote.


Elias ametoa wito kwa Serikali kuendelea kupiga vita unywaji wa pombe aina ya gongo ambayo kwa sasa viungo ambavyo vinawekwa ndani yake si salama na havina viwango kwa afya ya watumiaji hasa kwa Wakazi wa vijijini ambao hutumia na elimu juu ya athari zake bado hazijafika kwa kasi zaidi.


Na amesema kuwa "Jamii na Taifa kwa ujumla ikiwa na watu ambao wanaipa kipaumbele matumizi yasio salama ya unywaji wa pombe lazima tutaendelea kuzalisha vifo vitokanavyo na ajali  zinayosababishwa na madereva walevi pia masuala ya ukatili wa kijinsia, ubakaji na vitendo vibaya vya utovu wa nidhamu kutokana na ulevi uliopitiliza" alisema Elias

Na pia  Elias amefafanua kuwa Mtandao wa kudhibiti matumizi mabaya ya pombe  (TAAnet) ipo kwa ajili ya kutoa elimu juu ya kuacha pombe na kudhibiti matumizi mabaya  pombe na kuleta usawa katika jamii.
Mwenyekiti wa Mtandao wa kudhibiti matumizi mabaya ya pombe (TAAnet, Sophia Komba akizungumza na waandishi wa habari kuhusu athari zitokanazo na matumizi ya pombe uliofanyika katika ofini kwao leo jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Chama cha Afya ya jamii (TPHA) Dk.Mashombo Makamba akizungumza na waandishi wahabari kuhusu magonjwa yanayoshamiri kwa sasa na matumizi ya pombe kuwa kisababisho kikubwa

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad